Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. DKT. HAMISI A. KINGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na niwapongeze Wenyeviti wa Kamati zote tatu pamoja na Wajumbe wao kwa kazi kubwa waliyofanya ya kutuletea taarifa zilizosheheni uchambuzi wa kina juu ya mambo mbalimbali yanayohusu mustakabili mwema wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nitaanzia pale alipoishia Mheshimiwa Simon Msonge kuhusiana na KADCO kuweka taarifa sawa tu. In fact KADCO ilipokuwa inaingia Mwaka 1998 Mwezi Julai wakati wanasaini mkataba ilikuwa imeshasajiliwa kama kampuni yenye malengo ya kwenda kuendesha Kiwanja cha Ndege Kilimanjaro miezi mitatu kabla lakini kwenye mkataba wake na Serikali Taasisi hii ya KADCO ilikuwa inapewa mkataba wa miaka ishirini na tano, Concession’s Agreement (mkataba wa uendeshaji), lakini mkataba huo utaweza kuhuishwa kila baada ya miaka 15, lakini hauna kiwango cha fee au charge yeyote ile ambayo KADCO itaenda kulipa Serikali. Kampuni hiyo baada ya kusajiliwa miezi kadhaa baadaye ikaiuzia Serikali ya Tanzania asilimia 24 ya hisa. Kwa hiyo Serikali akawa sehemu ya hiyo kampuni ya KADCO.

Mheshimiwa Spika, pamoja na masharti hayo ya ajabu ya mkataba huo, mkataba ambao kimsingi haukuweka vifungu vya ukomo, kampuni hiyo ya KADCO pamoja na Serikali kushindwa kuivunja kwa sababu hakukuwa na ukomo baada ya maamuzi ya Baraza la Mawaziri mwaka 2009, Serikali ika-resort kununua zile hisa za wanahisa wengine ambao walikuwa Kampuni ya South Africa ilikuwa inaitwa SAIF ilikuwa kampuni ya Uingereza ilikuwa inaitwa Mott MacDonald International, lakini pia kulikuwa na kampuni ya Tanzania ya Inter-Consult ambayo ilikuwa na hisa asilimia 4.6 tu wakati wale Mott MacDonald walikuwa na zaidi ya asilimia 41, nawale SAIF walikuwa wana asimilia 30. Serikali ikakopa pesa takribani bilioni 12.5 (5.3 USD) ikanunua zile hisa za wale wanahisa.

Mheshimiwa Spika, maamuzi ya Baraza la Mawaziri yalikuwa yanaelekeza kwamba zile hisa zikinunuliwa hasahasa uendeshaji ya Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro utapelekwa chini ya mikono ya TAA.

Mheshimiwa Spika, katika hali ya kusikitisha ni kwamba mpaka leo kile kiwanja kinaendeshwa na Kampuni ya KADCO. Sasa ukijiuliza kama maamuzi ya Baraza la Mawaziri yalikuwa kwamba baada ya zile hisa kununuliwa na Serikali ikakopa Benki ya CRDB 5.3 milion USD na TAA wale wakalipa kufikia mwaka 2014 wakawa wamemaliza lile deni, kwa nini bado kuna KADCO mpaka leo? Hupati majibu. Hata hivyo, KADCO wale wanaendesha ile kampuni ambayo asilimia mia inamilikiwa na Serikali kupitia TR msajili wa Hazina na mkataba wao ulihuishwa tena mwaka 2008 kwa sababu katika ule mkataba wa awali mkataba una uhai wa miaka 25, lakini ikifika miaka 15 unahuishwa tena, kwa hivyo ulihuishwa tena mwaka 2008 kabla hata ya ile miaka 15.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye hili unaona wazi kwamba jinsi ilivyoanzishwa hii KADCO na jinsi ilivyokuja kumpa Serikali asilimia 24 na jinsi baadaye Serikali ilivyokuja kununua zile hisa pale mwanzoni na jinsi ambavyo hii KADCO mpaka leo bado inaendelea kuendesha na kusimamia shughuli za uendeshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro, kuna harufu kubwa ya upigaji kwamba KADCO ni dili tupu. KADCO inanuka rushwa, inanuka mipango na hatuelewi wale waanzilishi walikuwa akina nani? Kwa nini walianzisha kampuni hii na akina nani halisi walio nyuma ya hii KADCO ambao mpaka leo wanaendelea kuipa mafao na mafanikio ambayo haipo kihalali?

