Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Haizuiliki kuzungumzia masuala ya kisera ya Wizara ya Afya ambayo wamesema kwamba kila kijiji kiwe na zahanati na kila kata iwe na kituo cha afya. Sera wanaimiliki wao, TAMISEMI kazi yao ni kusimamia na kuratibu utekelezaj wa sera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo langu kubwa ni ceiling ambazo Serikali huwa inailazimishia mikoa. Kwetu sisi Tabora kwenye ceiling ya TAMISEMI ambayo ndiyo tumepitisha bajeti, kwenye sekta yote ya afya ni shilingi bilioni 19 kwa mkoa mzima. Kama tunataka kutekeleza sera inavyotaka kila kijiji kiwe na zahanati na kila kata iwe na kituo cha afya, kwenye Wilaya ya Sikonge peke yake tunahitaji vituo vya afya 18 vipya na zahanati mpya 41. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo langu linakuja, nimewauliza watalaam wa afya kule kwangu, ili ujenge kituo cha afya kwa mujibu wa miongozo ya Wizara ya Afya, majengo, vifaa, wataalam na kila kitu unahitaji zaidi ya shilingi bilioni mbili. Ili ujenge zahanati kwa mujibu wa miongozo ya Wizara ya Afya kwa kila kitu unahitaji zaidi ya shilingi milioni 500. Ina maana kwa Sikonge tu tunahitaji zaidi ya shilingi bilioni 65, tutazipata wapi na tutakamilisha lini ikiwa Serikali inatupangia ceiling ya shilingi bilioni tatu kwenye wilaya yetu? Kwa hiyo, hilo ni tatizo kubwa na tusije tukaiacha hivyo hivyo, Serikali kwa ujumla wake inatakiwa ilifanyie kazi suala hili ili kusudi kweli sera hii iweze kutekelezeka, hilo lilikuwa la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu Maafisa wa Maendeleo ya Jamii. Zamani hawa tulikuwa tunawaita Mabwana na Mabibi Maendeleo. Taarifa ya Waziri kule mwisho kwenye majedwali inaonyesha kabisa kwamba Wilaya ya Sikonge tuna Maafisa Maendeleo ya Jamii 14 na wote wako Makao Makuu ya Wilaya. Katika kata zangu 20 hakuna Afisa Maendeleo ya Jamii ambaye yuko kwenye kata. Nashauri Serikali iachane na maneno, wakati wa utekelezaji ndiyo huu, hapa kazi tu, tuhakikishe kwamba hawa Mabibi na Mabwana Maendeleo wanafika kwenye kata ili kusudi waweze kuhamasisha maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, ni kuhusu Vyuo vya Maendeleo ya Jamii na Vyuo vya Wananchi hivi (FDCs). Tumeambiwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba tuna Vyuo tisa vya Maendeleo ya Jamii nchi nzima. Napendekeza vyuo hivyo viboreshwe zaidi ili vifikie hatua ya kutoa diploma na hata digrii ili kusudi tusomeshe watu wengi zaidi kwenye hii fani ya maendeleo ya jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu hivi Vyuo vya Wananchi (FDCs - Folk Development Colleges), kama tulivyokuwa tunazungumza siku tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na hata siku ya kujadili Wizara ya Viwanda, tunahitaji watu wengi, tunahitaji staff, tunahitaji nguvu kazi ambayo itaajiriwa kwenye viwanda vidogo vidogo, kama hivi Vyuo vya Maendeleo ya Jamii vitaendelea kufundisha elementary sijui kushona nguo, kitu ambacho hata fundi cherehani wa mtaani anaweza akakifanya, naomba hivi vyuo vibadilishwe viwe VETA za maendeleo ya jamii ili kusudi viweze kusaidia uchumi wetu na maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne ambalo nataka kuchangia ni ukatili wa kijinsia. Kwa mwaka mmoja tu 2015, kwenye hii hotuba ya Mheshimiwa Waziri aliyotupatia, inaonekana Mikoa ya Dar es Salaam, Mbeya, Morogoro, Pwani na Tanga imeongoza katika ukatiri wa ngono, hiyo mikoa mitano. Wana matukio zaidi ya 300 ya ukatili wa ngono, hii mikoa niliyoitaja. Mikoa ambayo ina matukio chini ya 100 ni Mkoa wa Simiyu peke yake, hii ni hatari!