Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kama walivyotangulia kuongea wenzangu napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu, Bunge lako Tukufu pamoja na Wabunge wote kwa namna ambavyo kwa pamoja tunashirikiana katika kuhakikisha kwamba miradi ya maendeleo inatekelezwa vizuri inasimamiwa vizuri na tunaishauri vizuri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru zaidi Mheshimiwa Rais kwa sababu ameweza kutenga fedha nyingi katika mwaka wa fedha huu tunaoumaliza ili kuhakikisha kwamba miradi mingi inakwenda na kwa kweli inakwenda, kwa kweli nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kujikita katika maeneo machache sana leo katika kuchangia kwenye bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza ningependa kuzungumzia miundombinu ya barabara pamoja na madaraja, ninaanza kwanza na barabara kuu.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na barabara nyingi ambazo zimefanikishwa na Serikali kujengwa na madaraja mengi kama hayo ya Tanzanite, barabara ya njia nane kutoka Ubungo kwenda Kimara mpaka Kibaha, lakini kule kwenye barabara ya Kilwa Serikali imefanya kazi kubwa sana kuanzia pale gerezani kwenda mpaka bandarini, kwenda mpaka rangi tatu kuna kilometa 20 pale kazi inakwenda moto moto katika kuhakikisha kwamba barabara ya mwendo kasi inajengwa kwa speed kubwa ili kuwaondolea adha wananchi ambao wanakwenda Mikoa ya Kusini ya Lindi, Mtwara Ruvuma mpaka Njombe siku hizi wanatumia barabara ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna shida katika eneo la kutoka pale Rangi Tatu eneo wanaita Tanita kwenda kutokea pale Kongowe kuna shida kubwa, kuna kipande pale cha kilometa kama 12 hivi kimesahaulika, kile kipande tangu enzi za hayati Rais wetu wa Serikali ya Awamu ya Tano alipokuwa Waziri wa Ujenzi kile tayari kililengwa kujengwa kwa kiwango cha lami barabara nne mbili zinakwenda mbili zinarudi matokeo yake leo ni zaidi ya miaka 10 sasa hivi, diversion zimewekwa kwenye barabara ile sasa zinaota nyasi na kuota miti bado barabara ile haijaanza kujengwa toka pale Tanita kwenda Kongowe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaiomba Serikali katika bajeti ya Mwaka 2022/2023 tuweze kuijenga ile barabara kwa kiwango cha lami njia nne ili kupunguza adha ambayo inawakuta wananchi ambao wanakwenda kwenye Mikoa hiyo niliyoitaja.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli barabara ile ikifika asubuhi wakati watu wengi wanakwenda katikati ya Jiji au wakati wa jioni wakati watu wanarudi majumbani kwao, kwa kweli imekuwa na adha, kipande kile cha kilometa 12 watu wanatumia masaa matatu hadi manne pale foleni ilivyokuwa imekaa vibaya, kwa hiyo naomba sana Serikali iangalie ile barabara ikiwezekana kwenye bajeti ya 2022/2023 basi iweze kufanyiwa kazi.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nikienda kwenye upande wa TARURA naishukuru Serikali pia kwa kazi kubwa ambayo imefanya ya kuongeza fedha hasa zile za maendeleo kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya barabara, lakini nilikuwa na rai kwenye upande mmoja. Barabara zile pamoja na kwamba zimekuwa zikiletewa fedha nyingi na Serikali tena kwa wakati lakini taratibu za manunuzi zimekuwa zikichelewa sana kiasi kwamba hadi mvua kubwa za mwisho wa mwaka na mwanzo wa mwaka zinapoanza unakuta bado miradi haija-take place kwa sababu zabuni inatangazwa katikati ya mwaka wa fedha, kwa hiyo, unakuta kipindi kama hiki sasa ndiyo wanahangaika sasa kuchakarika kuweza kutengeneza barabara wakati fedha zilishakuja muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba Serikali isimamie TARURA ili iweze kutengeneza utaratibu ili angalau 60 percent ya zabuni ziweze kutangazwa kipindi kama hiki ili mwaka unapoanza wa utekelezaji wa miradi mwezi Julai basi tuweze kuendelea vizuri bila shida ili hiyo asilimia 40 inaweza ikatangaza zabuni zake baadaye kama ambavyo wanafanya wenzetu wa TANROADS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia ningeomba Serikali itenge fedha za dharura kwaajili ya TARURA. Nchi yetu miaka ya karibuni imekuwa na bahati nzuri ya kuwa na neema ya kuwa na mvua nyingi, na matokeo yake kwa kuwa miradi inachelewa lakini vile vile kwa kuwa fedha za emergency hazipo basi inapofika mahali imetokea mvua kubwa, madaraja, makalavati yamebomoka inakuwa shida kupata fedha za kurekebisha hali inayojitokeza kwa haraka ya uvunjifu makalavati na madaraja hayo.

