Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kukupongeza wewe binafsi kwa kuliongoza Bunge letu Tukufu lakini kwa kuaminiwa na Waheshimiwa Wabunge tuliomo ndani ya Bunge hili na kuweza kukaa kwenye Kiti ambacho umekaa hapo mbele. Na tunafarijika ukiwa hapo unatuongoza ndani ya Bunge letu Tukufu, Mungu akubariki sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutuletea bajeti ambayo sasa hivi tunaizungumza na tunaijadili katika Bunge hili lakini kutuletea matumaini katika uwekezaji wa uchumi wa viwanda na maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, nitumie kwa dhati kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anachapa kazi lakini kwa namna ambavyo ametupatia fedha nyingi katika Majimbo yetu kutekeleza miradi mbalimbali. Tumeshuhudia miradi ya ujenzi wa madarasa katika sekta ya elimu katika madarasa ya shule ya msingi sekondari na mengineyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na hata Hospitali za Mikoa pamoja na Hospitali za Rufaa. Pia tumeona namna ambavyo barabara zetu zimeendelea kuimarishwa kuboreshwa kupitia TARURA pamoja na mambo mengine. Pamoja na hayo yote mazuri ambayo yameendelea kufanyika katika Majimbo yetu, lakini bado tunazo changamoto mbalimbali na sasa tunaomba Serikali isimamie katika kuhakikisha kwamba changamoto hizi zinapungua ama zinaondoka kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la elimu tuna changamoto upande wa shule zetu za sekondari kukosa nyumba za Walimu, hii imekuwa ni changamoto kubwa sana na hasa kule vijijini Mwalimu anapokaa kwenye nyumba ambayo haina hata umeme namna ya kuandaa masomo yake ambayo anategemea siku ya pili aende akayafundishe darasani inakuwa ni changamoto. Ningeiomba Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha kuhakikisha Walimu wanapata nyumba bora za kuishi na kuwatia moyo kuendelea kusimamia masomo yao madarasani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunayo changomoto upande wa barabara. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais ametupatia fedha nyingi katika kuboresha barabara zetu lakini bado tunayo changamoto kubwa hasa katika eneo la Lindi mjini. Zipo barabara hizi zina miinuko na mabonde kwa hiyo, uwekekaji wa kifusi katika barabara zile upo tofauti na barabara tambarale. Kwa hiyo, gharama kubwa inahitajika ya fedha katika kuhakikisha kwamba wanaimarisha barabara zile ziweze kupitika wakati wote wa kifuku na kiangazi.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaiomba Serikali kuwaongezea bajeti ndugu zetu wa TARURA waweze kusimamia kuboresha barabara zetu na ziweze kutumika vizuri lakini tujipange katika uwekezaji ambao wananchi wetu wanategemea kuwekeza katika maeneo yao. Tusipoimarisha barabara zetu uwekezaji utakuwa ni mgumu sana.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna sekta ya nishati. Katika eneo la Lindi Manispaa tumepitiwa na bomba la gesi linalotoka Mtwara kwenda Kinyerezi kule Dar es Salaam na walinzi wakubwa wa miundombinu ile ni wananchi katika maeneo husika ambayo bomba hili limepita. Lakini tunayo changamoto wananchi wetu wa Lindi Manispaa, Lindi Mjini na Jimbo la Mchinga unaposema upo Manispaa halafu unakosa umeme, mwananchi hakuelewi. Kwa hiyo, tunayo changamoto kubwa katika maeneo yetu ya baadhi ya maeneo kukosa miundombinu ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumejaribu kuongea sana na Serikali inatuambia kwamba tuna mradi wa peri-urban unaokuja, sasa mwaka wa tatu hatujaona mradi wa peri- urban. Sasa ninaomba Waziri atuambie ni lini mradi wa peri- urban utakuja Lindi Manispaa kuhakikisha kwamba wananchi wa eneo la Lindi Manispaa wanapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa katika vijiji ambavyo vimepitiwa na bomba la gesi, wananchi wale waliahidiwa kwamba