Mheshimiwa Spika, wafanyakazi wake waliajiriwa na private company, lakini mpaka leo bado wapo wanakusanya mapato pale, hatujui yanaenda wapi, CAG hajui yanaenda wapi. Kama wana mkataba wa Concession Agreement tulimhoji Katibu Mkuu alipokuja mbele ya Kamati yetu, akasema KADCO inaendelea kuendesha ule uwanja kwa sababu kuna Concession Agreement ambayo ilisainiwa mwaka 1998. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukamwambia sasa hiyo Concession Agreement inabaki kwa masharti yapi? Kwa sababu mkataba wa ukodishwaji maana yake kuna kiwanja cha pesa ambacho unalipa. Kwa hivyo sasa wale KADCO hawalipi chochote Serikalini, lakini wanakusanya na kile wanachokikusanya wanakipeleka wapi na wanakusanya kwa Mkataba upi au kwa makubaliano yapi? Unakosa majibu. Walishindwa kujibu, tukawapa muda watuletee na mpaka leo hawajawahi tena kuleta majibu ya ziada. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kingwangalla nalinda muda wako. Hebu nisaidie, hii KADCO inaitwa KADCO kule BRELLA ni nani mmiliki halali wa hii Kampuni kwa sasa? Ni nani mmiliki? Bado ni wale waliokuwepo ambao walishalipwa ile asilimia 100 iliyolipa Serikali ama kuna mahali hapo imebadilika imekuwa ya Serikali? Yaani kwamba nikienda BRELLA leo nitawakuta wale wamiliki au naikuta Serikali?

MHE. DKT HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi KADCO inamilikiwa na Serikali ya kwa asilimia mia moja chini ya Msajili wa Hazina toka huo mwaka 2010.

SPIKA: Sasa, samahani nakuuliza wewe kwa sababu unaonekana unazijua sana hizo taarifa na mimi nataka nizijue. Kama Serikali ilishanunua hii Kampuni maana yake ni ya Serikali.

MHE. DKT HAMISI A. KIGWANGALLA: Ndio.

SPIKA: Ni mahali gani inatokea tena kurejea kwa wale watu ambao walikuwepo tangu mwanzo?

MHE. DKT HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Nataka kuelewa tu siyo kwamba wewe ndiyo Serikali, maana hii sasa ni ya kwetu sisi, hii ni taarifa ya Kamati, kwa hiyo nataka nifahamu vizuri.

MHE. DKT HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, nakuelewa vizuri na actually huo mkanganyiko unaoupata wewe na ndiyo mkanganyiko alioupata CAG na ndiyo mkanganyiko tulioupata sisi na ndiyo maana tunaona kwamba hakuna haja ya kuendelea…

SPIKA: Labda swali langu la mwisho. Kama Serikali imeshalipa asilimia mia moja huo mkataba unatambuliwaje mpaka kuna maswali ya kuhuishwa wanahuisha kitu gani ambacho hakipo? Kwa sababu Serikali si ilishanunua asilimia moja? Sasa, ni mkataba gani tena unaoendelea mpaka unahitaji kuhuishwa tena na ukasema haujaisha, haujaisha vipi, wakati…

MHE. DKT HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, Mkataba ulisainiwa Mwaka 1998, ilipofika mwaka 2008 kukawa na hoja kwamba KADCO wameshindwa kufanya uendelezaji kadri ulivyokuwa mkataba wa awali wa mwaka 1998 na hivyo Mkataba ule uvunjwe. Sasa katika kikao cha Baraza la Mawaziri ikaonekana kwamba waende waka-negotiate ili kuvunjwa ule mkataba. Wale KADCO ambao ni wabia wa Serikali kwa kipindi kile cha awali wakakataa kuvunja ule mkataba, walipokataa kuvunja ule mkataba ndipo Serikali sasa ikaamua kununua zile hisa za wale wanahisa wengine ambazo nimesema alikuwepo Mott MacDonald International alikuwa na asilimia 41, alikuwepo SAIF alikuwa na asilimia 30, alikuwepo Inter-Consult Limited alikuwa na asilimia 4.6 na Serikali alikuwa na asilimia 24. Kwa hivyo Serikali akawalipa wale ili waondoke.