Mheshimiwa Spika, kwahiyo ningeomba Serikali itenge pia fedha za dharura ili ikitokea emergency basi mara moja fedha ziweze kwenda na TARURA iweze kuchukua nafasi na kufanya kazi yake sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, ningeomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya miradi maalum. Kama walivyotangulia kuongea baadhi ya Wabunge wenzangu siku ya leo, kwamba kuna baadhi ya maeneo kwenye baadhi ya majimbo kuna mabonde makubwa. Mimi pia pale kwangu, katika Jimbo langu, kuna bonde la Mto Hanga kutoka Kinjumvi kwenda Mtialambuko, lina urefu wa zaidi ya kilometa tano, ambapo wakati wa mvua maji yanajaa sana. Kwahiyo katika miradi kama ile unaweza ukakuta ukitegemea ile bilioni 1.5 ya maendeleo unaweza ukajikuta hela yote inazama kwa ajili ya kujenga tuta na kujenga daraja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwahiyo nilifikiri kwamba Serikali itafute vyanzo vya ziada ili tupate hela za ziada kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa kama ile ambayo inahitaji fedha nyingi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni la pembejeo. Kumekuwa na shida katika mwaka uliopita, lakini nimefurahi Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu wake hivi karibuni walikuja na ajenda ya 10/30 ambayo inaonekana itakuwa muarubaini sasa kwenye mambo ya pembejeo na miundombinu mingine ya uendeshaji wa shughuli za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kwakweli hali ilikuwa mbaya kutokana na changamoto ambayo imeelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya uwepo wa COVID 19. Hata hivyo bado Serikali inatakiwa iweke mkakati wa kudumu wa kuhakikisha kwamba changamoto ya upatikanaji wa mbolea pamoja na pembejeo isiwe endelevu ili tutatue hii changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano mwaka jana msimu uliopita tulikuwa na ununuzi wa mbolea aina ya urea ambayo ilifikia wastani wa shilingi 104,000 kwa pakti moja, mbolea ya aina ya sulpher iliuzwa mpaka shilingi 86,000. Wakati huo huo kwa wakulima wa mahindi walio wengi, Serikali ilinunua gunia moja kwa shilingi 55,000. Kwahiyo unaweza ukaona namna ambavyo wakulima wetu wanavyoumia, hasa wale ambao hawapewi ruzuku za bure. Tunaishukuru Serikali msimu uliopita kwa zao la korosho walitoa ruzuku ya bure, lakini kwa mazao mengine ilikuwa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumepata promise ya Mheshimiwa Waziri kwamba mazao mengine ya kimkakati nayo yatasaidiwa. Basi pale ambapo itashindikana tujitahidi kudhibiti hizi bei za pembejeo, hususani mbolea, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanalima kilimo chenye tija ili kuusukuma mbele uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini nikienda kwenye uvuvi na mifugo; tumeanza kupata ahueni kupitia ajenda 10/30 kule kwenye kilimo. Wataalam wetu wa mifugo na uvuvi wamekuwa na shida ya vyombo vya usafiri. Wale wa kilimo tayari wameshapewa pikipiki 6,704. Naomba Serikali ielekeze jicho lake sasa kwa wataalam wetu wa mifugo na uvuvi ili nao waweze kupatiwa vitendea kazi hususani hivi vitendea kazi vya usafiri na hizo kits za kufanyia kazi katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile ningependa niiombe Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo na benki nyingine ambazo zinatoa mikopo ziwafikie wakulima, wavuvi na wafugaji wadogo kwa sababu wakulima, wavuvi na wafugaji wakubwa ndio wamekuwa wakipata mikopo hii kwa wingi. Na kwa sababu wao wana mitaji, wana uwezo wa kuajiri mtu wa kuandika maandiko; na kwa sababu masharti ni magumu na very complicated kiasi kwamba hayawezi kuwa attained na wale wafugaji, wakulima wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba tuwe na special funds. Kwamba, tunaweza tukaanzisha mfuko maalum wa maendeleo kwa ajili ya wakulima, wavuvi pamoja na wafugaji wadogo ili hata yule mkulima mwenye heka tatu aweze kunufaika na mikopo hii. Kwa sababu kwa hali iliyopo sasa hivi ni ngumu, kuna taratibu nyingi ambazo zinawafanya wale wakuliwa wasiweze kupata mikopo hiyo. Kwa hiyo ningeomba kwamba turekebishe, tushirikiane na watu wa vyama vya ushirika, tushirikiane na watu wa halmashauri; na ikiwezekana taratibu zake zifanane fanane na zile asilimia 10 zinatolewa na halmashauri ili kuwarahisishia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FRANCIS K. NDULANE: …wakulima, wavuvi na wafugaji kupata hiyo mikopo ili waweze kuboreshewa zana zao za kufanyia kazi, waweze kuchakata mazao vizuri, lakini vile vile waweze kuongeza thamani ya mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.