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nchi iwe na programu maalum ya elimu dhidi ya ukatili wa ngono, hilo ni suala la aibu sana, linatakiwa lipatiwe programu maalum kabisa. Sijaiona hiyo programu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, naomba sana suala hili lizingatiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwenye haya matukio ni mashambulio ya kudhuru mwili na matusi. Haya mambo ni mabaya na yanasababisha chuki katika jamii na familia nyingi. Imeonekana Mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Morogoro tena na Rukwa ina matukio zaidi ya 1,000, hii ni hatari. Mikoa yenye matukio chini ya 100 ni Dodoma, Kilimanjaro, Lindi, Mara, Mwanza, Mbeya, Pwani, Ruvuma na Simiyu tena. Hivi kule Mara walitumia mbinu gani kupunguza matatizo haya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Mheshimiwa Waziri apeleke timu Mkoa wa Mara kuchunguza kuona hivi wale watu, kwa sababu wanaaminika wana hasira sana, wamepunguzaje haya matukio ya kushambuliana ili elimu ile iweze kutumika kwenye mikoa mingine hasa hii ambayo ina matukio mengi ili kupunguza matatizo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tano ambalo nataka kuchangia ni uchangiaji wa halmashauri kwenye Mfuko wa Wanawake - WDF. Katika halmashauri ambazo zimetajwa kwenye hotuba ya Waziri ni Halmashauri moja tu ya Iringa ndiyo imeonekana imechangia kwa asilimia 100. Kuna Halmashauri kama ya Kinondoni, Kigoma Ujiji, Sumbawanga, Tabora Manispaa, Misungwi, Mwanza na nyingine nyingi ziko chini ya asilimia 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hatua gani ambayo Serikali inachukua sasa kuhakikisha kwamba watu wanaboresha michango yao angalau inafika zaidi ya asilimia 50 na kuendelea. Kuna baadhi ya halmashauri mchango wao ni chini ya asilimia moja, hii ni serious. Naomba suala hili liweze kuchukuliwa kwa umakini wa hali ya juu kwa sababu hawa wanaotekeleza ni waajiriwa wa Serikali, wanatakiwa waheshimu miongozo inayotolewa na Serikali, wasiendelee kufanya kinyume na utaratibu ambao umeelekezwa na Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo nataka kuchangia ni suala la wazee. Naomba Serikali isimamie kikamilifu utekelezaji wa maelekezo yake ya kisera. Kwa mfano, suala la huduma bure za afya kwenye hospitali za Serikali na vituo vya afya na zahanati kwa wazee lisibaki kwenye maneno wala kwenye makaratasi. Najua Waziri wa Afya alitoa Circular mwezi Februari lakini imeendelea kutoheshimika kwenye maeneo yaliyo mengi hapa nchini. Naomba sana ufuatiliaji wa karibu uwepo ili hiyo Circular iweze kutekelezwa isibaki kwenye karatasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wakati mgombea wetu wa Urais alizungumzia kuhusu pesheni ya wazee. Hili ni suala ambalo ukizunguka kwenye vijiji unaulizwa na wazee, bwana tuliambiwa kuhusu pesheni imefikia hatua gani? Naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama aweze kulitolea maelezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuna Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake na Mfuko wa Vijana, sawa, lakini wazee wanauliza Mfuko wa Wazee vipi? Kwa maana ya hawa wazee waliostaafu, Mfuko wa Wazee Serikali inatufikiriaje sisi? Kwa sababu Mheshimiwa Waziri wa Afya ndiyo anahusika na masuala ya wazee, naomba wazee wangu wa kule Sikonge wasikie leo anazungumza kuhusu Mfuko wa Wazee atauanzisha lini? (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Wataona baadaye usiku. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ya kwangu yalikuwa ni hayo lakini naomba nimalizie kwa vituko vya kisiasa. Ukistaajabu ya Mussa walisema utaona ya Firauni. Kule Uganda kilitokea kituko kimoja kikubwa sana jana lakini nisingependa kukieleza kwa kina kila mtu anajua. Kwa hiyo, kumbe Tanzania sisi tuna afadhali katika demokrasia na ni mfano wa kuigwa. Wenzetu wamefikia katika hali mbaya, naomba tuwaombee ili kusudi nchi ile iendelee kuwa na amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja.