Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya nchini, pia kwa jambo kubwa ambalo juzi amezindua la kuhakikisha kwamba anaendelea na kazi ya kumtua Mama kuni kichwani, amekaribia kumaliza ndoo kichwani sasa anaendelea kuni kichwani ili akina Mama na akina Baba watumie Nishati safi kwa ajili ya kupikia.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa naomba nikupongeze sana wewe mwenyewe hasa kwa mjadala huu wa ripoti hizi za ukaguzi kwa kweli umeonyesha umadhubuti na nikiangalia michango inayotokea hapa mikali mikali sijaona ukisema wewe kaa chini, wote waseme kadri wanavyoweza, tunakupongeza sana na sisi tupo na wewe kwa sababu tunajua hili ndio jukumu lako kubwa la msingi kuhakikisha kwamba unalinda maslahi ya watanzania kupitia rasilimali zao.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusikiliza michango ya wenzangu mingi, kama kawaida yangu huwa napenda kukaa upande tofauti kidogo kama kioo. Sasa nikianzia na suala hili la TANROADS kufikia malipo ya Bilioni 68. Kwa ajili ya riba kwa makandarasi, nikasema sawa ni TANROADS wamefanya hivyo lakini kitovu cha suala hilo kiko wapi? Kitu gani kinasababisha wanashindwa kuwalipa hawa makandarasi kwa wakati? Kwa sababu ni lazima tukubali pia upande wa ufanyaji kazi, mtu yeyote yule anayefanya kazi yako na wewe akishakugundua kwamba huna tabia ya kulipa kwa wakati anajilinda, kujilinda anaweka kipengele kwamba ukichelewa kunilipa itabidi na mimi nipate riba kidogo.

Mheshimiwa Spika, ninachouliza, kwa sababu kama ni barabara ili zitangazwe ina maana tunakuwa tumeshatenga bajeti kwa ajili ya kazi hiyo, kitu gani kinasababisha hatulipi kwa wakati? Ni TANROADS wanakuwa na fedha hawataki kulipa? Au hizo fedha wanazipata kutoka maeneo mengine kiasi kwamba yale maeneo hayawapatii fedha kwa wakati? Kwa hiyo, nataka hili tunapotibu tutibu mstari wote mpaka mwisho tupate jambo ambalo ni la uhakika badala ya kuanzia na sehemu tu iliyotokea tatizo tukaacha mzizi ulikoanzia. Kwa hiyo, nadhani hata watu wa Hazina wanalo la kuzungumza hapa kwa maana Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, suala la pili napenda kuzungumzia hizi Halmashauri zetu. Kuna Halmashauri za matajiri na Halmashauri za makabwela, mimi binafsi natoka kwenye Halmashauri za makabwela ambayo kipato chao ni kidogo sana kutokana na makusanyo yao. Sasa kuna hili suala la kula fedha mbichi, siungani kabisa na Halmashauri katika suala la kula fedha mbichi, lakini yawezekana kichochezi cha kula fedha mbichi ni pamoja na mifumo yetu wenyewe tulivyojiwekea. Kwa sababu, kwa mfano tukimaliza kujadili Bajeti yetu mwezi Juni, tunapoingia mwezi Julai mpaka mifumo kuweza kufunguka na kuruhusu Halmashauri kuanza kutumia fedha inachukua muda mrefu wakati mwingine mpaka miezi miwili mifumo haijafunguka.