Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia hoja hizi tatu zilizoko mbele yetu. Niwapongeze sana Wenyeviti kwa kuwasilisha hoja nzuri ambazo tunazichangia leo hii. Nitajikita kwenye maeneo mawili; eneo la kwanza nitaanzia na KADCO, Kiwanja cha Ndege cha KIA.

Mheshimiwa Spika, Kiwanja cha Ndege cha KIA ni kiwanja cha ndege cha Serikali kwa asilimia 100. Kabla ya mwaka 2009 Kiwanja cha Ndege cha KIA kilikuwa na wanahisa wanne, mwanahisa wa kwanza alikuwa ni Serikali ambaye alikuwa anamiliki asilimia 24, mwanahisa wa pili alikuwa ni McDonald kutoka Uingereza ambaye alikuwa anamiliki asilimia 41.4, mwanahisa wa tatu alikuwa South Africa Infrastructure Fund ambaye alikuwa anamiliki asilimia 30 na mwanahisa wa mwisho alikuwa Inter Consult Limited ya Tanzania ambayo ilikuwa inamiliki asilimia 4.6.

Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka 2009 mpaka 2010 Serikali ilifanya maamuzi ya kununua wanahisa wengine ambapo Serikali ilinunua wanahisa hao kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Kampuni ya McDonald ambayo ilikuwa na asilimia 41.4 ilinunuliwa kwa dola za kimarekeni milioni 2.752.

(b) Mheshimiwa Spika, Kampuni ya South Afrika, South Africa Infrastructure Fund ambayo ilikuwa na asilimia 30 ilinunuliwa kwa dola za kimarekani milioni 1.994

(c) Mheshimiwa Spika, na kampuni ya Kitanzania Inter Consult Limited iliyokuwa na asilimia 4.6 ilinunuliwa kwa dola za kimarekani 839,737.

Mheshimiwa Spika, kwa maelezo hayo kuanzia mwaka 2011 au mwisho wa 2010 KADCO ilikuwa ni kampuni ya Serikali kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya KADCO inaendeshwa au imeundwa kwa mujibu wa Sheria ya Kampuni, Sura Namba 212 ya Mwaka 1978. Kwa sasa Kampuni ya KADCO inasimamiwa na Wizara, lakini iko chini ya Msajili wa Hazina na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya KADCO pamoja na Bodi ya Kampuni ya KADCO wanateuliwa na Serikali, wote wanateuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya KADCO inalipa kodi. Inalipa kodi Corporate Tax na inalipa Service Levy kwenye Halmashauri ya Hai, pia, Kampuni ya KADCO inalipa dividend. Kwa mfano, mwaka 2016/2017 ililipa shilingi milioni 555; mwaka 2017/2018 ililipa milioni 583; mwaka 2018/2019 ililipa shilingi bilioni moja; mwaka 2019/2020 haikulipa kwa sababu, kulikuwa hakuna wasafiri kutokana na ugonjwa wa Covid; mwaka 2020/2021 vilevile haikulipa dividend kwa sababu ilikuwa kuna ugonjwa wa Covid-19 na wasafiri walipungua sana. Na hizi dividends zote zililipwa kwenye Serikali.

Mheshimiwa Spika, wafanyakazi wote wa KADCO ni Watanzania, hakuna mtu mgeni wote ni wafanyakazi wa Tanzania na karibuni ni vijana wadogo tu. Kwa vile mtu akisema kama ni kampuni ya wageni, Hapana, haelezi ukweli na sio sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya KADCO, kama nilivyosema, inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria za Makampuni, haiko chini ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kwa sababu, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege iko chini ya Sheria ya Uwakala wa Serikali (Agencies). Hivi tulivyo tuko katika mpango wa kuibadilisha sheria hiyo na kuifanya iwe mamlaka au authority, pengine huko mbele ndio tunaweza tukaziunganisha taasisi hizi mbili, lakini kwa sasa ni taasisi ambazo zinaendeshwa kwa sheria tofauti.

Mheshimiwa Spika, nafikiri hili lilikuwa ni jambo muhimu kulieleza kwa sababu, leo limezungumzwa sana kwamba, Kampuni ya KADCO ni kampuni ambayo inamilikiwa na watu wa nje wakati si kweli. Kwa asilimia 100 inamilikiwa na Watanzania, yaani ni Serikali.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam unaendeshwa na kampuni gani?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam unaendeshwa na Kampuni ya TAA… (Makofi)

SPIKA: Ngoja kidogo Waheshimiwa Wabunge.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, unaendeshwa na Kampuni ta Tanzania Airport Agency (TAA).

SPIKA: Wakati Serikali ikilipa pesa 2009 na kununua zile hisa na kurejesha uwanja kwenye umiliki wa asilimia 100, ule mkataba unazungumziwa sasa hivi ni mkataba gani? Baada ya kuwa Serikali imeshalipa pesa zote?

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ni mkataba ambao ni wa Serikali kwa asilimia 100, lakini kwa jina unaendeshwa na Kampuni ya KADCO. Ni jina tu, lakini kampuni yenyewe ni ya Serikali kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, naweza kuitwa Peter ama nikaitwa Mbarawa, lakini hakutakuwa na tofauti yoyote ndio nitakuwa ni mimi tu.

(Hapa, baadhi ya Wabunge walipaza sauti)

SPIKA: Unajua tunapata hii changamoto kwa sababu, sasa hivi Waheshimiwa Wabunge hatuamshi jambo jipya, tunatazama Taarifa za Mkaguzi wa Hesabu za Serikali amesemaje. Mkaguzi wa Hesabu hicho alichokisema, Kamati wamepata nafasi ya kuonana na Wizara na hao watu wa KADCO na TAA, bado inaonekana kuna changamoto.

Ukisoma taarifa ya Kamati yetu wanazungumzia mkataba kwamba, mkataba unaisha Juni, 2023. Ni mkataba gani kwa sababu, KADCO kimsingi ile iliyokuwepo awali ni kwamba, haipo, ndio msingi, kisheria ni kwamba ile kampuni iliyokuwepo awali sasa haipo kabisa. Kama haipo haya mazungumzo ya mkataba yanatokana na nini? Hilo moja. (Makofi)

La pili, kwa nini hiyo KADCO wakati Serikali iliponunua haikurejesha TAA kama ambavyo TAA inafanya Dar-es- Salaam ifanye na huko kwa sababu, haya yote yasingejitokeza kama CAG hakuonesha kuna shida? (Makofi)

La tatu, pesa umeeleza hapa na niwapongeze sana Serikali kwamba, mnafuatilia kwamba, KADCO inalipa pesa. Sasa hata wewe unaona ni KADCO inalipa pesa, sio Serikali inajilipa pesa. Hii KADCO imezishikilia wapi hizi pesa ambazo kwa kawaida zinashikiliwa sehemu nyingine halafu yenyewe ndio inailipa Serikali? (Makofi)

Hayo tu Mheshimiwa Waziri, halafu tuendelee na michango mingine.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, hili la kwanza kama ulivyosema, mkataba unaisha tutalifanyia kazi, hilo sitaki kulizungumza sana naomba tulichukue tukalifanyie kazi tuone mkataba unaishaje na tunafanyaje, lakini kuna mpango wa Serikali ambao sisi wenyewe tunataka kuhakikisha kwamba, KADCO inarejea kwenye TAA hiyo tunao mpango, lakini kwa sasa kwanza tubadilishe Sheria ya TAA ambayo inasimamia Kiwanja cha Dar-es-Salaam, kiwanja cha Mwanza na viwanja vingine.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kama nilivyosema TAA sasa hivi inasimamiwa na Sheria ya Uwakala (agencies), kwa vile tunachotaka kufanya ni kuhakikisha kwamba TAA inakuwa mamlaka na baada ya hapo mchakato wa kuhamisha KADCO utaendelea. Mazungumzo yameanza muda mrefu ya jambo hili kwamba KADCO lazima iwe chini ya TAA, hilo tunaendelea kulifanyia kazi, hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Spika, pesa zinawekwa wapi, pesa kama kuna akaunti mbalimbali zinawekwa. Katika Mashiriki yote ya Serikali mengi yanaweka pesa zao katika akaunti zao BOT na ikifika wakati wakulipa dividend inatoa BOT inaipelekea Serikali, kama taasisi zingine zilivyo kama TPA na nyingine zote ambazo huwa kunakuwa na akaunti maalum ambayo inawekwa BOT, wakitaka kutumia kawaida wanaomba kibali kama taratibu zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, naomba hilo kwa ufafanuzi wa jambo hilo, lakini kwa ufupi tutalichukua na tutalifanyia kazi kuhakikisha kwamba mwisho wa siku KADCO inarudi chini ya TAA.

Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, mimi nitakupa tena nafasi, siyo leo ili hayo mengine ukayafanyie kazi. Nitakupa nafasi tena Jumamosi wakati wanahitimisha Wenyeviti wetu, Mawaziri mtapata nafasi ya kufafanua mambo mbalimbali na wewe Mheshimiwa Waziri pia utapewa.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, sawa.

SPIKA: Itaturahisishia ili Bunge liweze kufanya maazimio ambayo kwanza yanatekelezeka, pili yana uhalisia wa huko nje. Mheshimiwa Waziri utatusaidia kufafanua hii KADCO akaunti yake ipo pia BOT? Kwa sababu ni ya Serikali asilimia mia moja, halafu ulisema unayo mambo mawili kwa hiyo hili la KADCO umeshatoa maelezo, haya mengine ambayo nimeuliza kama ulivyosema unalichukua utalitolea ufafanuzi Jumamosi. Hilo la pili sasa nakupa fursa, maana ulisema una mambo mawili, karibu sana.

WAZIRI WA UJENZI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nina mambo mawili, jambo la pili lilizungumzwa kuhusu viwanja vya ndege sasa hivi vinasimamiwa ujenzi na TANROADS kwa nini visisimamiwe na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA). Ni kweli jambo hili uamuzi ulifanyika mwaka 2017 ambapo instrument ilibadilishwa na viwanja vya ndege kupelekwa TANROADS, vilipelekwa kwa kipindi hicho kukiwa na sababu za msingi lakini baada ya muda mrefu tukaona hizo sababu hazipo na sasa tuko kwenye mchakato wa kurejesha baadhi ya ujenzi chini ya TAA. Kuna ujenzi ambao umeanza mfano, hapa Msalato tumepata pesa za ADB itakuwa ni vigumu sasa kuanza kutoa uwanja wa Msalato chini ya TANROADs kwenda TAA kwa sababu mchakato wenyewe unakuwa mrefu na kazi imeanza. Kwa vile, viwanja ambavyo vitaanza kujengwa sasa hivi ujenzi utasimamiwa na TAA kama Sheria ya ICAO inavyosema.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba kuwasilisha. Ahsante sana. (Makofi)