Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuzungumza jioni hii ya leo kuchangia taarifa za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, CAG. Nitachangia kwenye Kamati mbili, Kamati ya LAAC pamoja na Kamati ya PAC. Kabla ya kuchangia ninaishukuru sana Serikali inayoongozwa na Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuwekeza fedha nyingi katika miradi ya maendeleo ambayo kupitia hiyo miradi ndiyo taarifa nyingi tumezipata hapa ambazo zinaonesha kwamba kuna hoja nyingi katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane kwanza na Mbunge wa Kasulu, Mheshimiwa Vuma, ambaye asubuhi aliongea kwa kirefu kuhusiana na mapengo katika Bodi za Wakurugenzi kwa Taasisi zetu nyingi za Umma. Kwa kweli kutokuwa na Bodi za Wakurugenzi au kuwa na Bodi za Wakurugenzi zenye mapungufu kumepelekea kuwa na mapungufu makubwa katika uendeshaji wa taasisi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachelea kusema kwamba ilitolewa taarifa hapa kutoka kwa Mheshimiwa Mtaturu, akitolea mfano wa Klabu ya Simba na ubora wa Bodi yake ya Wakurugenzi, akazungumzia namna ambavyo timu fulani maarufu ambayo jana ilicheza katika mashindano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika, namna ambavyo imeshindwa ku-cope na mazingira ya utawala bora ambayo yanafanikishwa katika Klabu ya Simba, ambayo tangu wameunda Bodi ya Wakurugenzi imara, miaka mitano iliyopita wamekuwa wakifanya vizuri kwa kucheza hatua za makundi katika mashindano ya vilabu Barani Afrika na kuweza kuiwakilisha nchi yetu katika hatua mbalimbali ikiwemo kufika hatua ya robo fainali. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ngoja kwanza kuna taarifa, nafikiri Mheshimiwa alikuwa anataka kuelezea pia kwamba Bodi hiyo inasaidiaje kwenye timu za ndani au ni nje tu. Karibu Mheshimiwa Getere. (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji anayechangia, mchango huo haupo kwenye taarifa za Kamati. Mimi naomba aifute.(Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane unapokea taarifa?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hii taarifa kwa sababu hii mifano tunayoitoa ni mifano muhimu. Wenyewe mmeona jana hali ilivyokuwa.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji anachozungumza ni vitu ambavyo vinagusa watu rohoni na yaliyotokea jana ni mambo ya kawaida, sasa huwa yanatokea bahati mbaya hata yeye mwenyewe yalishamtokea, sasa ningeomba hiyo hoja aiache. (Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane zingatia yaliyokutokea huko nyuma, unapoke taarifa ya Mheshimiwa Musukuma?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninaipokea kwa lengo la kuweka msisitizo kwenye jambo hili. Tunawaombea ndugu zetu katika mechi ya marudiano kwa sababu hakuna nafasi nyingine ya kuwasaidia ni kupitia mazungumzo kama haya ndiyo maana tumeamua kusema, kwa hiyo, wana nafasi ya kujirekebisha kwenye mechi ya marudiano. Tulisema tangu kwenye Kikao cha Bajeti wakati tunachangia Wizara ya Michezo kwamba jamani hakuna dhambi kwenda kusikiliza ushauri kutoka kwa watani! Hapa kwenye Bunge hili tunae mmoja wa wanabodi ya Wakurugenzi ya Simba.

T A A R I F A

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa kuna taarifa, Mheshimiwa Rama eeh!

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, tungemuomba mchangiaji ajielekeze kwenye hoja zilizoko mezani. Simba na Yanga hapa siyo hoja ya leo ya kujadili. Kwa hiyo, ajielekeze kwenye hoja za Kamati zilizosomwa za PAC LAAC na PIC. Tuendelee mbele nchi hii inataka kusikiliza mawazo yake siyo habari za Simba na Yanga.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Ndulane unapokea taarifa?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Siipokei taarifa lakini niishie hapo na ninawatakia kila la kheri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijikite kwenye taarifa rasmi za Kamati zetu tatu, especially zile mbili za LAAC na PAC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia na Kamati ya LAAC, taarifa ambayo waliitoa ilikuwa ni nzuri, imebainisha madhaifu mengi ambayo yalitokana na taarifa ya ukaguzi ya CAG. Nikienda moja kwa moja kwenye usimamizi wa miradi, dosari zilijitokeza nyingi lakini nijikite pale ambapo ilionekana kwamba kuna upotevu kwenye interest ambazo zilikatwa kutokana na malipo ya jumla ya Shilingi Bilioni 664,0 ambayo ilizalisha interest jumla Shilingi Bilioni 68.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukailaumu taasisi ya TANROADS wakati kumbe mfumo wetu wa malipo una changamoto nyingi. Huko tulikotoka tulikuwa tunatumia mfumo katika kulipa na kuandaa malipo ya Wakandarasi. Katika mfumo huu unatoa siku 56 ambapo inatakiwa Serikali imlipe Mkandarasi anapokuwa amefanya kazi, kinachoonekana kule nyuma tulikuwa tunakwenda vizuri kwa sababu hizi siku 56 zilikuwa zinagawanywa, siku 28 Consultant anatakiwa aandae certificate, iwe approved, ipitiwe lakini mwisho wa siku wanaisukuma TANROADS. Ikifika TANROADS kuna kitengo kinaitwa IDA kinasimamia malipo yote ya kazi za wale development partners, yale malipo ambayo yanafadhiliwa na wafadhili mbalimbali wa nje ya nchi. Tukifika pale nao wanapitia zile certificates, pamoja na wale Engineers wanapitia, wakishapitia inaenda kwa Desk Officer wa Wizara ya Fedha na Mipango ambapo kazi yake ni kuangalia usahihi wa yale malipo ambayo yameandaliwa au yale madai ambayo yameandaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatimaye akishapitisha, na ni kazi inachukua kama masaa mawili tu, baadae zile claims zinarudi TANROADS, baadae zinakwenda kwa development partner naye anajiridhisha, malipo yako sawa. Baadaye yanalipwa ndani ya siku 56 Mkandarasi anakuwa tayari ameshalipwa. Hii ilikuwa inazuia kupatikana kwa hizi interest ambazo tunaziona leo kwenye hoja za ukaguzi za CAG.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichopo sasa hivi certificate ikishaandaliwa ikitoka kwa Mkandarasi inakwenda kwa consultant, ikitoka kwa consultant inakwenda TANROADS wanaipeleka Wizara ya Ujenzi. Pale kuna maafisa wasiopungua wawili wanashughulikia lakini ikitoka hapo inakwenda kwa Permanent Secretary wa Wizara ya Fedha na Mipango. Ikitoka pale kuna Maafisa zaidi ya Kumi wanasimamia, unapita katika mlolongo wa Maafisa zaidi ya Kumi. Ikitoka hapo inarudi TANROADS. TANROADS baadae inarudi kwa development partner, nae anajiridhisha hatimaye ndiyo inalipwa. Kwa hiyo kuna maafisa zaidi ya 15 wanahusika na malipo na matokeo yake ndiyo haya sasa tunayoyaona leo kwamba kuna fedha nyingi Serikali inalazimika kuongeza kulipia ile miradi kwa sababu ya uwepo wa riba kutokana na ucheleweshaji wa malipo. Kwa maana zile siku 56 zinakuwa hazitoshi kulipa Mkandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwa upande wa Serikali zetu za Mitaa, nilikuwa naperuzi vizuri sana kuhusiana na wingi wa hoja za ukaguzi katika Halmashauri zetu. Katika Halmashauri zetu nilitazama Halmashauri ya Korogwe nilikuta ina hoja ambazo hazijafungwa 91. Halmashauri ya Bumbuli ilikuwa na hoja za ukaguzi 89 ambazo hazikufungwa mpaka wanakuja kwenye Kikao cha LAAC. Kuna Halmashauri ya Msalala ilikuwa na hoja 61. Halmashauri ya Bunda ilikuwa na hoja 56 ambazo hazijafungwa mpaka wanafika kwenye Kamati ya LAAC. Nini nataka kusema?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiasi kikubwa, Halmashauri hizi zimekuwa na hoja nyingi za ukaguzi ambazo wameshindwa kuzijibu kwa sababu wameshindwa kuvitumia vizuri vyomba vya ndani ya Halmashauri katika kukabiliana na hizi hoja. Kwa mfano, tunavyo vitengo vyetu vya ukaguzi wa ndani, vile vitengo vimekuwa havitumiki sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwanza, haviwezeshwi kufanya kazi zake sawasawa. Vifaa vya usafiri hawana, vifaa vya ofisi hawana lakini mwisho wa siku hata ile audit independence imekosekana kwa hiyo wanajikuta mwisho wa siku, wale Wakaguzi wa Ndani wamekuwa kama ni watoto yatima ndani ya Halmashauri wakati ilitakiwa wawe msaada mkubwa kwa Maafisa Masuuli katika kuisimamia halmashauri. Kwa hiyo, ombi langu katika jambo hili ni kwamba Halmashauri ziwatumie vizuri Wakaguzi wa Ndani katika kipindi hiki cha mpito, na kwakuwa Wizara ya Fedha iliahidi kwamba itarekebisha mfumo wa usimamizi wa hawa wakaguzi wa ndani. Ninawaomba waharakishe ule mchakato ili mwisho wa siku ikiwezekana hawa Wakaguzi wa Ndani wapelekwe katika Ofisi ya Chief Internal Auditor wa Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna hii inaitwa Audit Committee, hii ndiyo msaada kwa Maafisa Masuuli wa Halmashauri ambao ni Wakurugenzi. Kuwepo kwa Kamati hii inawezesha kwanza kufanya mapitio ya fedha zinazoidhinishwa za bajeti kabla hazijaenda kwenye Baraza la Madiwani na kabla hazijaja huku kwenye Bunge. Pia mwisho wa siku inawezesha kupitia hoja zote za ukaguzi wa ndani na nje ili kuwezesha kuboresha kile ambacho kinaonekana kina dosari. Kwa hiyo, ninaomba pia Maafisa Masuuli wazitumie vizuri hizi Kamati za Ukaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)