Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hii taarifa ya Maguzi Mkuu wa Serikali (CAG). Kwanza, napenda nimshukuru Mungu kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuongea kwa niaba ya wana Mbogwe, kuhusiana na taarifa ya madudu yaliyooneshwa na CAG.

Mheshimiwa Spika, hii taarifa ni ndefu, imebainisha vitu vingi. Nimejitahidi kadri ya uwezo wangu kuchambua madudu yaliyooneshwa na CAG. Anasema amepitia jumla ya taasisi za Serikali na mashirika 331, nikajitahidi kujumlisha hasara zinazooneshwa na CAG ambazo zinaonekana za mwaka 2020/2021 mwezi wa Saba japo zipo mpaka za mwaka 2018 na 2019.

Mheshimiwa Spika, naomba nifafanue vizuri. Kwa vile imetajwa na Halmashauri yangu ya Mbogwe kwamba imo kwenye hati yenye mashaka. Napenda niliambie Bunge lako Tukufu kwamba haya mambo nilisema mapema kwamba nilikuwa siyajui hapo mwanzo, lakini kwa kuwa yamejirudia, naomba nifafanue vizuri ili wananchi wasiwe na hofu kwamba sasa msimamizi wao pamoja na Baraza la Madiwani imekuwaje tena?

Mheshimiwa Spika, ijulikane kwamba hizi taarifa zilizopita ni za siku nyingi. Kwa sasa hivi Mbogwe tuko salama. Nimeikuta Mbogwe ikiwa na mapato ya Shilingi milioni 700 lakini kwa sasa hivi tuko kwenye bajeti ya Shilingi bilioni tatu. Kwa maana hiyo, kwa kifupi sisi tulipoingia tulibainisha na tukaazimia, kipindi hicho Waziri wa TAMISEMI akiwa dada yangu Mheshimiwa Ummy, anajua ripoti ile ambayo tuliazimia Baraza la Mbogwe. Kwa hiyo, nimeona nifafanue tu kwa kifupi hapo.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye asasi. Nimeangalia wanakamati wa Wizara hii pamoja na taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu, wameongea kwa hisia kubwa sana. Rafiki yangu wa Magu jana nilimwambia usiwe na wasiwasi tiririka tu, nami huku naandika. Kweli nilikuwa naandika kabisa maana jambo hili ni kubwa. Jambo hili tukilifumbia macho litatuharibu. Naona aibu kufa kwenye meli ambayo naona inaenda kuzama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite kushauri, nimejumlisha hasara zote nikaona Shilingi trilioni 4,590 ni fedha nyingi sana ambapo nikifanya mgao kwa halmashauri zetu 184, tunaweza kujenga barabara kwa ile Ilani yetu yenye page 303. Tuna uwezo wa kujenga lami za kuunganisha Mkoa na Wilaya tukamaliza hiyo ahadi tuliyoitoa kwa kila Mbunge hapa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa zimetajwa taasisi nyingi ukianza na ukurasa wa tatu, imezungumzwa TANESCO kwamba ililipa Dola za Kimarekani 153.43. Uki calculate kwa rate ya leo unapata karibia Shilingi milioni 360. Ukurasa wa pili huu imeonekana Shilingi bilioni 68 ambazo zimelipwa kupitia Shirika la Serikali hii TANROAD, kwa hiyo, naona aibu kwanza kuendelea kuwazungumza hawa watu kwa kuwa wameshazungumziwa na watu wengi, sasa nijikite kushauri tu.

Mheshimiwa Spika, kwa vile jambo hili umelileta kwetu tushauri kwa niaba ya wananchi na mjumbe hauawi, naomba kabisa uchukue hatua kikwelikweli. Najua hakuna Mbunge ambaye hataazimia kwa kitendo hiki kilichofanyika. Sisi sote humu tunapigiwa kura, kuanzia Waheshimiwa Mawaziri, huwa wanapitia kwanza kwenye hii michakato na baadaye wanateuliwa kuwa mawaziri huko. Kwa hiyo, katika maamuzi tutakayoyaazimia kesho, naomba tuungane kwa nia moja ili Taifa letu tuweze kulibadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kumvumilia mtu ambaye anakula kodi za wananchi. Nikiangalia nilikotokea jinsi wanavyolipa kodi wale wafanyabiashara wadogo, ni jambo la kusikitisha, lakini unaona hapa kuna wafanyabiashara wakubwa hawalipi kodi, wanategemea kesi zao ziishie Mahakamani na walishajua hizi sheria zetu ni dhaifu, niungane na mwenzangu Mheshimiwa Tabasam, kuna kila sababu hizi sheria kuziboresha ziseme kabisa vizuri mtu anapoonekana na makosa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nitakuwa labda nje sana, sheria hizi zinatakiwa zitaje, endapo mtu anaonekana ana makosa ya kuhujumu uchumi, pesa za watu wanyonge waliojichanga ili kuisaidia Serikali mtu akazitafuna, zitamke kunyongwa kabisa. Huyo mtu akionekana anyongwe ili watu waogope, kwa sababu sheria tulizonazo sasa hivi watu hawaogopi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeshuhudia Mawaziri wengi wanapiga kelele hata kwenye miradi. Unamwona Waziri anapiga kelele kabisa kwamba hapa hela zimepigwa, zimeliwa; akitoka Waziri, watu wanaendelea kula bia. Hata mimi mwenyewe Mbunge huwa najaribu kufuatilia sana; mimi ni mkali sana kwenye jimbo langu, maana najua likiharibika nimo mimi, itakuwa ni aibu ya hatari sana. Hawa wasomi walishasoma hizi sheria wakaona zina udhaifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namwomba Mwanasheria Mkuu wa Serikali atusaidie Wabunge kwa hilo, tuziboreshe sheria zetu zizungumze vizuri. Hapa hazijazungumza vizuri kwa sasa hivi, tutakuwa tunapiga kelele tu Waheshimiwa Wabunge, mwisho tutaonekana wa ajabu, Bunge tunapigwa vita, Bunge la ajabu, halina maamuzi. Sijui tufikie maamuzi halafu watu wasichukuliwe hatua, tutakuwa wageni wa nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya tumesema watu wakamatwe, hawakamatwi, tunakutana nao mitaani, wanatutukana; tuna watoto wana watoto, tufanye nini?

