Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nami napenda kuchukua fursa hii, kama walivyoanza wenzangu, kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia kukutana hapa leo tukiwa na afya njema. Kipekee kabisa napenda nikushukuru wewe mwenyewe kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia hoja za kamati tatu zilizoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, ninaomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati pamoja na Wenyeviti wa Kamati zote tatu na Waheshimiwa Wabunge wote waliopata fursa ya kuchangia kwenye hoja hizi. Naomba niwahakikishie Wajumbe wa Kamati kwamba michango yao ni mizuri na tunaendelea kuithamini.

Mheshimiwa Spika, kwa muda wa siku tatu kulikuwa na mchango uliendelea kwa muda mrefu kuhusu KADCO. Ninaomba nami nianze kuzungumzia KADCO.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1998 Serikali iliagiza ukodishaji na uendelezaji wa Kiwanja cha Ndege cha KIA (Kilimanjaro International Airport) utekelezwe na kampuni ya binafsi. Hii ilikuwa ni moja kati ya uendelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma yaliyofanywa kwa kipindi hicho.

Mheshimiwa Spika, baada ya mchakato wa ubinafsishaji kukamilika, Kiwanja cha Ndege cha KIA ilianzishwa kampuni binafsi ambayo ni KADCO tarehe 11, Machi 1998 chini ya Sheria ya Makampuni sura 212, wakati huo kampuni hiyo ikiwa na wanahisa wawili. Mwanahisa wa kwanza alikuwa ni Motor Mc Donald International ya Uingereza na mwanahisa alikuwa ni Inter- consult Tanzania limited. Baadaye waliongezwa wanahisa wawili ambapo mwanahisa mwingine alikuwa ni Serikali na mwanahisa mwingine wa nne alikuwa ni South African Infrastructure Fund.

Mheshimiwa Spika, wanahisa hao walikuwa na mgawanyo wa hisa kama ifuatavyo: -

(a) Motor Mc Donald International ya Uingereza ilikuwa na hisa 41.40%,

(b) South African Infrastructure Fund ilikuwa na hisa 30%,

(c) Inter Consult Tanzania Limited ya Tanzania ilikuwa na hisa 4.6%, na

(d) Serikali ilikuwa na hisa 24%.

Mheshimiwa Spika, katika ubinafsishaji huu kulikuwa na changamoto kubwa zilizojitokeza. Changamoto ya kwanza iliyojitokeza ni kuwa wanahisa walishindwa kuwekeza kwenye Kiwanja cha Ndege cha KIA, changamoto ya pili ilyojitokeza ni Serikali kutonufaika na mkataba wa uendeshaji wa Kiwanja cha Ndege cha KIA, na Changamoto ya tatu iliyojitokeza ni kukosa kipengele cha kuitaka KADCO kulipa ada ya uendeshaji (concession fee), na changamoto ya nne iliyojitokeza, kulikuwa na exclusive right ya kuzuia uwekezaji au ujenzi wa kiwanja cha ndege ndani ya usawa wa mzunguko (radius) ya kilomita 240. Yaani ndani ya radius ya kilomita 240 hakukutakiwa mwekezaji yeyote awezekujenga kiwanja cha kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hizi Serikali iliona mkataba huo unamaslahi machache. Kwa hivyo Serikali ikaamua kwamba sasa iko haja ya kuvunja mkataba huo. hata hivyo kabla ya hapo kulikuwa na mikataba mitatu ambayo ilisainiwa. Mkataba wa kwanza ilikuwa ni sharehold agreement, mkataba wa pili ulikuwa ni uendeshaji (concession fee) na mkataba wa tatu ni wa ukodishaji (lease agreement) ambao uliwekwa kati ya Serikali na KADCO.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto zilizojitokeza Serikali ilifanya maamuzi ya kuamua kuwanunua wanahisa. Ambapo Kampuni ya Motor Mc Donald International ya Uingereza ililipwa dola za Marekani 2,752,540.6, hizi ni Dola za Kimarekani, South African Infrastructure Fund ililipwa dola za Marekani 1,994,593.52 na Inter Consult Tanzania Limited ya Tanzania ililipwa dola za Marekani 339,373.01.