Mheshimiwa Spika, kabla ya mkataba ule Serikali kuamua kununua zile hisa mwaka 2009, mwaka mmoja nyuma 2008, mkataba ule wa awali wa concession agreement ile ikahuishwa upya mwaka mmoja kabla, kwa hivyo inapaswa kuisha mwaka 2023. Leo hii wanasema wanaendelea kuitumia KADCO kuendesha Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro kwa kutumia concession agreement. Sasa concession agreement na nani? Kama KADCO ni mali ya Serikali kwa asilimia 100, Serikali inampa kampuni nyingine tena ambayo ni ya kwake haki ya kutekeleza majukumu ambayo yangepaswa kutekelezwa na TAA.

Mheshimiwa Spika, wakati huohuo kwenye maamuzi ya Baraza la Mawaziri, maamuzi yalisema hivi categorically kabisa, very explicitly kwa lugha ya kisheria kwamba, share za KADCO za wale wabia binafsi zinunuliwe na Serikali na sikishanunuliwa na Serikali Uwanja wa Ndege wa KIA urudishwe chini ya TAA ili auendeshe kama ambavyo anaendesha viwanja vingine vyote vya ndege, ikiwemo kiwanja kikubwa zaidi hapa nchini cha Dar-es-Salaam, lakini hilo halijawahi kufanyika toka 2010 mpaka leo. Sababu wanayosema ni kwamba, kinachofanya wasiiondoe KADCO ni concession agreement ambayo ilisainiwa wakati Serikali akiwa kwenye ubi ana wadau wa sekta binafsi hao niliowataja. Kwa hivyo, ndiyo mkanganyiko tunaousema.

Mheshimiwa Spika, unachokiona kwa kuwa, kule kwenye KADCO wanakusanya mafao na yale mafao sasa hayaji kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina yanaenda kwenye ile kampuni ya KADCO, ndiyo tunasema kuna harufu ya kwamba, pengine hii KADCO inawanufaisha baadhi ya watu ambao wako nyuma yake, ndiyo maana hawataki kuiondoa. Nafikiri nimejieleza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakwenda kwenye hoja yangu ya pili. Napenda kuzungumzia suala la mradi mkubwa wa kimkakati wa reli ya kisasa (SGR). Kulitokea hoja hapa nafikiri ilikuwa Bunge la Bajeti ambapo ilionekana kuna utata kwenye namna tenda ya awamu ya tano ya mradi wa SGR ilivyotolewa kwa njia ya single source kwa kampuni inayotokea nchi ya marafiki zetu Republic of China. Ikaonekana kwamba, majibu yaliyotolewa hapa ni kwamba single source kwenye phase five ya SGR imefanya tumepata Mkandarasi kwa gharama nafuu sana na hii ni reli iliyokuwa inatoka Tabora kwenda Kigoma.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge waliochangia ile hoja, nakumbuka, walisema huyo aliyepewa ni yule ambaye ametekeleza awamu ya tatu ambayo inatoka Mwanza mpaka Isaka, kule kwenye ile lane hajafanya kazi yoyote mpaka sasa, huu takribani ni mwaka wa pili hajafanya chochote. Kwa hivyo inakuwaje ameongezewa kipande cha Tabora kwenda Kigoma, hiyo ndiyo hoja iliyokuwepo.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi hoja yangu ni kwamba, mwezi Agosti mwaka huu TRC wametangaza awamu ya sita ambayo inatoka Uvinza kwenda Gitega, nchi jirani ya Burundi kupitia Msongati. Wametangaza open tendering process competitive bidding ushindani unaruhusiwa, kwa maana hiyo wamerudi kwenye kile ambacho walikikataa. Sasa kama single sourcing ambayo wameitumia kwenye kipande cha kutoka Tabora kwenda Kigoma imetupa ahueni kwa nini kwenye awamu hii ya sita wamerudi tena kwenye ushindani wakati mwanzoni walisema ushindani haulipi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilipenda kuhoji suala hilo na pengine kuomba Bunge lako Tukufu liridhie kufanya uchunguzi maalum wa namna zabuni zote za mradi huu mkubwa wa kimkakati zilivyotolewa ili tuwe na majibu yaliyo clear bila kutubabaisha-babaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda kuzungumzia eneo la pili kwenye mradi huu wa SGR. Pale Dar-es-Salaam reli ya SGR inapaswa kuingia bandarini na ifahamike kwamba, kwenye biashara ya uchukuzi kwa njia ya reli kinacholipa zaidi ni mizigo ni cargo, hata sio abiria. Kwa hivyo, cargo kwa kiasi kikubwa inapaswa kuchukuliwa bandarini moja kwa moja ili kwanza kuongeza efficiency ya bandari, lakini pili kule kuna mapato makubwa zaidi ukilinganisha na mapato ya abiria.

