Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu wake kwa kazi kubwa waliyoifanya; na kwa sababu Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni Wizara pacha na Wizara ya Afya lakini ukienda katika Wizara ya Elimu, Wizara ya Maji unaikuta TAMISEMI inazungumzwa muda wote; na ukiangalia michango mingi sana imejilenga katika suala zima la uboreshaji wa huduma za afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirejea mchango wa Kamati ambao maelekezo yake kwa kiwango kikubwa na michango ya baadhi ya Waheshimiwa Wajumbe wengi sana walipendekeza ikiwezekana mambo ya afya yote yabakie katika Wizara ya Afya, ambalo hili nimeona watu walikuwa wakipendekeza kwamba itoke TAMISEMI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nifanye rejea kidogo katika Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 1977, nawaomba Waheshimiwa Wabunge ikiwezekana turejee katika Katiba, Ibara ya 145 na Ibara ya 146 yenye kuweka utaratibu wa Serikali za Mitaa, lakini vile vile Ibara 146 ikizungumza majukumu ya Serikali za Mitaa. Hili lina umuhimu mkubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hapa kuna ajenda moja ya msingi ambayo tunatakiwa kama Wabunge tuiangalie kwa pamoja, tuone jinsi gani tutafanya kuweza kupata fedha za kutosha kuhakikisha tunahudumia huduma za afya. Hili ndilo jambo la msingi. Kwa sababu hata ukichukua mambo yote ukipeleka Wizara ya Afya; leo hii tunapozungumza deni hata la MSD halipo TAMISEMI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sugu alikuwa anazungumzia suala zima Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kwamba haiko TAMISEMI. Maana yake ni nini? Ni kama Taifa, kama Serikali sasa hivi inavyojipanga ya Awamu ya Tano kutafuta fedha kwa kadiri iwezekanavyo kutoa huduma za kijamii katika jamii yetu, hilo ni jambo la msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niseme kwamba, kama Wabunge tujiandae vya kutosha tuone jinsi gani tutaimarisha Sekta ya Afya. Tutaimarisha Sekta ya Afya katika kuhakikisha tunafanya kila liwezekanalo kutafuta fedha nyingi za kutosha kuhudumia miradi ya afya. Hili tukilifanya vizuri, maana yake ni nini? Ukizungumza kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI, walioajiriwa zamani wanafahamu. Leo hii mhudumu wa afya au nurse yuko Kigoma au yuko Kibondo, umwambie siku ya kupandishwa daraja lake, maana yake ni mpaka aende Makao Makuu ya Wizara. Ndugu zangu, tutazalisha matatizo makubwa kuliko tanayoyaona hivi sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuseme, ninyi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi, naamini kila Mbunge alishiriki katika bajeti ya Halmashauri yake na kila Mbunge aliainisha vipaumbele vyake vya ujenzi wa zahanati na vituo vya afya na kila Mbunge aliweka kipaumbele chake cha ununuzi wa gari la wagonjwa, halikadhalika Hospitali ya Wilaya, lakini bajeti ni mchakato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaanza katika ngazi za Vijiji, unakuja katika ODC, inakuja katika Halmashauri, inaenda katika Wizara, lakini mara nyingi sana tunazungumza ukomo wa bajeti. Ukomo huu wa bajeti tusipoweka nguvu za kutosha za ukusanyaji wa kodi, maana yake hapo tutakwama. Kwa hiyo, nataka niwashawishi Waheshimiwa Wabunge, kwamba katika ile ajenda ya kufikiria kwanza saa nyingine tuiondoe yote, ina maana kwanza tunakuwa tumevunja Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa Ibara 145 na Ibara 146. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata watumishi tunaowahudumia ambao wako vijijini itakuwa ni changamoto kubwa, itakuwa ni mzigo mkubwa sana, tutakuja kumlaumu hapa Waziri wa Afya kwamba kuna watumishi wako, wako kule Kibondo, Mtwara au wapi, hawajapanda madaraja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utaratibu utakuwa mzuri, kama fedha zitakuwa zinapatikana vizuri, naamini tuta-empower Mabaraza yetu ya Madiwani, yatafanya maamuzi sahihi zaidi katika kuweka vipaumbele vya kuhakikisha Sekta ya Afya inakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwashawishi Waheshimiwa Wabunge hapa, haya mambo kwa sababu naamini Wizara ya Afya kama ni regulator, yeye anasimamia sera na anasimamia hospitali za Serikali, halikadhalika katika sekta binafsi, jambo hili tukiliweka vizuri hasa katika kutafuta rasilimali fedha halafu kuzisukuma chini katika Halmashauri na kwa sababu kuna mfumo uliokamilika kwa…