Mheshimiwa Spika, baada ya kulipwa fedha hizo na Serikali, Kampuni ya KADCO ikawa asilimia 100 ni Kampuni ya Serikali na share zake zote zipo chini ya Msajili wa Hazina kama ilivyo kampuni nyingine za Serikali. Haya yote yanathibitishwa kupitia hati ya usajili namba 33,616 ya BRELA kuhusu usajili wa KADCO.

Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kununua share hizo, shareholding agreement automatically ilikufa yenyewe kwa sababu wana-share hawapo. Mikataba miwili iliyobaki, concession agreement pamoja na lease agreement zilikuwepo lakini hazikufanyiwa mabadiliko yoyote. Tulitegemea pengine zingefanyiwa mabadiliko na kukawa na agreement back kati ya TAA na KADCO lakini haikufanywa hivyo. Nitaeleza huko mbele hatua ambazo Serikali itazichukua kwa ajili ya kufanya mabadiliko hayo.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie kidogo kuhusu wafanyakazi wa KADCO. Kama nilivyosema, KADCO ni kampuni ya Serikali kwa asilimia 100 na bodi ya KADCO pamoja na wanabodi wa KADCO na Mwenyekiti wa bodi wanachaguliwa na Serikali na hivi ninavyosema kwamba bodi hii iko na inaenda vizuri.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuna taarifa kuktoka kwa Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa Waziri, alikuwa ametupeleka vizuri, ametuonesha njia na dola zilivyolipwa na mikataba ile mitatu, sasa angetumaliza kwenye hiyo hoja halafu akaenda ya wafanyakazi ili tukawa na mtiririko mzuri wa mambo hayo. Kwa sababu akiturudisha huku tena tutakuwa tumesahau, atupeleke huko huko alikokuwa anatupeleka tumalizie. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Getere yeye ndiyo alilvyopanga mtiririko wa mchango wake sasa tusimchanganye ila tusikilize kama unalo kwenye hili analosema unaruhusiwa kutoa taarifa, lakini yeye amepanga mtiririko ambao yeye anauelewa maana yeye ndiyo anatoa maelezo. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nitakwenda hivyo anavyotaka kwa sababu kila kitu kiko hapa, hakuna tofauti yoyote. Kama nilivyosema KADCO ilianzishwa kama kampuni kwa sura ya 212. Lakini TAA (Tanzania Airport Authority) ilianzishwa kupitia tangazo la Serikali Namba 404 la mwaka 1999 chini ya kifungu namba tatu cha Sheria ya Uwakala wa Serikali. Kwa vile Tanzania Airport Authority si mamlaka, inaitwa tu jina hilo kwa sababu sheria iliyoanzisha ilikuwa ni Sheria ya Uwakala wa Serikali Sura Namba 244 ya mwaka 1997.

