Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuchangia. Awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu ya kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Pia nichukue nafasi hii kipekee kuishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri zinazofanywa chini ya mama yetu Samia Suluhu, hasa hasa kuleta pesa nyingi ya maendeleo kwa wananchi wetu. Ni ukweli usiopingika pesa inakuja na miradi inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nataka nizungumzie kwanza upandaji wa bidhaa. Ni vizuri tukaeleza hapa ukweli. Nilikuwa najaribu kufuatilia taarifa za EWURA; ukifuatilia taarifa za EWURA mara nyingi Waheshimiwa Mawaziri na wengine wamekuwa wakisema bidhaa zimepanda kwa sababu ya mafuta. Hebu tuangalie taarifa za EWURA zinasemaje kuanzia mwezi wa 12 mpaka sasa.

Mwezi wa 12 mwaka jana bei ya mafuta kwa Dar es Salaam ilikuwa ni shilingi 2510 na kwa Kigoma kule Uvinza ilikuwa ni shilingi 2754 mwezi wa pili mwaka huu bei ya mafuta ilishuka ikawa shilingi 2480 kwa Dar es Salaam na kule Uvinza Kigoma ikawa 2720, maana yake ilishuka kwa shilingi 30. Tukaja mpaka mwezi wa tatu bei ya mafuta ilikuwa ni shilingi 2500 kwa Dar es Salaam mpaka 2784 kwa Uvinza kule Kigoma.

Sasa Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wanaotusikiliza lazima tueleze ukweli. Bidhaa zilizopanda mimi niseme ukweli hazitokani na upandaji wa mafuta. Kwa sababu ukija kuangalia hapa hizi takwimu za EWURA haiwezekani hii shilingi 60 ambayo imepanda kwenye soko la mafuta ndiyo iongeze bei kiasi hiki. Mimi nitoe mfano, kule kwangu kuna sabuni mbili tunazozitumia, kule Kyerwa. Sabuni ya nyota mwezi Januari ilikuwa inauzwa shilingi 1,000 lakini mpaka sasa ile sabuni inauzwa shilingi 3,500. Sabuni ya mkwano ilikuwa inauzwa shilingi 2,000 leo hii hiyo sabuni inauzwa shilingi 5,000. Hivi hii shilingi 60 iliyoongezeka kwenye soko la mafuta ndiyo imepandisha bidhaa kiasi hiki?

Mheshimiwa Spika, lakini ukija kwenye mafuta ya kula ni jambo ambalo ni la ajabu. Mafuta yaliyokuwa yanauzwa shilingi 1,700 leo hii haya mafuta ni shilingi 3,500. Yaani hii haikubaliki. Ukienda kwenye vifaa hivi vya ujenzi, mimi mwaka jana mwezi wa 12 niliagiza pale kwenye vifaa vya ujenzi vya aluminum; pale nilivyoagiza wakanipa quotation ya shilingi milioni 18. Nimekwenda juzi wananiambia hivyo vifaa bei imebadilika ni milioni 35. Waheshimiwa Wabunge na Watanzania lazima tuwaeleze ukweli. Suala la kusema mafuta yamepanda tuongee tarehe sita juzi, siyo miezi hii miwili mitatu iliyopita, hili haliko sawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ninachokiona kwenye suala la upandaji wa mafuta tunaongelea kipindi hiki cha juzi, lakini miezi mitatu kule nyuma mafuta yalikuwa hayajapanda kiasi hiki cha kuweza kupandisha bidhaa zikapanda namna hii hili haliko sawa. Mimi nilichokiona baada ya kufuatilia hawa wanaouza wameachiwa uhuru wameamua kujitawala kufanya wanavyotaka.

