Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote mimi nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, tarehe 23 alitutembelea sisi Wana-Hanang’ na alikuwa kwetu mpaka tarehe 26 akijaribu kuhamasisha maendeleo ndani ya Mkoa wa Manyara. Akiwa kule alileta salamu za Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdori Mpango. Hakuja hivi hivi, alikuja kueleza zile neema ambazo zimekuja kwenye mkoa wetu na kwenye Wilaya yetu, ya madarasa kwenye shule shikizi pamoja na shule za sekondari, kwenye sekta ya afya pamoja na sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati alipokuwa Hanang’ aliwaahidi Wana-Hanang’ mambo kadhaa. Ninachoomba tu mimi nilivyosimama hapa salamu zile za shukurani za Wana-Hanang’ lakini kukumbusha tuu mambo machache kati ya yale ambayo Wanahanang walimuomba.

Mheshimiwa Spika, Hanang’ ni Wilaya kongwe; Mji wa Katesh ni Mji wa muda mrefu lakini changamoto kubwa ni ya maji. Tunashukuru tangu tumeanza na watu wa BAWASA wanafanya kazi nzuri sana; kabla tulikuwa tulikuwa na KAWASA. Hata hivyo wanayo changamoto, fedha za mabomba zilizoahidiwa hazijafika; bado fedha za kutekeleza ule mradi hazijafika. Tunaomba sana hizo fedha zitolewe kwa wakati ili Mji wa Katesh uweze kupata maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi wa Maji wa Gehandu ulioahidiwa na Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni. Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Sita, Mama Samia Suluhu Hassan alisema kwamba yeye akisema inatekelezwa na kweli imetekelezwa. Mkataba wa bilioni 2.8 umeshasainiwa. Tunachoomba; mwaka huu maji ni changamoto kubwa, mvua ni chache wananchi wa Gehandu wako milimani. Ili wapate nafuu huu mradi uliosainiwa wakandarasi waende kwenye site kwa wakati ili waweze kuwasaidia wananchi hao wasipate changamoto kubwa ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mradi mkubwa wa maji kutoka katika Ziwa Basutu. Kwenye eneo hili, niwapongeze na kuwashukuru sana wadau wa maendeleo wa Water Aids walitoa milioni 500. Serikali kupitia fedha hizi tulizozikopa kupitia World Bank milioni 550 zimeenda pale, lakini kabla zilienda milioni 70; ni mradi wa bilioni 12 kwa vijiji zaidi ya 9. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali yangu iuangalie mradi huu kwa jicho la kipekee. Lakini na hao wadau wanaotusaidia waweke nguvu zaidi ili tuhakikishe kwamba wananchi wale ambao bado hawajafikiwa wawe wamefikiwa.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mji wa Katesh wakati ule wa kampeni tuliwaahidi kilometa 10 za lami. Nilimuomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati alivyokuja kwenye jimbo letu, kwamba, kwenye bajeti hii tunayoenda 2022/2023 atupe angalau, au atupiganie kupata kilomita nne za lami ili tupunguze ile 10 aliyoahidi mama tukiwa tunaelekea kwenye 25 wakati wa kuomba kura, Wanahanang tumewaahidi lami kidogo kidogo kwa kipindi kirefu. Tukiwapa nne halafu tukaanza kidogo kidogo, kama tukienda na mbili mbili tutakuwa tumeenda zaidi. Ukifikia asilimia 70 utakuwa umefaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba sana, kwenye eneo hili ni kwamba, tupate hizo kilometa nne kwenye bajeti hii ya 2022/2023 ili tuendelee na hizi ahadi ambazo zimetolewa tangu mwaka 2010 ili zianze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tuna barabara yetu ya Katesh - Masutu - Haydom. Ukifika Mlima Chavda pale changarawe ile inatereza, tunamwaga ngano nyingi sana pale. Tusaidiwe kwenye eneo hilo, barabara ile iwekwe lami, ni kilometa 70 tu.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana Mheshimiwa Flatei alitaka kupiga sarakasi kwenye eneo hili. Ninaomba tusifike kwenye hatua ya kupiga sarakasi, kazi hii ifanyike kwa sababu ni ahadi ambayo imetolewa wakati wa uchaguzi na tumeihaidi kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2020/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tuna barabara ya Nangwa – Gisambalang – Kondoa. Kwa sasa barabara ile imekatika kabisa, mvua ikishanyesha haipitiki kabisa. Hakuna shughuli inayoendelea kwenye kata zaidi ya sita. Barabara hiyo ndiyo inayounganisha Wilaya ya Hanang na Wilaya ya Kondoa. Tunazo Kata za Gisambalang, Dirma, Simbay, Sirop, Kata ya Wareta pamoja na Kata yenyewe ya Nangwa. Kote huko wananchi wangeweza kupita katikati tu hapo ambapo ni kilomita kama 50, lakini wanalazimika kutembea zaidi ya kilometa 200 kufanya shughuli zao za kiuchumi. Tunaomba Serikali itusaidie kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, katika barabara hiyo daraja limeondolewa na mafuriko ya mvua ya 2019/2020. Tuliamini lingekuwa ni suala la dharura, lakini mpaka sasa Daraja la Munguri B halijatengenezwa. Ukitaka kupita pale mvua ikinyesha uombe Mungu upite. Tumekuwa tukipata changamoto kubwa kwaajili ya eneo hilo, tunaomba tupate usaidizi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba nisemee kidogo uchumi wa Wilaya ya Hanang’. Sisi tunategemea kilimo na ufugaji. Kwenye eneo la mifugo kwa kipindi kirefu tulikuwa na malambo ambayo yamejengwa kwa ajili ya kusaidia kunyweshea mifugo, ikiwa ni pamoja na changamoto nyingine ya malisho. Malambo yale yaliyojengwa mengi ni ya muda mrefu, yamechakaa, ni ya tangu mwaka 1980. Serikali iangalie namna ya kukarabati na kujenga.