Mheshimiwa Spika, katika kutatua tatizo la KADCO na kuweka utaratibu mzuri wa kuendesha viwanja vya ndege, Serikali tumeanza mchakato wa kutengeneza Sheria ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kama mamlaka, na kwenye sheria hiyo tutahakikisha kwamba KADCO inaelekezwa vizuri. Kwenye sheria hiyo, tutahakikisha kwamba KADCO inaelekezwa vizuri, aidha imilikiwe moja kwa moja; sasa hivi inamilikiwa na TAA, lakini imilikiwe ndani ya sheria au alternative ifanyike kwamba, ianzishwe kampuni tanzu ambayo yenyewe ndiyo itaendesha Kiwanja cha Ndege cha KIA. Suala la KADCO linaweza kuwepo ama linaweza kufa moja kwa moja, itategemea sheria itakavyoelekeza. Hayo tutayafanya sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu, kwenye sheria hiyo tunaangalia utaratibu ambao utavifanya viwanja vyetu vya ndege viwe salama na ulinzi ukamilike kwa sababu kuna changamoto kubwa sana kwenye viwanja vya ndege. Sheria iliyopo sasa hivi haikidhi uendeshaji wa viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Spika, ninaamini kwamba sheria hii itakapokuja kupitishwa hapa Bungeni tatizo la KADCO litamalizwa maisha, litakuwa limeisha. Inaweza kuendeshwa moja kwa moja kupitia TAA yenyewe au inaweza kuanzishwa kampuni nyingine ambayo itasimamia Kiwanja cha Ndege cha KIA.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Saashisha Mafuwe.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa kwamba wananchi wa Hai sasa hivi wako kwenye TV wanasubiri maagizo ya Serikali kwenye jambo hili. Ameeleza historia vizuri, akaja akatuambia KADCO ni ya Serikali, katikati hapa anasema inaweza ikawepo au isiwepo. Kwa hiyo, nataka tu kumwambia, leo tunategemea kupata majibu ya Serikali thabiti kwamba KADCO ni ya Serikali au siyo ya Serikali; na hatma yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa taarifa yangu kwa sababu kule kuna jambo linaendelea na hizi taarifa kule zinachanganya wananchi. Sasa hapa tunaambiwa ni ya Serikali asilimia 100, lakini inaweza ikaondolewa au isiondolewe. Serikali inasemaje kuhusu jambo hili ili sisi wananchi wa Hai tunaosikiliza Serikali hapa tujue hatma ya jambo hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, kikanuni unapotoa taarifa ni kwamba unamwongezea yule mchangiaji jambo fulani, siyo unamwuliza maswali. Sijui tunaelewana! Eeh, yaani siyo umwulize maswali, sasa inakuwa kimegeuka kuwa kipindi cha maswali na majibu. Hapa anayeruhusiwa kuuliza maswali ni mimi hapa. Mimi ndio naruhusiwa kuuliza maswali, lakini ninyi toeni tu taarifa kwa mujibu wa kanuni zetu.

Mheshimiwa Waziri, malizia mchango wako.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, tutaleta sheria hapa kama nilivyosema ambayo itaeleza mfumo mzima wa uendeshaji wa viwanja vya ndege, ikiwemo Kiwanja cha Ndege cha KIA. Wakati utafika Waheshimiwa Wabunge nyote mtapata hiyo fursa, mtalichambua jambo hili kwa kina na ushauri wenu sisi tutaupokea.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kwamba Serikali kupitia Kikao cha Baraza la Mawaziri namba 15 cha mwaka 2009 kilichofanyika Mei 14 mwaka huo, kilielekeza kwamba Wizara ya Uchukuzi iache majadiliano na Kampuni ya Omniport ambayo ilikuwa inataka ikabidhiwe Uwanja wa Ndege wa KIA badala ya KADCO kwa kuwa KADCO alishindwa kuwekeza. Taarifa zilizoletwa zilionesha kwamba hata huyo Omniport ambaye alikuwa apewe huo uwanja, naye hakuwa na uwezo wa kuwekeza, ilikuwa ni usanii. Hatua ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili, Serikali…

SPIKA: Mheshimiwa taarifa ni moja.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, inaendana na hiyo tu. Ni kwamba katika maamuzi hayo ya Serikali, ikaelekezwa kwamba KADCO, huyo Omniport wote watolewe, Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro urudishwe chini ya mikono ya TAA. Sasa ni kwa nini haukurudishwa na mpaka leo hii tunajadili KADCO wakati maelekezo ya Serikali yalikuwa upelekwe chini ya mikono ya TAA? (Makofi)

SPIKA: Sawa ahsante. Mheshimiwa Waziri unaipokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, inanipa taabu kwa sababu kujibu kwa nini haikurejeshwa, hilo swali siwezi kulitolea ufafanuzi hapa.

