Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili nami jioni ya leo nichangie hoja zilipo mezani. Pia kwa upekee wake nitajikita zaidi kwenye hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kama ambavyo imebainisha na taarifa ya CAG kwa hesabu za kuishia Juni, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya leo nitakuwa na hoja kubwa mbili tu. Hoja ya kwanza ni uwezo wa halmashauri zetu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kwa mujibu wa taarifa ya CAG kumekuwa na changaomoto katika kutekeleza miradi ya maendeleo katika mamlaka zetu za Serikali za Mitaa, na kwa ridhaa yako naomba nitoe mifano michache;

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na Halmashauri ya Mji wa Newala, sekta ya elimu peke yake Shule ya Msingi Lidumbe mradi wa nyumba ya mwalimu umetelekezwa tangu mwaka 2015. Shule ya Msingi Mnaida, mradi wa nyumba ya mwalimu umetelekezwa tangu mwaka 2012. Shule ya Msingi Mcholimbili, mradi wa nyumba ya mwalimu tangu mwaka 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri ya Wilaya ya Bumbuli, madarasa 25 yametelekezwa, nyumba za walimu 37 zimetelekezwa, maabara 26, zahanati 12 na mabwalo ya chakula mawili. Halmashauri ya Kasulu miradi 34 ambayo imeanzishwa na jamii imetelekezwa, haikuweza kukamilishwa. Nimalizie kwa mifano michache na halmashauri ya Kigoma Ujiji, kati ya miaka mitatu hadi kumi na moja, miradi yenye thamani ya shilingi 1,251,000,000/= imetelekezwa bila kukamilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini maana yake hapa? Maana yake ni kwamba, fedha za Watanzania walipa kodi zimeangamizwa bila kuleta tija yoyote. Jambo kama hili, sisi kama wabunge, wawakilishi wa wananchi ambao ndio walipa kodi haipaswi kulinyamazia. Hapa tumezungumzia fedha ambazo zimeingizwa kwenye miradi hii ya muda mrefu ambayo haikukamilika na haitumiki. Maana yake ni kwamba fedha za Watanzania zimekwenda bila kuleta tija. Hilo ni eneo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo kikubwa ni kwamba halmashauri zetu hatujazijengea uwezo katika maeneo mawili; eneo la kwanza ambayo ni usimamizi na eneo la kutoa ruzuku kwa halmashauri zetu katika kutekeleza miradi ya maendeleo. Baadhi ya Wabunge hapa wamechambua, kwamba kumekuwa na uwiano usioridhisha wa kutoa ruzuku za miradi ya maendeleo katika halimashauri zetu. Zipo halmashauri ambazo zimepata ruzuku zaidi ya asilimia 100 na zipo ambazo zimepata ruzuku chini ya asilimia 40, kwa mujibu wa taarifa ya CAG. Hii imesababisha ndio matokeo ya miradi zaidi ya miaka minane, imetelekezwa na haina tija yoyote.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ni matokeo ya haya ni usimamizi usioridhisha wa mamlaka zetu za Serikali za mitaa kwenye vyombo vyake vya usimamizi. Hapa kwa upekee kabisa niseme, regional secretariat (Sekretarieti za mikoa). Kimsingi, kwa utendaji usioridhisha wa halmashauri zetu, mtu wa karibu kabisa ambaye ndiye mkono wa karibu wa ofisi ya Rais, TAMISEMI wa kusimamia ni Ofisi ya Mkuu wa Mkoa chini ya Sekretarieti ya mkoa. Lakini, ni kiwango gani sekretaieti zetu za mikoa tumeziweshesha kusimamia halmashauri? Ni kwa kiwango gani watendaji pamoja na maafisa waliopo pale kwenye sekretarieti za mikoa wamejengewa uwezo wa kusimamia Mamlaka zetu za Serikali za Mitaa.? Ni kwa kiwango gani mamalaka zetu za sekretarieti za mikoa watendaji wake wamekuwa na uzoefu wa kutosha wa usimamizi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Hili ni janga na ni jukumu la Serikali kuliangalia eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili mahsusi ambalo ningependa kulitolea uchambuzi katika taarifa hii ni mfumo wa ukusanyaji wa mapato. Halmashauri 46, kwa mujibu wa