Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo siku ya kipekee, siku maalum iliyopatikana kwa maamuzi yako makubwa kwa nia njema kabisa ya kuisimamia Serikali, kwa maneno hayo kwa dhati kabisa nakupongeza wewe na kwa kweli umeonesha kwamba yanapofikia mambo haya mazito your very serious, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru pia mimi Benaya Kapinga, hivi karibuni umenipeleke kwenye Kamati hii nzito, Kamati ya LAAC, kwa hiyo, nakushukuru kwa uteuzi napata nafasi ya kuisaidia nchi yangu lakini kuona namna gani Watumishi tuliowapa dhamana wanavyokwenda kutuvuruga, wanavyokwenda kuharibu rasilimali ambazo Seirkali imeziweka kwa ajili ya kusaidia nchi. Kwa hiyo, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimia Spika, nitajielekeza katika maeneo mawili, matatu. Ripoti za Mkaguzi zimetuonesha kuna mapungufu makubwa kwenye utekelezaji wa maagizo na mapendekezo. CAG anasema katika Taasisi za Serikali hizi hususan Halmashauri kuna shida kubwa ya kutekeleza maagizo yanayotolewa. Kwa nini maagizo yanatolewa, au mapendekezo yanatolewa, CAG anapofanya ukaguzi anakutana na vitu tofauti tofatui, anaona dosari tofauti tofauti, ndipo inafikia hatua ya kutoa mapendekezo ili kuondoa hizo dosari. Pia Bunge linapoona kuna dosari hizo ndiyo linakuja kutoa maagizo. Sasa inapofika huyu anayeagizwa hatekelezi yale maagizo inakasirisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, taarifa zinasema mwaka uliotangulia walitoa maagizo zaidi ya Elfu Kumi, kati ya hayo ni maagizo 3,511 tu ndiyo yaliyotekelezwa. Sasa najiuliza wewe ni mwalimu, kule chuo ulikuwa unatoa assignment mwanafunzi harejeshi, unatoa assignment, hivi mwisho wa siku si unajua hatua inayofuata? Nami napendekeza hapa kwa taasisi ama Halmashauri ambazo hazitekelezi haya maagizo kwanza zinaonesha kiburi, jeuri. Kwa nini zinafanya hivyo? Nia ni moja tu Halmashauri za namna hii ni kuzichukulia hatua kali ikiwemo kuziondosha mezani, hakuna haja kuendelea baadhi ya Halmashauri hapa naambiwa zina hoja hizi miaka Kumi, zina hoja hizi miaka saba, kila zinaitwa mezani, zinapigwa maneno zinaondoka, kesho tena…

Mheshimiwa Spika, kwa kweli jambo hili linonesha kupunguza hadhi ya Bunge ambayo inatoa maagizo. Sasa tusikubaliane nalo tuchukue hatua kubwa ikiwemo kuzifukuza hizi Halmashauri na kama zitarejea basi hatua kali zidi ichukuliwe dhidi ya Halmashauri hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee pia suala la upotevu wa mapato, taarifa zinasema kuna upotevu mkubwa sana wa mapato ya Serikali, yako maeneo tofauti tofauti ambayo yanayosababisha upotevu wa mapato ya Serikali ikiwemo wakati wa makusanyo, pia wakati wa matumizi. Katika wakati wa makusanyo, ziko Halmashauri hazipeleki fedha benki, hapa taarifa inasema katika mwaka wa ukaguzi zaidi ya Bilioni 20 hazikupelekwa benki, sasa najiuliza hizi fedha zilienda wapi? Hawa watu wanafahamu sheria iko wazi, ukikusanya ndani ya muda fulani unatakiwa upeleke fedha benki. Sasa kwa vile wanayo mikakati yao na namna yao, Serikali imeanzisha utaratibu mzuri wa makusanyo kupitia POS, inafika baadhi ya sehemu hizo POS zinazimwa, baadhi ya hizo POS zinakusanya fedha hazionekani, baadhi ya hizo POS zinakusanya fedha mtu mmoja ana-ID zaidi ya mbili. Nia hapo ni mbaya sana, nia ovu ya kutaka kutumia hizi fedha za Serikali, sasa Bilioni 20 hazipelekwi benki zinaenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunaambiwa Bilioni 33.9 hazikukusanywa kabisa, kwenye maeneo ya ushuru wa mazao, kodi za pango, mauzo ya viwanja, leseni za vileo, sokoni, pamoja na ushuru wa hoteli hazikusanywi. Sasa hapa ni mipango inayofanywa na baadhi ya hawa watumishi, wanafanya mipango wanachukua kidogo cha chini cha juu wanamwachia Serikali inapata hasara.

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana tuweke maazimio hapa makali, ya kuwataka Wakurugenzi hawa watekeleze Sheria na Kanuni za Fedha, muda mfupi huu wanapokusanya hizi fedha wazifikishe benki na ambaye hajapeleka hizi fedha benki hatua kali ichukuliwe, ikiwemo pia na kumfunga, kwani wezi hawafungwi? Huyu mtu ambaye hapeleki fedha benki kwa maksudi.

Mheshimiwa Spika, nasema nakushukuru kwa sababu ninashuhudia pale tunapofanya mahojiano na Maafisa Masuuli, sababu zingine unaona ni za kawaida mno haifai kabisa. Kwa sababu naona kengele ya kwanza imenigongea na sijui tunachangia dakika ngapi ni dakika Tano ama dakika Kumi? Naona kengele imenigongea Mheshimiwa Spika.

SPIKA: Imegonga ya kwanza, kwa hiyo wewe malizia.

MHE. BENAYA L. KAPINDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Eneo lingine ambalo linatupotezea fedha nyingi ni eneo la uwekezaji. Taarifa hapa imesomwa na Wenyeviti wetu wametuambia, uwekezaji huu kwa baadhi ya Halmashauri wanaufanya na wamelenga kupeleka kwenye maeneo hasa mawili, stendi na soko. Imejidhihirisha maeneo hayo baadhi ya Halmashauri hayana tija. Ningeshauri Sana soko na stendi zijengwe kwenye maeneo labda ya Miji mikubwa na halmashauri za Majiji lakini kule Vijijini tuwe na stendi za kawaida sana ambazo hazina sababu ya kutumia fedha nyingi.

Mheshimiwa Spika, mfano Jiji la Mbeya walikopa fedha kujenga soko la Mwanjelwa, zaidi ya Mabilioni yamewekwa pale na taarifa ya CAG inatuambia deni lile linatakiwa lirejeshwe kufikia 2033, Halmashauri inapaswa kurejesha kila mwaka zaidi ya Shilingi Bilioni Mbili lakini mapato halisi ya pale Halmashauri ni Shilingi Milioni 750 hadi Shilingi Milioni 850, sasa watapata wapi fedha hizo zaidi ya Bilioni na kidogo ili kurejesha benki, tena benki ya kibiashara, hiyo hasara kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya miradi hii wakati mwingine inafanyika pasipo kufanyika kabisa wanaita tathmini na upembuzi yakinifu, lakini cha zaidi kile kinaitwa project plan - andiko la kibiashara, andiko la kibiashara ndiyo litaonesha mradi huu hapa utakaa kwa namna gani, utatoa faida kiasi gani mpaka mwaka gani, sasa watu wanakwenda wanaweka tu mradi pale hawajafanya chochote wanaleta Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, ninaomba hapa kwamba tusikubali kuruhusu mradi wowote pasipokuwa na tathmini, upembuzi yakinifu wa eneo hilo. Lakini tusikubali kuanzisha mradi pasipo kuwa na hili andiko la kibiashara ambalo litatuonesha faida na muda wa kupata faida huo mradi.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee pia miradi iliyotelekezwa. Taarifa ya CAG inatuambia kwamba ipo miradi ya zaidi ya Bilioni 41.5 imetelekezwa kwa muda mrefu. Miradi hii ukiwauliza Maafisa Masuuli wanasema hii miradi ni ya nguvu za wananchi, mwananchi anapoibua mradi maana yake kaona tatizo anataka kuondokana na lile tatizo, kwa hiyo, hii miradi ni muhimu kuliko hata haya masoko na vingine. Mwananchi kaona hapa tuna shida ya zahanati anaona hapa kuna shida, jambo hili tuitake Serikali itenge fedha nyingi najua inatenga fedha lakini iongeze zaidi fedha ili miradi hii iliyoanzishwa na wananchi ikamilike na lengo la kuanzisha ile miradi kwa wananchi litimie kuliko ilivyo sasa tunawavunja moyo sana wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupe mfano mmoja.

SPIKA: Utamalizia na huo mfano.

MHE. BENAYA L. KAPINDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika Halmashauri yangu kuna ujenzi wa zahanati, zahanati ile imejengwa toka mwaka 1995 imepauliwa mpaka leo ipo hivyo hivyo, yaani imeisha kupauliwa. Sasa ukiona eneo inapotolewa huduma utalia, ni kibanda tu kamepigwa bati hapo ndipo wanakotolea huduma, hapa kuna jengo nzuri, fedha imeenda pale, tena wanasema wananchi walikuwa wanachota maji mbali kweli toka mwaka 1995 hadi leo zahanati ya Kilanga Juu Kata ya Mbuje, lakini Maafisa hawa Masuuli wapo, Afisa Mipango yupo miaka inaenda, miaka inaenda hawaoni hata sababu ya kukamilisha ile miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii miradi kama nilivyosema Serikali ipeleke fedha nyingi pia hata Halmashauri zenyewe kuliko kuanzisha miradi mingine ikamilishe hiyo miradi iliyopo. Ahsante sana. (Makofi)