Mimi niombe tumsaidie Mheshimiwa Rais, tusiende na hoja ya kusema bidhaa zimepanda kwa sababu ya mafuta. Leo hii tukianza kutangaza sawa kwa sababu mafuta yameongezeka takriban kwa 500 zaidi. Kwa hiyo mimi ninapinga suala la kusema bidhaa zimepanda kwa sababu ya mafuta kupanda.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilisemee ni kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa maamuzi ambayo ameyafanya kule Kagera kwenye suala la kahawa. Kwa uchumi wa mkoa wa Kagera tunategemea sana kahawa, na hawa wakulima wamesahaulika kwa muda mrefu. Kwa hiyo mimi nipongeze Serikali kwa hatua ambayo umechukua na kuruhusu kahawa kuuzwa kwenye AMCOS.

Mheshimiwa Spika, kahawa ilikuwa inauzwa kwenye Vyama Vikuu, wanakusanya na ndio wanauza, lakini Vyama Vikuu kimekuwa ni kichaka cha kuwanyonya wakulima na kuwaibia. Sasa niombe sana Waheshimiwa Wabunge wale ambao wanatoka kwenye mikoa inayolima kahawa tuunge mkono utaratibu huu. Mimi mwaka jana niliiomba Serikali, nikaomba huu utaratibu utumike angalau waangalie unaendaje. Mwaka jana tumeujaribu, utaratibu huu ni mzuri wa kuuza kahawa kwenye vyama vya msingi; kwa hiyo ninapongeza sana Serikali kwa hatua hii ambayo imefikia.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine, ili nchi hii iweze kuwa, pamoja na vipaumbele vingine, tunaona Serikali imeanza kuwekeza kwenye kilimo ambacho kimesahaulika kwa muda mrefu. Niiombe sana Serikali wampe nguvu Mheshimiwa Bashe, kazi anayoifanya ni nzuri. Serikali iongeze pesa tuingie kwenye kilimo ambacho kina tija kilimo ambacho kitakuwa na faida kwa nchi lakini pia kwa mkulima. Leo hii ukienda kwenye viwanda vyetu tunaagiza bidhaa na malighafi nje kwaajili ya kuleta kwenye viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, fedha za kigeni zinaenda nje, kitu ambacho hakijakaa sawa. Hii nchi Mungu ameijalia, tuna vipindi virefu vya mvua, tuna udongo mzuri, ukiingia kule kwetu Kyerwa ni raha tupu. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, tuwekeze kwenye Kilimo ambacho mkulima akihitaji mbolea anaipata kwa wakati, mkulima akihitaji mbegu bora, azipate kwa wakati. Ninaamini nchi hii tunaweza tukatumia kilimo na kikaongeza fedha nyingi kwenye uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la kusemea ni hawa watumishi wanaojitolea. Juzi Serikali imetangaza kuajiri. Kuna watumishi wamekuwa wakijitolea muda mrefu. Hawa watumishi inapofika wakati Serikali inapotaka kuajiri, hao wanaojitolea huwa wanaachwa. Sasa naiomba sana Serikali, hao watumishi ambao wamejitolea muda mrefu, Serikali iwape kipaumbele ndio waanze kupewa nafasi. Kwa hiyo, hili naomba Serikali iliangalie, kwa sababu hili jambo ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine, MSD wameshindwa, lazima tueleze ukweli. Sijui pale kuna mdudu gani? Kipindi cha nyuma alikuwepo yule kijana anaitwa Laurian, alikuwa anafanya vizuri, tunapata dawa kwa wakati. Wakaingiza fitina, sijui nini na nini, hata kesi yenyewe aliyofunguliwa hatuioni, lakini madudu tunayoyaona ndiyo haya. Hakuna dawa, hali ni mbaya huko vijijini. Kwa hiyo, naomba sana Waziri anayehusika, huyu bwana waliyemweka pale, kama ameshindwa, wamweke pembeni watafute mtu ambaye anaweza akawapatia wananchi dawa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya mambo ya kulea watu, huko vijijini hali ni mbaya. Hili haliwezekani, ni lazima tuelezane ukweli. Mtu kama ameshindwa kazi, akae pembeni, wanaoweza kazi waendelee.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru, ahsanteni sana. (Makofi)