Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kwa kunipa nafasi, ninakupongeza kwa namna ambavyo umeendesha mjadala huu, pia ninakupongeza kwa kazi nzuri ambayo unaifanya.

Mheshimiwa Spika, kipekee pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anaendelea kuliongoza Taifa letu, vilevile Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na viongozi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda pia kuwashukuru Kamati, hususan ya LAAC pamoja na PAC kwa taarifa zao, zaidi kwa michango, maelekezo na ushauri mbalimbali ambao pia wameweza kuutoa, bila kuwasahau Waheshimiwa Wabunge wote walioweza kuchangia hoja hizi. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba, kunakuwa na thamani halisi ya matumizi ya fedha kwa hiyo, kipekee tunawashukuru sana kwa ushauri mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze katika kuchangia hoja hizi, ninaomba niweze kuanza na hoja ya kwanza kwa upande wa LAAC na baadae muda ukiruhusu nitaenda hoja za PAC. Kwa upande wa LAAC kulikuwa kuna hoja za aina mbalimbali za hati za ukaguzi ambazo zimekuwa zikitolewa, ninapenda tu kushukuru kwa namna ambavyo wameeleza mitiririko mbalimbali, lakini na mimi nipende kusema kwamba, ukiangalia mwenendo mzima wa ukaguzi na hati mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa za ukaguzi utaona namna ambavyo kumekuwa na kuimarika katika nidhamu, hususan nidhamu ya mapato, matumizi, pia namna ambavyo uandaaji sasa wa taarifa zetu mbalimbali za hesabu za mwaka ambavyo zimekuwa zikiendelea kuboreshwa.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia nikiainisha miaka miwili ya fedha iliyopita, huko nyuma ukienda na mwaka 2021 katika hati ambazo zilikuwa zinaridhisha, ukiangalia katika mwaka 2019/2020 tulikuwa tuna hati 124 ambazo zilikuwa sawa na asilimia 67. Halmashauri 124 ndiyo zilipata hati safi, lakini ukiangalia kwa mwaka 2020/21 takribani Halmashauri 178 ambayo ni sawa na asilimia 96, unaona namba inazidi kuongezeka, ni kweli bado zipo Halmashauri ambazo zina hati zisizoridhisha, lakini walao unaona namna ambavyo Serikali inachukua hatua katika kuimarisha nidhamu ya mapato. Tunaendelea kuahidi Bunge lako Tukufu tutaendelea kusimamia kwa umakini kuhakikisha kwamba, kunakuwa na matumizi sahihi, kuhakikisha kwamba taarifa zetu zinazingatia vigezo vinavyohitajika na kwamba, tunakuwa na hati zinazoridhisha.

Mheshimiwa Spika, vilevile ukiangalia kwa mwaka 2019/2020 kwa hati zenye mashaka. 2029/2020 tulikuwa na Hati zenye Mashaka 53 ambayo ilikuwa ni sawa na asilimia 29, kwa mwaka 2020/2021 utaona zimepungua hadi kufikia hati Sita ambayo ni sawa na asilimia Tatu. Kwa hiyo, utaona kutoka Halmashauri 53 kwenda kwenye Halmashauri Sita, hata hizo Sita hatutaki ziwepo, lakini walau utaona kuna maboresho ambayo Serikali imeendelea kuyafanya na hatua zimechukuliwa.