asilimia ya mapato yatarudi kuja kuwekeza katika shughuli za maendeleo katika maeneo husika, lakini tangia bomba lile limepita wananchi tunaendelea kulinda hatujaona hata Shilingi Moja inakuja kwetu Lindi Manispaa kuwekeza katika miradi ya maendeleo, nalo watuambie ni lini watatuletea fedha hii ije kutekeleza miradi ya maendeleo Lindi Manispaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuna mradi wa LNG ambao tunatarajia kwamba Lindi katika Kata ya Mbanja kule Likong’o utakuja kutekelezwa, lakini wananchi wanashangazwa vikao vyote vinafanyika Arusha why visifanyike Lindi Mjini? kuna tatizo gani wananchi wanakiu kubwa ya kuona vikao vinavyojadili suala la mradi wa LNG vinafanyika katika eneo la Lindi Mjini, Lindi Manispaa. Kwa hiyo, ni matarajio yetu ya kwamba vikao hivyo vinavyoendelea Arusha sasa virudi vigeuke kuja Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hayo tu tunataka mashirika haya ambayo yanakuja kuwekeza yaweke ofisi zao pale Lindi Mjini, tuone shughuli sasa zinaendelea lakini hata Shirika la TPDC waweke Ofisi pale Lindi Manispaa, ile kusafiri kila wiki wako Dar es Salaam wako Lindi sisi hatufurahishwi tungependa kuona kwamba Shirika la TPDC linaweka Ofisi Lindi majengo yapo, maeneo ya kujenga Ofisi yapo, tunawakaribisha waje Lindi kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la Kilimo. Nimefurahishwa sana na hotuba mbalimbali zinazoendelea hivi punde nimetoka katika kikao pale cha Bodi ya Korosho namna ambavyo Mheshimiwa Bashe anatutia moyo katika kuleta mapinduzi makubwa katika mazao yetu ya biashara hasa katika zao hili la korosho. Kwa hiyo, nishukuru sana lakini niendelee kumpongeza nimtakia kheri katika mapinduzi yale makubwa ambayo tunatarajia kuyapata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imezungumzia suala la Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Sasa kushuka kwa wakulima wadogo wadogo tumeona ya kwamba benki hii imewawezesha wakulima wakubwa, sasa tunahitaji wakulima wadogo wafikiwe na benki hii. Tusipomuwezesha mkulima kupata fedha ya kuwekeza kwenye mashamba yake, kilimo chao kitakuwa hakina tija miaka nenda rudi, tunajua ya kwamba Serikali inatupatia Sulphur, pembejeo bure lakini pembejeo ile wasipokuwa na fedha ya kuendelea kwenda kuwekeza katika mashamba tutakuwa bado hatujawasaidia.

Mheshimiwa Spika, Wakulima wetu hawakopesheki kwa sababu hawana Hati Miliki ya mashamba yao kwa hiyo, ninaiomba Serikali kuhakikisha kwamba sasa tuwarathimishe wakulima wetu waweze kupata Hati Miliki na waweze kuingia kwenye vyombo vya fedha waweze kupata fedha na waweze kuendelea kuwekeza katika shughuli za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la miradi ya kimkakati, muda mrefu sasa yapata miaka minne tumeomba fedha kutoka Serikali Kuu kutuwezesha kujenga soko jipya, soko la kisasa lakini kujenga stendi mpya ya mabasi ya kisasa. Katika Manispaa pekee haina stendi ya kisasa ni ya Lindi Manispaa. Inasikitisha sana mwaka wa Nne sasa tunafuatilia hakuna kinachopatikana, ninaomba wakati wa ku-windup Waziri husika atuambie kuna tatizo gani la kutotupatia fedha kwa ajili ya uwekezaji wa ujenzi wa soko jipya la kisasa lakini pia ujenzi wa stendi kuu ya mabasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la Wenyeviti wetu wa Serikali za Mitaa, Wenyeviti hawa wanafanya kazi kubwa sana na wanatusaidia sana katika kuimarisha ulinzi na usalama, lakini haijatokea hata siku moja tukawanunulia vitendea kazi. Kila kazi wanafanya kwa pesa yao lakini mapato wanayoyapata ni madogo sana. Ninaiomba sana Serikali kuangalia kwa jicho la huruma Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba Posho yao wanaongezewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaomba kuunga mkono asilimiamia moja. Ahsante sana. (Makofi)