taarifa ya CAG zenye POS 1,355 hazikuwa katika mfumo wa kukusanaya mapato mpaka ripoti hii inatolewa. Pia halmashauri nane zilipoteza POS 34 na halmashauri 27 zilifanya marekebisho ya ankara kiasi cha shilingi bilioni moja milioni mia sita na ushee, bila kiambatisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma kulikuwa na utaratibu katika halmashauri zetu, watendaji wasio na nia njema ya nchi hii kuiba fedha za wananchi wakati tukitumia mfumo wa stakabdhi za kuandika kwa mikono maarufu kama HW5. Kulikuwa na utaratibu wa kupoteza vitabu kwa makusudi wakati tayari fedha zimekusanywa, halafu watendaji wasio na nia njema walikuwa wanapiga hizo fedha. Tulipoleta mifumo hii ya ukusanyaji wa fedha kwa njia za kielektroniki tulidhani utakuwa ndio mwarobaini wa kurekebisha mapungufu haya. Badala yake watendaji hao hao wasiokuwa na nia njema na nchi yetu, wamekuwa wakitumia mifumo hii hii ya kielektroniki, kwa maana ya mashine za kukusanyia mapato lakini bado wanapiga kwa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoambiwa kwamba halmashauri nane zilipoteza POS maana yake ni kwamba walikusanya halafu fedha za Watanzania zikaenda mifukoni mwa watu binafsi halafu baadaye wanasema POS zimepotea. Hili ni jambo ambalo haliwezi likakubalika. Pia tunaambiwa kwamba katika halmashauri ambazo zimakaguliwa na CAG kwa taarifa ya kuishia Juni, 2021 kiasi cha shilingi bilioni 17 za mapato zilikusanywa na POS lakini hazikupelekwa benki. Maana yake ni kwamba zilibaki kama fedha mbichi na zilitumika zikiwa fedha mbichi bila kupelekwa benki. Sasa haya mambo ni msiba mkubwa sana katika taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwasababu hiyo nilikuwa na mapendekeo yafaatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, kama nilivyosema, kwamba haya yote ni matokeo ya mifumo ya usimamizi isioridhisha. Kwa hiyo jukumu la kwanza kabisa ni kuimarisha mfumo wetu wa usimamizi hususani kuimarisha eneo lile la regional secretariat ili Ofisi ya Rais TAMISEMI isipate shida sana, kwamba Maafisa wa TAMISEMI kuhangaika kuwa wanashuka kwenye halmashauri. Tuna halmashauri 184 nchi nzima, watumishi au maafisa wa Wizara hawatoweza kutosheleza kuzunguka kwenye halmashauri 184 kwaajili kutoa au kujenga uwezo kwa watendaji wetu au kusimamia miradi. Jukumu la regional secretariat ni kuisaidia Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa maana ya Wizara, kwa niaba yake, kuzisimamia hizi halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uwezo wa kiutendaji na wa kiuzoefu wa maafisa waliopo kwenye regional secretariat zetu unakuwa si kwenye kiwango ambacho wangeweza kuzisimamia halmashauri hizi.

Mheshimiwa Mwenyekti, jambo lingine ambalo nimeliona ni changamoto na nipendekeze hapa ni muundo wenyewe uliopo kati ya watendaji wa halmashauri na muundo wa regional secretariat.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Ofisi ya Rais TAMISEMI ilipitisha muundo ambao ulinakwenda kutekelezwa na watendaji wetu wa halmashauri lakini muundo huu kimsingi si muundo ambao ulikuwa shirikishi. Sisi kama Madiwani, Wabunge hatukushirikishwa katika kupendekeza muundo huu. Hata hapa Bungeni sidhani kama kulikuwa na semina ya kuonesha kwamba tunaenda kutekeleza nuundo huu. Sasa tunapotekeleza muundo ambao umetoka juu na kushuka tu kutekelezwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa bila kuhusisha wadau wakaingiza inputs zao matokeo yake ndiyo haya ambayo CAG anakuja kuyaibua. Utaratibu huu wa mapungufu ya kiutendaji na usimamizi yataendelea kuwa ni mwiba katika nchi hii mpaka pale ambapo muundo wa usimamizi utakapokuwa umekaa vizuri.

Mhehimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.