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna Sheria zinagongana ukipata msiba wa mtumishi inabidi umsafirishe, umzike, kwa kutumia taratibu zilizowekwa kwenye Sheria. Wakati huo hakuna fedha, Mkurugenzi unategemea atachukua fedha za mfukoni mwake? Ataenda kula hela mbichi kwa kutumia wale watu wake ili mradi aweze kwenda kuzika. Kwa hiyo, nadhani pia na taratibu hizo za kuchelewesha kufungua mifumo ziangaliwe au Halmashauri ziwekewe fedha kidogo za kutumia wakati mifumo hiyo inaendelea labda na taratibu za kiuhasibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuzungumzia suala la Kamati katika ukurasa wa romani ya pili ya summary yao ambayo imeshauri kwamba Serikali iongeze mtaji kwa Mashirika kama TANESCO, TPDC na STAMICO, hilo ninawapongeza sana wameliona, hatuwezi kwenda tunalalamika tu lazima tena tushauri na mambo mengine ambayo yanafanya haya mashirika yetu tunayoyategemea yafanye vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia TANESCO na TPDC ni ndugu hawa, wako katika Kamati moja ya Nishati na Madini, lakini unakuta huyu TANESCO kwa sababu anawajibu wa kuhakikisha umeme unapatikana anamkopa ndugu yake TPDC. TPDC naye kwa kuogopa kwamba nitasema nini kwa sababu anategemea ruzuku kutoka Serikalini anaruhusu madeni ya kukopwa na TANESCO, kwa hiyo unakuta ni Shirika moja linamtafuna mwenzake lakini wote wanatekeleza majukumu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa mazingira kama hayo iko haja wakati mwingine tunapoona ukweli na hali halisi Serikali yenyewe ichukue hayo madeni, deni kama la TPDC ichukue yenyewe halafu ile fedha ambayo inalipwa kidogo kidogo na Shirika kama la TANESCO ilipwe Hazina baada ya Hazina kuwa imeshachukua deni lake na imeshamrejeshea TPDC fedha zake ili iweze kuendelea na shughuli zake zinazohitajika hasa za kiutafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi tunayo changamoto kubwa ya kuhama kutoka kwenye nishati ambayo inaitwa nishati isiyosafi kwenda kwenye nishati safi. Tunategemea utafiti mwingi ufanyike, tunategemea mambo makubwa ya haraka ya kuhakikisha kwamba tunasonga mbele kiteknolojia na kiujuzi kwa ujumla yanafanyika.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa unakuta Mashirika kama TPDC, TANESCO na STAMICO wanakosa fedha za kutosha. Kwa mfano, ukiangalia kazi za STAMICO; na hapa niwapongeze kwa kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwao; wanatakiwa kufanya tafiti mbalimbali kwenye nchi. Maeneo mengine hata hayafikiki kiurahisi, hakuna barabara, kwenye misitu, tunajua kuna rasilimali kama za madini, lakini vifaa wanavyotumia ni duni sana; magari sehemu nyingine hayafiki. Walitakiwa watumie hata ndege au helikopta ziwafikishe huko wafanye kazi za utafiti, lakini unakuta hakuna, kwa hiyo tunazungumzia kugawana gawana kilichopo. Tujipange sasa ili tuweze kupata fedha za kutosha ili taifa liweze kupanga matumizi yake bila kutegemea sana mikopo.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo mimi naungana na Kamati iliyopendekezwa kwamba haya mashirika matatu ya kimkakati waongezewe fedha ili waweze kutimiza wajibu wao ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala lingine ambalo limezungumziwa, mradi wetu mkubwa sana wa maji wa Mwalimu Nyerere. Mimi nimeamua kuwa balozi wa kujitegemea kwa mradi ule. Nasema hivyo kwa sababu mradi ule Watanzania wote wanauangalia. Mradi ule wote tunajua kwamba tukifanikiwa Tanzania itakuwa imepiga hatua, itakuwa pia imeshiriki kikamilifu katika kupunguza nishati zinazochangia hewa ukaa na kuwa kwenye nishati safi.