SPIKA: Nami nimekusaidia. Yaani mtu akitoa taarifa, ni ile taarifa ambayo haina swali, kwa sababu wewe siyo kazi yako kujibizana na Mbunge. Au umeshamaliza mchango wako? Wewe malizia mchango wako, kama taarifa yake unaona imeuliza swali, wewe endelea na mchango. Maswali ni mimi hapa ndio naruhusiwa kuuliza.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kuhusu wafanyakazi wa KADCO, kama nilivyosema, KADCO ni kampuni ya Serikali na Bodi ya Wakurugenzi pamoja na Mwenyekiti wanachaguliwa na Serikali. Hivi ninavyozungumza, tuna bodi pamoja na wajumbe wote na wanafanya kazi. Wafanyakazi wote wa KADCO ni Watanzania. Pia KADCO inayo mwanasheria ambaye anaitwa Winfrey Komba ambaye yeye alihamishwa KADCO mwezi Januari, 2021.

Mheshimiwa Spika, pia KADCO inaendelea kulipa kodi mbalimbali, kwa mfano tu imelipa gawio mwaka 2016/2017 Shilingi milioni 555; mwaka 2017/2018 ililipa Shilingi milioni 583; mwaka 2018/2019 ililipa Shilingi bilioni moja; miaka miwili iliyofuatia 2019/2020 na 2021 haikulipa kutokana na ugonjwa wa Covid na sekta ya anga iliathiriwa kwa asilimia kubwa. Pia KADCO inayo akaunti Benki Kuu ya Tanzania na malipo yote yanayofanywa na makampuni ya ndege yanawasilishwa kule. Hiyo ni hoja kuhusu KADCO.

Mheshimiwa Spika, pia naomba niongelee hoja kuhusu maingiliano kati ya TANROADS na TAA kuhusu ujenzi wa viwanja vya ndege. Ni kweli yalifanyika maamuzi mwaka 2018 kuhamisha ujenzi wa viwanja vya ndege kwenda TANROADS. Kulikuwa na changamoto ambazo zilisababisha kufanya hivyo na ilifanya hivyo kupitia GN namba 293 ya mwaka 2000 ya TANROADS ambayo ilifanyiwa mabadiliko ili kazi hiyo iweze kufanyika ndani ya TANROADS.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia mchango wako.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea, sasa hivi tumeshafanya mchakato na ujenzi wa viwanja vya ndege sasa vitaanza kurejeshwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA). Ila kwa ile miradi ambayo inaendelea, kwa mfano Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Sumbawanga, Kigoma na Tabora, mchakato utaendelea chini ya TANROADS kwa sababu tukiurejesha tena utachukua muda mrefu na viwanja vya ndege hivyo havitajengwa.

Mheshimiwa Spika, pia kuhusu Kiwanja cha Ndege cha Msalato ambacho kinajengwa chini ya ufadhili wa ADB nacho kitaendelea kutekelezwa na TANROADS kwa sababu mchakato wenyewe kuurejesha tena utatuchukua muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ambalo nilitaka kuligusia ni kuhusu suala la Bandari ya Tanga. Mheshimiwa Kapinga alilizungumza kwa hisia kali suala hili, lakini naomba kumwambia tu na Wabunge wote na Watanzania kwa ujumla kwamba Bandari ya Tanga ni muhimu sana kwetu sisi na tunaendelea na ujenzi na mkandarasi yuko site. Kuhusu kwamba kuna Mkandarasi alipewa subcontract kwa bei ndogo, hili linafanyiwa kazi na CAG na naliomba Bunge lako Tukufu, utupe muda CAG afanye uchunguzi maalum, halafu tutapata ripoti na tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. (Makofi)

SPIKA: Naamini Mwenyekiti ameshasikia. Sasa katika ufafanuzi wako Mheshimiwa Waziri; kwanza Waheshimiwa Wabunge mtakumbuka ile siku nadhani ni juzi, nilisema ningempa nafasi Mheshimiwa Waziri leo na amepewa. Nilisema katika majibu yake, mojawapo ya mambo anatakiwa atuambie ni akaunti za KADCO ziko wapi? Leo amejibu hapa, nadhani mmemsikia, amesema akaunti za KADCO ziko Benki Kuu. Nimesikia vizuri Mheshimiwa Waziri au sijasikia vizuri?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ndiyo akaunti ya KADCO iko BOT.

SPIKA: Sawa. Sasa Mheshimiwa Waziri ili tuongozane vizuri kwenye haya maazimio ya Kamati na Wenyeviti wanasikiliza hapa kwa sababu kuna maeneo watafanya marekebisho kwa kuwasikiliza na kama watakuwa wameelewa. Wakati hii KADCO ilikuwa ni kampuni binafsi; na natumia neno “ilikuwa kampuni binafsi”, Serikali ikanunua shares zote, ikalipa pesa wale watu binafsi; ikahamia kuwa kwenye umiliki wa Serikali kwa asilimia 100. Mkataba ambao umesema kwamba ulikufa, ni mkataba mmoja tu kati ya mitatu uliyoitaja, kwamba ni ule mkataba wa hisa ndiyo uliokufa. Mkataba wa upangishaji (lease agreement) bado upo, kwa maelezo uliyotoa. Mkataba wa concession ambao ulikuwa unaipa kampuni binafsi mamlaka ya kuendesha pale na kufanya hivi, bado upo. Huu mkataba wa upangaji, nani ni mpangaji sasa na nani mpangishaji? (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema kuna mikataba miwili ambayo ipo concession agreement na lease agreement na mikataba hii ilikuwa kati ya Serikali na KADCO. Kwa hiyo,…

SPIKA: Ilikuwa kati ya Serikali na KADCO wakati KADCO ni binafsi.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ni wakati huo. Wakati huo KADCO ilikuwa ni Kampuni ya binafsi, lakini baadaye KADCO ilibadilika kuwa kampuni ya Serikali kwa asilimia 100.

SPIKA: Hapo tuko wote, pamoja kabisa. Hoja ni kwamba, huu mkataba wa upangishaji, kabla hata sijaenda kwenye concession, mkataba wa upangishaji ni kati ya nani na nani kwa sasa? (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, mikataba hii ilikuwa ifanyiwe mabadiliko, lakini ilivyo sasa hivi…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, siyo hoja yake binafsi ni hoja ya Serikali, wala siyo yeye aliyekuwa ofisini. Kwa hiyo, msiwe mnamtaza kama vile…

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, mkataba ulivyo sasa hivi hata ukichukua mkataba ule unaona ni kati ya KADCO na Serikali…

SPIKA: KADCO binafsi?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, KADCO binafsi, lakini ilibadilika kuwa ya Serikali.

SPIKA: Sawa, ahsante. Ngoja, hapo tumeshaelewa. Mkataba wa upangishaji ni kati ya KADCO binafsi ambaye alishakufa, lakini kwenye mkataba huu anaishi. Sawa. (Makofi)

Halafu concession agreement pia ilikuwa kati ya KADCO binafsi na Serikali. Niko sahihi?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ndiyo, lakini KADCO mpaka sasa hivi ipo, isipokuwa zile shares zilibadilika kutoka watu binafsi kuja kwenye Serikali.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nilitaka kuyaelewa haya ili tunapoelekea kwenye maazimio tujue tunaazimia nini? Maana ni jambo la muda mrefu. Haiwezekani kila siku inazungumziwa KADCO, KADCO, KADCO! Lazima tufike mahali. (Makofi)

Jambo la mwisho Mheshimiwa Waziri, huu mkopo ambao TAA iliagizwa kukopa na Serikali, kwamba kwa kuwa wewe ndio unashughulika na viwanja vya ndege, kopa kalipe. Huu mkopo analipa nani? TAA au KADCO ya Serikali?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema kwamba mkopo huu Serikali iliagiza TAA ikope na imelipa TAA kutoka Benki…

SPIKA: Imelipa TAA na siyo KADCO?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, siyo KADCO.

SPIKA: Haya, ahsante sana. (Makofi)