Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana kwa kupata nafasi niweze kuchangia katika hoja ambazo ziko mbele yetu. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya ambayo sisi Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi kwamba kuna miradi mingi inaendelea katika majimbo yetu pamoja na huduma za jamii. Nikupongeze pia wewe binafsi Mheshimiwa Spika kwa kuongeza Bunge letu vizuri na tunakupongeza kwa umahiri mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nipongeze wenyeviti na makamu wenyeviti na wajumbe wa kamati hizi tatu, kwa maana ya PIC, PAC pamoja na LAAC kwa kuchambua taarifa hizi, ripoti ya CAG pamoja na uwekezaji wa mitaji ya umma katika taasisi ya mashirika mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza kwanza kwenye kamati ya PIC, uwekezaji wa mitaji ya umma. Faida ambayo inatarajiwa kupata na Serikali katika utendaji huu ni gawio, mchango wa asilimia 15, marejesho kutoka TTMS, yaani mtambo unaosimamia masuala nchini riba na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha uliyoishia Juni 30, 2021, kwa upande wa gawio, malengo ambayo TR aliweka kwa kukusanya ilikuwa ni Shilingi bilioni 408.4, lakini makusanyo halisi ni Shilingi bilioni 308 sawa na ufanisi wa asilimia 76.3. Tukienda kwa upande wa michango ya asilimia 15 ya mapato ghafi, Msajili wa Hazina aliweka lengo la kukusanya Shilingi bilioni 395.4, lakini makusanyo halisi ni Shilingi bilioni 202.2, sawa na ufanisi wa asilimia 51 ya lengo. Kwa upande wa marejesho kutoka TTMS, malengo kwa mwaka wa fedha huu uliyoishia Juni 2021 ilikuwa ni Shilingi bilioni 15, lakini makusanyo halisi ni Shilingi bilioni 10.3 sawa na ufanisi wa asilimia 68.3.

Mheshimiwa Spika, picha inayoonekana hapa ni kwamba kwa ujumla mwenendo wa mapato yasiyokuwa ya kodi, yanayotokana na uwekezaji huu uliofanywa na Serikali, yamepungua sana kwa mwaka huu wa fedha uliyoishia Juni 2021. Vilevile tukumbuke kwamba fedha hizi ni sehemu ya bajeti zetu, maana mapato yote haya yanaingia kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali (consolidated fund). Kwa hiyo, tunapokuwa hatufanikishi bajeti zetu ni kwa sababu ya usimamizi usioridhishisha kwa baadhi ya taasisi au mashirika ambako Serikali imewekeza. Matokeo haya yanaonyesha dhahiri kwamba baadhi ya taasisi ambazo Serikali zetu imewekeza kodi za wananchi hayasimamiwi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Taarifa ya Kamati ya PAC kusomwa ukurasa wa 22 inazungumzia taasisi kutokuwa na Bodi za Wakurugenzi. Bodi ya Wakurugenzi ni chombo kikuu cha uamuzi katika taasisi na mashirika ya Umma. Kwa hiyo, unapokosa chombo cha maamuzi pale ambapo Serikali imewekeza, unatarajia nini? Lazima utarajie matokeo haya ambayo hakuna mahusiano yaliyofika hata asilimia 80. Kwa hiyo, kutokufikia malengo haya ni kwa sababu kuna maamuzi ambayo yalitakiwa yafanyike, hayakufanyika. Hata wanaofanya biashara binafsi, kama ndani ya mwaka mzima hakuna kikao kinachokaa kufanya maamuzi, unatarajia nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana, suala la Bodi ni la msingi sana. Lazima kuwe na checks and balance. Kwa hiyo, naomba sana wale wanaohusika na uteuzi wa Bodi, wateuliwe Wajumbe wa Bodi wenye weledi katika taasisi hizi na mashirika ambapo Serikali imewekeza. Taasisi hizi zikifanya vizuri, haitaishia kupata gawio asilimia 15 ya mapato ghafi na marejesho haya, lakini yatapata faida ambayo pia italipa kodi ya mapato. Kwa hiyo, mashirika haya yakiboreshwa katika misingi hii yataongeza Mapato ya Taifa katika Mfuko Mkuu wa Serikali na Bajeti Kuu ya Serikali. Kwa hiyo, naomba sana kwa kweli jambo hili tulichukilie kwa uzito mkubwa sana kwa upande wa Serikali maana ni kwa faida ya Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC). Nampongeza sana Mwenyekiti na timu yake nzima kwa kazi kubwa waliyofanya, wamepitia Taarifa ya CAG, imeonyesha madudu ambayo tumeyaona. Taarifa ya CAG inasema, Serikali imepata hasara ya Shilingi bilioni 68.73 ambayo ilisababishwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) kuchelewa kuwalipa Wandarasi. Taarifa inasema, kusimama kwa ujenzi wa vihenge unaotekelezwa na Wakala wa Taifa wa Hifadhi (NFRA) wakati Mkandarasi ameishalipwa Dola za Marekani 33.4 sawa na karibu Shilingi bilioni 76.8; taarifa inaendelea kusema, malipo ya Dola za Marekani milioni 153.43 yalifanywa na TANESCO kwa SYMBION ambayo takriban ni Shilingi bilioni 350; taarifa hii inasema, fedha hizi ni nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, leo Waheshimiwa Wabunge tunalia hapa miradi ya barabara kwenye majimbo yetu, nishati ya umeme haipo, lakini kuna wenzetu ambao wamepewa dhamana ya kusimamia fedha za Umma, wanazichezea. Naomba sana wenzetu wenye dhamana hizi wawe na uchungu na Watanzania. Wawe wanatembea vijijini kuona hali halisi ya maisha ya Watanzania. Tukumbuke hizi ni kodi za Watanzania. Tunakaa Bunge hapa miezi mitatu tunapanga bajeti, halafu watu wachache wanakaa wanachezea fedha za Umma. Jambo hili linaumiza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna miradi mingi ya kimkakati inataka fedha, tuna upungufu wa kibajeti, tunataka fedha, tuna upungufu wa watumishi wa Afya, Elimu katika maeneo yetu, tunataka fedha; tuna deni la Serikali, tunataka fedha tulipe; Watanzania wana shida ya maji katika maeneo mbalimbali; tuna shida ya nishati ya umeme vijijini, lakini wapo wenzetu wameamua kucheza na fedha za Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umesikia michango ya Waheshimiwa Wabunge toka Bunge hili limeanza, inatia uchungu sana pale ambapo fedha za Umma zinachezewa. Kwa hiyo, naomba Bunge lako Tukufu liazimie kuwachukulia hatua wote waliohusika na ubadhirifu huu wa fedha za Umma. Sisi ni wawakilishi wa wananchi, tunaelewa uhalisia ulioko kwa wananchi kule. Kuna msemo wa Mheshimiwa Waziri wa Maji, kwamba mihemo ya mgonjwa anajua anayelala naye. Sisi ndio tunalala na wananchi wetu. Kwa hiyo, naomba Wenyeviti wa Kamati, pamoja na maazimio ambayo wameweka, basi tuongeze yetu kwamba lazima waliochezea fedha za Umma wachukuliwe hatua za kisheria na kikanuni za kiutumishi ili liwe fundisho kwa wengine kwa miaka mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani kila mwaka katika taarifa za CAG makosa yanajirudia kwa taasisi hizo hizo, na watu wapo tu. Jambo hili halikubaliki, sisi kama Wabunge lazima tusimame na kuwatetea Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya machache, nashukuru kwa kunipa fursa na ninaunga mkono hoja zote tatu.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana (Makofi)