Mheshimiwa Spika, vilevile Halmashauri zenye Hati Mbaya. Ukiangalia katika mwaka 2019/2020 ilikuwa ni takribani Halmashauri Nane zilikuwa na Hati Mbaya, lakini kwa mwaka 2021 ni Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ambayo Mheshimiwa Getere ameisemea kwa umakini na ninaamini huko mbele ataendelea kusimamia kwa umakini na yeye kwa kuwa anaingia katika Kamati ya Fedha ili kuhakikisha kwamba, tunapokuja katika miaka mingine tumetoka Nane, tuko Moja na ikiwezekana miaka ijayo basi iwe ni Halmashauri 0 kabisa na ninaamini hili linawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapenda kusema kwamba kwa kweli mengi ya haya yametokana na kazi nzuri mnayoifanya LAAC pamoja na Kamati zingine. Tunaendelea kuwashukuru kwa mara nyingine tena, tunaahidi kuendelea kusimamia maelekezo yenu, pia ushauri mbalimbali na maelekezo ya CAG kama ambavyo yanabainishwa katika hoja mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ningependa pia kujielekeza katika hoja ya matumizi yasiyofaa, hususan katika Akaunti ya Amana ambayo imesemwa sana hapa. Kimsingi ninapenda kusema kwamba, akaunti hii ya amana katika Halmashauri mara nyingi inawekwa kwa ajili ya fedha maalum. Unakuta zinawekwa fedha nyingine kwa ajili ya kulipia labda Wakandarasi au kunakuwa kuna shughuli maalum hela zimehifadhiwa hapo. Upo mwongozo tayari umeshatolewa na Serikali kupitia Wizara ya Fedha kuhusiana na matumizi na usimamizi wa akaunti hii. Kipekee tutaendelea kuchukua hatua stahiki kuhakikisha kwamba, watu wote wanaosimamia akaunti hii wanasimamia ipasavyo na watakapokuwa wametumia fedha katika akaunti hii ya amana kinyume na utaratibu na miongozo basi hatua stahiki zitaweza kuchukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili suluhu ya yote tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona ni kwa namna gani sasa fedha zote zilizoko humu ndani zinakuwa ring fenced na zisiweze kutolewa bila utaratibu ili kuhakikisha kwamba kweli zinatolewa kwa madhumuni yale tu yaliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya Tatu kuhusiana na ruzuku ya miradi ya maendeleo kutolewa tofauti na bajeti iliyoidhinishwa na Bunge. Katika hili tutaendelea kukaa na Wizara ya Fedha kuona ni namna gani bora ya kuweza kutekeleza ushauri ambao Kamati yetu ya LAAC imeweza kuutoa.

Mheshimiwa Spika, hoja ya Nne ya udhauifu katika usimamizi wa manunuzi, hasa pamoja na mikataba. Tunapenda kusema kwamba, tumeshachukua hatua mbalimbali. Ukiangalia mpaka ilipofikia Agosti mwaka huu, tuliweza kuchukua hatua kwa watumishi 116 kama awamu ya kwanza na tumezielekeza ofisi zetu za Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Wakuu wa Mikoa kuhakikisha kwamba, inapofika tarehe 15 Novemba, wanaleta hatua ya pili ya utekelezaji wa ni namna gani wameweza kuchukua hatua kwa wote ambao wameonesha udhaifu katika usimamizi wa mikataba, vilevile katika usimamizi wa manunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda kutoa mchanganuo, ukiangalia tayari tunao watumishi zaidi ya 22 wameshafikishwa Mahakamani, tunao watumishi zaidi ya 23 wameshafikishwa Polisi na TAKUKURU. Tunao watumishi Watatu wamefukuzwa kazi, watumishi 20 tayari vilevile wamesimamishwa kazi, tunao watumishi takribani 47 ambao kwa mujibu wa taratibu za kiutumishi wamepewa barua ya onyo, vilevile tunae mtumishi Mmoja ambaye ameshushwa cheo.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka kutoa taarifa kwa mchangiaji kwamba, huko tunakoelekea sasa kwa maeneo anayozungumzia kumekuwa na tabia ya Watumishi wa Serikali kutoka TAMISEMI wanapokuwa wamekwapua maeneo mbalimbali, dakika mbili amepata barua ya kuhamishwa, ikiwepo Bunda sasa hivi wameagiza magari ya sensa, sensa imeisha magari hayajaja, tayari aliyekuwa anashughulika na sensa ana barua anapishana na Madiwani.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, huo ulikuwa tu ni mfano wa hizo changamoto, lakini unaweza kuwa huna taarifa nayo hapo. Kwa hiyo, endelea na mchango wako.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, labda nikijielekeza hapohapo tayari ukiangalia katika Manispaa ya Ubungo, Rorya, Mwanza, wako watumishi ambao walihamishiwa Makao Makuu ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na tumewarudisha katika Halmashauri hizo kuweza kujibu hoja zao. Tukifuatilia pia kwa Halmashauri ya Bunda kama na yenyewe ikithibitika hatutasita pia kuwarudisha katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda kuweza kujibu hoja zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumevua vyeo zaidi ya watumishi 57. Wako Waweka Hazina zaidi ya 15 vilevile tumeweza kuwavua vyeo, Wakuu wa Idara ya Utawala na Utumishi zaidi ya 14, Maafisa Mipango Watatu, Wakuu wa Vitengo vya Ukaguzi Watatu. Vilevile kwa watumishi takribani 384 ambao wamekaa kwa muda mrefu hasa Wakuu wa Idara wa DHRO, DPMUs, watu wa Internal Auditor na wengine na wenyewe pia tumewahamisha katika maeneo mbalimbali. Sasa hivi tunaandaa fedha kuhakikisha kwamba, watumishi waliokaa kwenye kituo kimoja zaidi ya miaka Saba wanahamishwa ili kuhakikisha tunaweza kuchukua hatua stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya Tano kuhusiana na udhaifu katika uwekezaji wa mitaji ya umma na katika miradi ya Halmashauri. Kwenye eneo hili kulikuwa kuna malalamiko kwamba, kumekuwa na uwekezaji ambao mwingine ulikuwa ukifanyika bila kuwa na upembuzi yakinifu, lakini bila kuwa na maandiko ya miradi. Ni kweli baadhi ya Halmashauri umekuta wengine pia wakiiga aina ya miradi hasa ya stendi na masoko, vilevile wengine wamekuwa wakipeleka hela katika uwekezaji katika benki ambazo hazina utendaji unaoridhisha na bila kufanya upembuzi yakinifu.

Mheshimiwa Spika, ninapenda tu kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, kwa sasa tumeshaandaa muongozo wa namna ya uandishi wa miradi mbalimbali ya uwekezaji katika Halmashauri zetu, vilevile tumeshirikiana na Wizara ya Fedha pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa la UNCDF, tayari tunayo Kamati ya Kitaifa yenye wajumbe au wataalam takribani 44, wameshapatiwa mafunzo wa kutoka TAMISEMI, Wizara ya Fedha pamoja na mamlaka zingine mbalimbali kuhakikisha kwamba, tunakuwa na mwongozo sahihi na tunaendelea kuwafundisha wataalam wa Halmashauri ili wanapoandaa miradi ya uwekezaji na mingi ni katika miundombinu, kuhakikisha kwamba wanakuwa na ubobezi na wametimiza vigezo vinavyohitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuanzia Julai 2022 tunashukuru Mheshimiwa Rais aliweza kuidhinisha muundo wa kiutumishi wa Halmashauri zetu au Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na muundo huu umeshaanza kutumika na kwa sasa tunayo Idara na Section mpya ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Lengo kubwa la kuanzisha Idara hii ni kuhakikisha kwamba, kabla Halmashauri hazijaja au hazijaanza kutekeleza miradi ya uwekezaji katika Halmashauri zao basi mapendekezo hayo au maandiko yanapitishwa katika Idara hiyo ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kuweza kupitiwa, wanapojiridhisha pia hawatamaliza wenyewe kule, wataleta TAMISEMI nasi pia kwa wataalam wabobezi waliopo, watapitia na kujiridhisha endapo kweli miradi hiyo inayopendekezwa ya uwekezaji inakidhi vigezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye eneo hilo pia, eneo la tatu…

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, kuna taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nasi tungekuwa tunawasimamisha hivyo kila dakika nadhani tusingefika hapa.

MBUNGE FULANI: Aah!

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Ni haki yake ya msingi Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Charles Kajege, taarifa. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka nimpe taarifa msemaji, anaonesha kutaka ku-deal na tatizo kwa kumfukuza nani huyu… kuwafukuza watumishi na kuhamisha watumishi wa ngazi ndogondogo badala ya ku-deal na tatizo kubwa ambalo tunaliona kwamba, liko Makao Makuu, Mheshimiwa Waziri atuambie kuhusu hapo?

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, sipokei taarifa hiyo. Naomba tupeane nafasi kidogo ili tuweze kumaliza hoja hizi.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunakamilisha mwongozo wa kusimamia miradi baada ya kukamilika hasa katika kuanzisha special purpose vehicle katika miradi yote ya uwekezaji. Kama ambavyo imebainishwa katika changamoto mbalimbali na Kamati, tunapenda tu kusema kwamba, tutaendelea kuhakikisha kwamba, tunazifanyia kazi kwa ukamilifu na tunaamini maboresho mbalimbali tuliyoyaeleza hapa kupitia masuala ya SPV, kupitia uanzishwaji wa Kitengo cha Biashara, Viwanda na Uwekezaji pamoja na mambo mengine basi tunaamini hili litaweza kutekelezwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya usimamizi na utoaji wa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Yapo mapendekezo mbalimbali ambayo tunayapokea, kulikuwa na mapendekezo ya kuanzisha akaunti maalum kwa ajili ya fedha zitakazotolewa na kurejeshwa ziwekwe katika kumbukumbu za vikundi vinavyokopa.

Mheshimiwa Spika, ninapenda tu kuliarifu Bunge lako Tukufu, tayari hili limeshatekelezwa. Kuanzia mwaka 2021/2022 Julai, tayari kuna akaunti mbili za Halmashauri katika masuala ya mikopo. Akaunti ya kwanza iko Benki Kuu na akaunti hii inatumiwa na Halmashauri kuweza kuchangia asilimia 10 ya mapato ya ndani, vilevile ni akaunti ambayo inatumika kwa ajili ya utoaji wa mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili au akaunti ya pili ni akaunti ambayo tumeifungua katika akaunti za kibiashara katika Benki ya NMB pamoja na CRDB ambayo ndiyo tunaitumia kwa ajili ya kupokea marejesho ya mikopo ya vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, la pili, marekebisho mengine ambayo tumeyafanya, kwa sasa tunao Mfumo wa Kielektroniki wa Ten Percent Loan Management Information System. Na kupitia mfumo huu ambao tumeshaanza kuutumia tangu Mei, 2022, tumeshaanza kuona mabadiliko katika suala zima la hali ya utoaji wa mikopo pamoja na urejeshaji wa mikopo.

Mheshimiwa Spika, kuna mikopo ya nyuma (mikopo chechefu), tumeshakaa na halmashauri zetu pamoja na maafisa ustawi wa jamii kuweza kupata tathmini tangu mpango huu ulipoanzishwa mpaka sasa ni kiasi gani cha fedha zimetolewa, kiasi gani kimerejeshwa na kiasi gani bado hakijarejeshwa mpaka sasa. Tumewaomba taarifa za mpaka Juni, 2022 na tumewapa muda mpaka tarehe 30, Novemba, 2022 waweze kuwa wamewasilisha taarifa hizo za backlog ya mikopo.

Mheshimiwa Spika, tunaamini baada ya kupata taarifa hizo na baada ya kusafisha data (kufanya data cleaning), basi tutaweza kuchukua hatua stahiki na kuhakikisha kwamba mikopo yote iliyotolewa inaweza kurejeshwa.

Mheshimiwa Spika, pia tumefanya marekebisho katika Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu za Mwaka 2019. Marekebisho haya yalifanyika mwaka 2021 ambapo kwa sasa halmashauri zimeruhusiwa kuweza kutenga fedha kati ya shilingi milioni sita hadi 60 kwa mwaka ili kuzitumia fedha hizo kutoa mafunzo ya kiungozi, kiutawala, usimamizi wa fedha, uendeshaji wa miradi na utoaji wa taarifa kwa vikundi vyetu.

Mheshimiwa Spika, fedha hizo pia – kati ya milioni sita mpaka 60 kwa halmashauri – zitaweza pia kutumika kufanya ufuatiliaji wa mikopo na tathmini ya namna ambavyo vikundi vinavyopata mikopo hiyo vinaendelea.

Mheshimiwa Spika, tunaona mabadiliko, tumeona hoja kwamba fedha nyingi zinatoka, na hata ukiangalia mwaka huu zaidi ya bilioni 75, na kwa kweli ni lazima fedha zote zilizotolewa ziweze kurejeshwa. Tupende tu kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba ukiangalia kuanzia mwaka 2019/2020 na 2020/2021 utaona namna kiwango cha mikopo kinachotolewa. Huko nyuma ilikuwa inaanza kutoka kwa asilimia 65, lakini kwa sasa, mwaka 2021/2022, takribani asilimia 90 ya mikopo imeweza kutolewa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa marejesho, mwaka 2019/2020 marejesho yalikuwa kwa asilimia 72 na mwaka 2021/2022 marejesho sasa yamefikia asilimia 84 na tunaendelea kuimarisha suala hili. Tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge wameliongea kwa hisia kali. Kwa kweli hizi fedha si msaada, zinatakiwa kweli kuwa ni mikopo na ni mikopo ambayo imetolewa kwa masharti nafuu. Kwa hiyo na sisi tunapokea hoja hiyo na tutaendelea kuimarisha mifumo kuhakikisha kwamba tunakwenda kwenye utoaji wa asilimia mia na hatimaye pia urejeshaji uwe kwa kiwango kikubwa kinachoridhisha.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya baadhi ya stahiki za watumishi kutolipwa ipasavyo, wengine michango yao ya hifadhi ya jamii imekuwa haipelekwi kwa wakati, hali ambayo imewaathiri wakati wanapostaafu, posho za likizo, gharama za uhamisho, gharama za masomo pamoja na posho nyingine nazo pia zimekuwa hazitolewi.

Mheshimiwa Spika, nikienda katika hoja ile ya watumishi waliostaafu katika halmashauri. Unakuta wengine wamestaafu lakini wameshindwa kulipwa mafao yao kutokana na baadhi ya halmashauri kutopeleka na nyingine ni shilingi laki mbili au tatu tu.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Watu Wenye Ulemavu tarehe 01, Novemba ilituita na tuliweza kufanya kikao pamoja na makatibu tawala wa mikoa na tumeshakubaliana kuweza kuhakikisha kwamba tunahakiki madai yote na kuhakikisha kwamba wanakuja na mpango kazi wa namna watakavyolipa madai yao hayo kwa ajili ya watumishi wetu hawa wa halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikubwa ambacho tumekubaliana na mifuko yetu ya hifadhi ya jamii, kwa kiasi kikubwa kwa madai ambayo yamesababishwa na halmashauri mbalimbali kutopeleka michango, basi waweze kulipwa fedha hizo bila ya kuleta usumbufu kwa mtumishi aliyestaafu.

Mheshimiwa Spika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia mchango wako.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, naomba nije kwenye hoja ile ya uthamini wa DART. Nipende tu kusema kwamba kwa wale wananchi wa eneo la Gerezani kulikuwa na maombi hapa au maelekezo ya Kamati kuhakikisha kwamba taarifa ya tathmini inaangaliwa upya na kwamba walioshiriki basi wanachukuliwa hatua.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwamba PAC ilielekeza nyaraka mbalimbali ziwasilishwe kwa CAG na sisi tutafanya hivyo na kuhakikisha kwamba CAG anapata nyaraka hizo ili apitie kwenye valuation report kuona kama kweli kilicholipwa kupitia yale malipo ya usumbufu na malipo ya uthamini ndicho ambacho kilistahili kulipwa au kuna malipo ya ziada au kama kuna mapungufu basi taarifa hiyo ndiyo itakayoelekeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye hoja ya kuungua kwa Majengo ya Shirika la Masoko Kariakoo, na kwamba alipokwenda CAG kuna hati mbalimbali za takribani shilingi bilioni 3.5 hazikuweza kupatikana, na kwamba hii ilitokea baada ya CAG kubaini tu baadaye soko likaungua.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwanza, mwezi Aprili, 2021, tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliunda timu; kabla hata haya hayajajitokeza, kwa ajili ya kuangalia ubadhirifu mbalimbali; na tayari kuna hatua nyingine zinaendelea kuchukuliwa. Lakini kwenye hili la kufanya forensic audit tunakubaliana na Kamati na tutafanya mawasiliano na mamlaka zenye dhamana ya kufanya forensic audit ili iweze kufanyika. Na endapo kuna jinai yoyote basi iweze kuthibitika.