Mheshimiwa Spika, tunalo Lambo la Gidahababieg ambalo Serikali kwa kipindi kirefu imeahidi kwamba lile lambo litaboreshwa kwa sababu mkondo ule una maji mengi. Kwamba watajenga bwawa kubwa ambalo pamoja na mifugo kupata maji, vilevile litasaidia wananchi kufanya umwagiliaji. Tunachoomba kwenye eneo hilo Serikali sasa itupie jicho la ziada.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye hotoba yake, ukurasa wa 24, amesisitiza sana suala la kilimo. Kwamba kilimo chetu ili kiende tunahitaji mbolea, mbegu za kisasa pamoja na viuatilifu. Ninachoomba kwenye eneo hili, tuwasaidie wananchi wa Hanang’.

Mheshimiwa Spika, kwenye hotoba ya Mheshimiwa Rais wakati anazindua Bunge hili la 12 alisema tuna nakisi ya tani laki nane mpaka milioni moja za ngano; na Hanang’ ilikuwa maarufu sana kwenye kilimo cha ngano. Tuliangalie eneo hili ili tuboreshe kilimo cha ngano, tuache kuagiza ngano kutoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na mashamba yale ya NAFCO. Mashamba yale mpaka sasa kwenye yale maeneo ambayo yamemilikishwa kwa wananchi, wakulima wakilima wanapata kati ya gunia nane mpaka 12. Sasa, tunazo ekali zaidi ya 42,000 tumemmilikisha mwekezaji. Mwekezaji huyu yeye akijitahidi sana yeye anapata kati ya gunia tano mpaka sita. Mwekezaji huyo, si wananchi wa kawaida ambao hawatumii mbolea, wananchi wa kawaida ambao wanalima kwa njia za kawaida za asili. Sasa naomba tufanye tathmini ya kina kwenye eneo hilo. Je, mwekezaji huyu bado tunahitaji kuwa naye?

Mheshimiwa Spika, kwa hekari 43,000, kwa hesabu za kawaida ambazo mimi nimezifanya, yeye akilima kwa namna ambayo analima kwa sasa, tunapata kati ya gunia 219,800 mpaka 263,000. Lakini wangepewa wananchi wa kawaida wa Hanang’ wangeweza kuzalisha kati ya 351,000 mpaka 439,000, wananchi wa kawaida ambao hawatumii mbolea, ambao wanatumia kilimo chao cha asili. Ukienda kwenye vyama vya ushirika ambao wanapata misaada mbalimbali kutoka maeneo kadhaa ikiwepo benki yetu ya kilimo wanaweza kuzalisha kati ya gunia 527,000 mpaka 659,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kazi ya kufanya kwenye eneo hilo. Ninachoomba ndugu zetu wa Wizara ya Kilimo, hao wenzetu ambao wamepewa haya mashamba, wapewe shamba moja tu kati ya mashamba yale ambayo wamepewa, yale mengine wapewe wananchi hao wa kawaida ili waweze kulima kwa namna ambavyo wanaona au vinginevyo wapewe vyama vya ushirika ili tuzalishe kwa tija na ili waweze kusaidia Wilaya ya Hanang’ kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushuruku sana. Ahsante sana. (Makofi)