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nikodemas Maganga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilitaka kumpa taarifa Mheshimiwa Maganga kwamba Bunge lililopita, nadhani Bunge la Kumi na Moja, tulitoa maazimio humu ndani, Waziri wa TAMISEMI alikuwa Mheshimiwa Jafo, tukasema sheria ile inayolinda fedha za asilimia 10 ipo wazi. Mkurugenzi wa halmashauri yoyote ambaye atakusanya fedha halafu akashindwa kutoa asilimia 10 ya nne nne mbili achukuliwe hatua hapo hapo, kwa sababu fedha zitakuwa zimeshakusanywa naye amekula hizo hela, ajifute yeye mwenyewe kwenye cheo. Alizungumza Mheshimiwa Jafo humu ndani, lakini mpaka leo kuna Wakurugenzi mia moja na kitu wamekula hizo hela na wapo.

SPIKA: Mheshimiwa Nikcodemas Maganga unapokea taarifa hiyo?

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo ya baba yangu kwa mikono yote miwili. Tusifanye vitu vya kuchekesha. Huwa namwangilia Waziri Mkuu anavyofanya ziara kwenye baadhi ya Mikoa na Wilaya, yuko serious kweli baba wa watu, lakini kila akifanya maelekezo sijui kama wale watu huwa wanakamatwa na sijawaona sijui wako Magereza ya nani? Aliwahi kuja kwangu nikiwa bado sijawa Mbunge, nilikuwa mfanyabiashara tu, akatoa maelekezo. Alipotoka tu watu wakaanza kunywa bia. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa sheria zetu naomba ziseme kabisa. Kwanza zimlinde Waziri Mkuu, akisema kitu, hiyo ni Serikali, aheshimiwe, huyo ni msaidizi mkuu wa Rais. Haiwezekani kila siku tuwe tunazungumza mambo yale yale kama ndugu yangu alivyonipa taarifa. Hivi tunamaliziana heshima. Ndiyo maana watu wengine huwa wanaichukia sana siasa, maana sheria hizi hazijazungumza vizuri. Yaani Mbunge wa Tanzania ni kama mpiga debe wa stendi, ulishaona wapi? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumza haya maneno kwa masikitiko makubwa sana. Haiwezekani Mbunge anahangaika hapa Dodoma miezi mingi anapanga matrilioni, ukiangalia hata kwenye akaunti zao sidhani kama kuna Mbunge ana Shilingi trilioni moja kwenye akaunti yake huko. Leo ndugu zangu wa Kamati wamezungumza kwamba kuna KADCO, haijulikani ni ya nani? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwanza, Wabunge, Bunge hili liseme kabisa, kwanza kuanzia hao mliokuwa mnakaa nao kwenye kamati, waanze nao. Mii nilishawahi kushuhudia pale Kahama, anakumbuka Waziri Mkuu, mwaka 2020 kuna wafanyabiashara walikuwa wanapunguza sukari kidogo tu, tena robo kilo kila mfuko; walishughulikiwa na Mkuu wa Mkoa peke yake. Watu walikuwa na vitambi, mabilioneam wakaishi pale Magereza ya Shinyanga, discipline ikapatikana. Leo watu waliomo ndani ya Serikali hawakamatiki jamani! Haipo sababu sasa ya kutengeneza Serikali! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, namhurumia sana mama yangu. Jana nimeona tumesamehewa kama Shilingi bilioni 31, anajitahidi sana, lakini hizi fedha kama hazina ulinzi, pamoja na misamaha hii ambayo tunapewa na Mataifa, sisi wenyewe kama hatujisimamii, siku moja haya Mataifa yatatudharau, hayatatukopesha tena fedha. Kwa sababu tutakopeshwa na tutafika sehemu tusikopesheke, kila tunachokopwa kinaliwa. Wabunge tunarudi hapa hakuna kinachozingatiwa. Mwisho wa siku watoto wetu wataambulia nini? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiangalia ukurasa wangu wa pili hapa unasema mikataba sijui ilikuweje, TANESCO hapa, hii kampuni ya Symbion, hawa watu wote wakamatwe mara moja. Hili zoezi ni dogo sana, ila ukilikuza linakuwa kubwa, lakini zoezi hili linaweza likamalizwa na mtu mmoja, tena Waziri wa Mambo ya Ndani, hili suala lipo ndani ya uwezo wake. Mara moja tu akitangaza kesho waripoti Dodoma hapa, kwani shida iko wapi? Waripoti wenyewe kesho, tuone trilioni zetu zote hizi, tukajenge barabara, tukafanye na mambo mengine, maisha yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ukomee hapo, nisije nikayarefusha sana mwishowe nitavuruga, maana nikiwa na hasira huwa nashindwa kuchangia vizuri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)