Mheshimiwa Spika, Mradi ule mashine yake moja itakayowashwa ambayo itakuwa inatowa mega watt 235, haifanani hata na mashine nyingine zote zinazozalisha maji katika nchi hii. Mradi ule kweli umechelewa lakini unakwenda vizuri; na hivyo nataka Watanzania waelewe hivyo, mama Samia amejitahidi. Hata leo Marehemu Mzee Magufuli angefufuka angemkumbatia dada yake mama Samia, kwamba kazi umeiweza, kazi inaendelea, mradi unaenda vizuri. Sasa, katika kuchelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kweli kuna mmoja wapo lazima akubali lazima kasababisha, sababu ni nini? Na hiyo hatuwezi tukafumba macho, kumbana aliyehusika katiaka kuchelewesha. Hata hivyo tunasema ni bora kuchelewa lakini tupate kazi iliyo sahihi, kwa sababu ule mradi ni very sensitive. Sasa, nilikuwa nasikia hapa kwa nini watoe riba kwa ajili ya kulipa fedha hizo za dola; lakini jamani si ni jambo la kawaida? Hivi leo wewe ukienda kununua dola yako exchange rate kama ni shilingi 2,000 kesho ukaikuta 2,500 utaipata dola kwa shilingi 2,000? Ni jambo lipo. Kwa hiyo mimi najaribu kusema tu kwamba sisemi ufanyike ubadhilifu, isipokuwa sitaki sisi Wabunge tuishi kama mambumbumbu wa kusema dola ukiinunua jana lazima leo itakuwa bei ile ile, tutakuwa hatujitendei haki, lazima tuwe wakweli kwatika haya tunayoshauri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nasema kwamba katika hilo hakuna ambaye atakuwa mzembe, aseme kwamba hela yake basi yeye alipwe kwa hasara, hilo jambo halipo jamani, tuambizane ukweli.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa misingi hiyo tunapozungumzia kuchukua hatua, kwa maeneo yale ambayo tunasema kwamba yamekuwa na ubadhilifu, basi tuhakikishe uchunguzi wa kina unafanyika na wale wanaostahili wachukuliwe hatua; na si tu kusema halafu tukamgusa ambaye hausiki. Nasema hivyo kwa sababu nimesikiliza michango hii tangu mwanzo, wengi wao wanaongea kwa ujumla jumla, angalau mmoja aligusa akashauri kwamba labda pengine Katibu Mkuu wa Wizara fulani, lakini wengi wanasema tuchukue hatua kwa ujumla jumla. Kwa ujumla jumla tunamchukulia hatua nani?

Mheshimiwa Spika, Kamati mnaficha nini kutuambia ni fulani na fulani? Kwa nini tunaenda kijumla jumla? Tunamwaogopa nani? Kama hatuwezi kusimama tukasema ni fulani na fulani wamehususika basi tusiseme haya ya kujaribu tu kuzungumza kwamba Wabunge tumesema, hapana. Hapa tungekuwa sasa hivi tunazungumza kauli moja, kwamba katika hawa wote safari hii hapana, lazima tuchukue hatua. Lakini sasa kwa sababu tunaongea kwa ujumla tutajikuta kwamba tumeongea tunatoka, hakuna kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi naungana na wanaosema ikiwezekana uunde Kamati Teule ifuatilie kwa kina katika yale maeneo ambayo yamezidi ubadhilifu, ikiwemo hiyo KADCO na maeneo mengine ili tuchukue hatua ya ukweli bila kusingizia na bila uoga, haki haina uwoga. Ahsante sana.

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Mhandisi Stella Manyanya hebu tusaidie, hapo kwenye jumla jumla ndio sijaelewa hapo. Kwenye, kwamba Wabunge walikuwa wanachangia jumla jumla, hebu fafanua kidogo.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ingekuwa ni mimi ninaposema tuchukue hatua; kwa mfano kwa Shirika kama TANESCO, nitasema kabisa. Katika eneo hili ubadhilifu umefanyika either na Mkurugenzi au na Mhandisi fulani au timu fulani ambayo yenyewe inajulikana kabisa ilihusika na hiyo kazi yaani nisingefichaficha. Ili tunapoenda kushughulikia sasa wa kuwaadhibu tunawapa. Sasa CAG taarifa yake haijamtaja mtu, unakuta huku hivyo hivyo na sisi tunachangia vilevile, lakini ubadhilifu unaonekana. Sasa, mimi naona kidogo hiyo inaleta uzito namna ya kushughulikia hilo jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.