Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami nitoe mchango wangu. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na afya njema.

Mheshimiwa Spika, nawapongeze sana Wajumbe wa Kamati wakiongozwa na Wenyeviti wa Kamati zote tatu kwa kuleta ripoti hii ya uchambuzi wa kina kuhusu hii ripoti ya CAG.

Mheshimiwa Spika, naomba nitofautiane kidogo na Wabunge, wenzangu. Pengine utaniongoza; sijajua role yetu kama Wabunge ni ipi katika kuisimamia Serikali? Je, ni kuishauri Serikali tu na kuisimamia? Je, sisi kama Wabunge tuna hakika kwamba tunaisimamia vizuri? Ni nani asiyejua madudu yanayoletwa na sheria ya manunuzi kwenye halmashauri zetu? Nani hajui mwanya mkubwa wa fedha nyingi za nchi hii zinapotea kwa sheria ya manunuzi? Mbunge gani hajui? Tumefanya nini kwa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Wabunge wengi hapa wametoa mawazo kwamba twende tukawaazimie. Nitoe mfano mmoja, tunataka kumuazimia labda Mkurugenzi wa TANROADS kwa madudu mengi yanayofanywa, na ni kweli kwamba fedha nyingi zinapotea. Hivi ni kweli Mkurugenzi wa TANROADS amepoteza hizi fedha? Sisi kama Wabunge tunaamini Mkurugenzi wa wa TANROADS amepoteza hizi fedha?

Mheshimiwa Spika, unaweza ukamwita Mkurugenzi wa TANROADS akaja na certificates za wakandarasi tatu, nne au tano hazijalipwa. Nani awajibike? Nani anapaswa kuwajibika? Lazima sisi kama Wabunge twende mbali zaidi, siyo tu kuwalaumu watendaji. Wakati mwingine tukizungumza, watendaji wanasema, hawa Wabunge bwana, wanasiasa. Kwa sababu hawaoni tunachokifanya. Hawaoni kwa sababu haya mambo tunayazungumza kila siku.

Mheshimiwa Spika, wakati tunapitia bajeti ya ujenzi hapa, hatukuona tumepitisha fedha kwa barabara zilizoisha? Barabara imeisha mwaka 2021 lakini tumepitisha fedha mwaka huu. Zinakwenda wapi? Zinakwenda kulipa madeni ya Wakandarasi. Nani amezalisha madeni?

Mheshimiwa Spika, tuwe serious kuisimamia Serikali. Hivi ni nani hajui kwenye halmashauri zetu hakuna wahandisi wa kutosha? Katika kuchangia bajeti nilisema, halmashauri zetu hazina wahandisi. Tena wakati ule mimi nilijichanganya kati ya wahandisi na wakadiriaji majengo. Unaweza ukakuta kwenye halmashauri kuna mhandisi lakini hakuna mkadiriaji majengo? Nyumba ya kuingia bati 300, zinanunuliwa bati 400. Nyumba inaingia nondo 10, zinanunuliwa nondo 20. Hatuna mkadiriaji majengo, nani hajui? Nani awajibike?

Mheshimiwa Spika, tunakwenda kumwajibisha Mwalimu Mkuu kwa sababu ujenzi wa shule hajausimamia vizuri. Tunakwenda kumwajibisha DMO kwa sababu kituo cha afya hakijajengwa vizuri, tuko sahihi? Are we serious? Tuna halmashauri ngapi zina wakadiraji majengo? Tuna halmashauri ngani zina wahandisi?

Mheshimiwa Spika, namwonea huruma sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kazi anayoifanya ni kubwa sana na dhamira yake ni njema sana na maono yake ni makubwa sana kwa nchi hii, lakini waliopata dhamana ya kumsaidia Rais wajipime. Kwa sababu akili yangu inakataal unakwenda kwenye halmashauri unakuta madudu.

Mheshimiwa Spika, halafu sasa ukiingia kwenye halmashauri kuna Mkaguzi wa Ndani wa Halmashauri anawajibika kwa Mkurugenzi. Is it fair? Yaani Mkurugenzi ampe mafuta na fedha kwenda kukagua mradi, aende akamkague; atampa? Mkurugenzi atampa usafiri Mkaguzi wa Ndani? Akishaenda kumkagua, hiyo ripoti inasomwa wapi? Siyo sawa, kuna mahali tumepotea. Nashauri, Mkaguzi wa Ndani akae pembeni, awe ni taasisi inayojitegemea. Haiwezekani Mkaguzi wa Ndani akae chini ya Mkurugenzi, amkague Mkurugenzi, siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, mpaka CAG anatuletea madude haya, hivi ni kweli tunasema kwenye Wizara zetu hakuna wakaguzi? TAMISEMI, hakuna wakaguzi? Huku kwenye Maji hakuna wakaguzi? Ujenzi hakuna wakaguzi tumtegemee CAG? Haya madude yapo. Nasi kama Bunge siyo mara yetu ya kwanza kuyaona. Sio CAG peke yake ndio katuonesha! Haya madude yapo!

Mheshimiwa Spika, kuna shida mahali. Kama tuko serious kuna shida mahali. Tuchukulie mfano mwingine, kwenye majengo hayo hayo; hivi ni kweli BOQ ya kujenga darasa moja Dar es Salaam itafanana na ya Njombe? Ndiyo, tunataka majengo yetu yote yafanane kama vituo vya afya vyote; jengo linaweza kuonekana kwa ndani linafanana, lakini ile BOQ ya ndani ni kweli inafanana? Hivi Njombe leo unajenga darasa moja lina feni sita darasani. Umeshafunga mafeni, Njombe, ni kweli!

Mheshimiwa Spika, hayo madarasa yanajengwa Dar es Salaam kwenye joto, Njombe huwezi kuweka feni, lakini unaweza kukuta darasa limejengwa wanakwambia BOQ ndio inavyosema. Hivi Njombe unahitaji dirisha la futi sita kwa sita? Dar es Salaam unahitaji dirisha la futi sita kwa sita kwa sababu ya joto, kuna mahali tunakosea.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano kwenye halmashauri yangu, tumepewa milioni 470 kujenga madarasa. Juzi nilikwenda kukagua, madarasa yote yamekamilika, yote yana feni zinafanya kazi wala umeme hatujui tutapata lini, lakini wamefunga mafeni na kila kitu, lakini hawajajenga choo, hela imeisha. Milioni 28 zimetumika kuingiza umeme kwenye madarasa lakini vyoo havijaisha. Mkurugenzi yupo, Mhandisi yupo, kila mtu yupo na hamna majibu. Ukiwauliza wanakwambia hiyo ndio BOQ, yaani usipofanya hivyo maana yake wewe kibarua chako kiko hatarini.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya umbali uliopo kutoka Liwale kwenda Dar es Salaam ambako wanatakiwa wakanunue vitu vya pamoja wamenunua mpaka bulb, wamekusanya kila kitu kiko stoo, lakini darasa haliwezi kutumika, shule haiwezi kufunguliwa, vyoo hakuna, jengo la maktaba hakuna, fedha zimeisha. Ukienda kuwakagua wametumia vizuri huwezi kuwashtaki. Ndio ile aliyosema kwamba mtu mwingine anaweza akafanya jambo zuri tu kwa nia njema likawa na faida, lakini kwa sababu hajafata Sheria ya Manunuzi akaadhibiwa.

Mheshimiwa Spika, mwingine anaweza aka-mess-up akafanya madudu tu, lakini kwa sababu amefata Sheria ya Manunuzi anaoneka yuko happy. Sasa tufike mahali sisi kama Wabunge, sio tu kuishauri Serikali, twende tuisimamie na inaposhindwa kutekeleza maazimio yetu tuwe na la kufanya. Kama hatuna la kufanya, hapa tutakuwa kama tunapiga story tu, si sawa, kuna shida mahali.

Mheshimiwa Spika, mfano mwingine, MSD inadaiwa na Serikali fedha nyingi tu, lakini halmashauri wanaidai MSD. Sasa ni wajibu wa Mkurugenzi MSD aamue fedha za halmashauri aendeshee taasisi yake, halmashauri wakose dawa au afanyeje sasa?

Mheshimiwa Spika, halmashauri wamepeleka fedha MSD, lakini Serikali hawajapeleka fedha MSD, Mkurugenzi atumie hela zipi kuendeshea ile taasisi? Shida ipo. Lazima kama tuko serious tufumue mifumo yote ya ukusanyaji wa fedha na utumiaji wa fedha, lazima tuwe makini kwamba, fedha tumekusanya kiasi gani, zinakwenda kufanya nini na anayetakiwa kuwajibika ni nani?

Mheshimiwa Spika, leo hii wakienda kumwajibisha Mkurugenzi wanawaonea tu, kule mahali kuna shida. Nimezungumzia Sheria ya Manunuzi, sasa narudi kwenye hoja za CAG. Nafikiri kama Bunge tufike mahali tuseme kama hoja imejirudiarudia ni mara ngapi na kwa muda gani? Tuweke kikomo. Lini hoja ifungwe? Tuweke kikomo na nani awajibike hoja isipofungwa? Vinginevyo CAG anakuja anakwambia hoja zisizofungwa za mwaka 2018 hizi hapa, hoja mpya ni hizi hapa. Nani ambaye amesababisha hoja hazijafungwa? Kwanza nani ameleta hiyo hoja ya ukaguzi? Kuna shida.

Mheshimiwa Spika, sisi Wabunge tunapopitisha bajeti lazima tuwe makini. Tunapopitisha bajeti Wabunge kama kweli tuko serious tuwe makini. Tunapopitisha bajeti ya miradi iliyokamilika lazima tuseme watuambie hizi hela zilichelewa wapi? Barabara imeisha 2018 lakini utakuta bado kwenye bajeti inatengewa fedha, ukiuliza deni la mkandarasi na haliishi, sisi Wabunge tunakubali tu. GAG akija kutustua tunakuwa wakali kwani hakuna kipya mimi ninachokiona hapo kwa CAG alichokileta. Vitu vyote ambavyo kila siku tunaviona, sisi tunabishana sana na Mheshimiwa Waziri wakati tunapitisha Bajeti ya Ujenzi tulibishana naye sana hapa. Akasema hizi fedha tulizopitisha mwaka jana hakuna mradi mpya uliotekelezwa? Akasema hapana zile tumetekeleza mradi uliopita, hatukupitisha hapa? Sasa kitu gani kipya?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka kengele ya pili imegonga…

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, asante.