Mheshimiwa Spika, sasa miradi hii ya SGR inavyotolewa inatolewa kwa njia ya design and build. Kwamba, anayebuni ule mradi anafanya usanifu wa ule mradi ndiye ambaye atajenga mradi husika. Ilikuwaje Serikali ikaingia mkataba wa kujenga reli ambayo ilianzia pale juu, pale station, kuja mpaka Morogoro na ikafuata awamu ya pili kuja mpaka Makutupora bila kuweka link ya kuingia bandarini (port link)?

Mheshimiwa Spika, kwamba, walikuwa wanawaza nini? Mkandarasi ame-design reli halafu hajaifikisha bandarini, halafu sasa hivi wanaanza mchakato wa kutangaza kipande cha kutoka pale station kuingia bandarini na kinawasumbua kidogo kwenye design. Kwa hivyo, nilipenda kulizungumzia hilo kwa sababu linaleta utata namna ambavyo reli itakuja ku-land kule bandarini kwa sababu, bandarini ni chini na hapa station ni juu. Sasa inasumbua magari yapatika wapi? Nafasi kule ndani inasumbua itakuwaje? Sasa ilikuwaje waka-design mradi wa kuendeleza bandari na huku juu waka-design mradi wa SGR bila kuweka link ya moja kwa moja ya hivi vitu viwili, pia bila kuweka link ni namna gani watu wataingia na kutoka bandarini kwa miguu, kwa magari na kwa treni kwa njia nyingine zozote zile ambazo zinapaswa kutumika?

Mheshimiwa Spika, design ya miradi mikubwa kama hii inapaswa kufuata njia ambayo inaitwa multi-modal designing. Kwamba, unapo-design logistics za sehemu lazima ufanye consideration ya aina zote za usafiri na uchukuzi zitakazopita katika eneo hilo. Iwe kama kuna urahisi wa kufika kwa ndege, kufika kwa helicopter, kufika kwa baiskeli, kufika kwa miguu, kufika kwa trams, kufika kwa gari, magari ya abiria, magari binafsi, ni lazima uweke consideration ya mambo hayo.

Mheshimiwa Spika, sasa bandari yetu na hii SGR vilipodizainiwa (design) mradi wa kutanua bandari ulivyodizainiwa (design) na mradi wa SGR walivyo-design hawakufanya hiyo multi modal kind of designing. Kosa hili pia unaliona kwenye mradi wa BRT. BRT imekuwa designed kwa gharama kubwa sana ukilinganisha na BRT nyingine ambazo zimejengwa katika nchi mbalimbali duniani, sisi ya kwetu inaendana na nchi moja tu ya Colombia.

Mheshimiwa Spika, walipo-design wanamwaga zege ya takribani nchi 10/12. Ni zege nzito sana kiasi kwamba, wangeweza kwa hapa juu kuweka provision ya tram, yaani treni nyepesi ya kupita mijini. Hapo inapaswa kuzingatiwa kwamba, Jiji la Dar-es-Salaam kwa sensa ya juzi limekutwa na watu karibu 5.6 million. Kwa siku watu wanao-move, wanao-commute katika jiji la Dar-es-Salaam wapo kati ya Laki Nne mpaka Laki Tano.

Mheshimiwa Spika, sasa usafiri huu wa BRT ndani ya muda mfupi tu utapoteza mantiki yake, hautaweza kuwasafirisha watu kutoka eneo moja kwenda jingine kwa ufanisi ambao ulitarajiwa wakati wa designing kwa sababu, kwanza designing ilifanyika zaidi ya miaka 20 iliyopita wakati huo Jiji la Dar-es-Salaam lilikuwa lina wakazi waliokuwa wanakadiriwa 4.3 million, leo hii imeshafika hapo, kama tunaenda hivi kwa trend hii, miaka 30 ijayo population ya Dar-es-Salaam ita-double pengine tutakuwa na wakazi zaidi ya Milioni 12. Hapo maana yake ni nini, kama hukufanya multi modal designing, ukaweka provision ya barabara za juu, ukaweka provision ya trams kwenye hiyo BRT hapohapo, maana yake huo mradi ni white elephant. Na tumekopa, kwenye hii awamu ya kwanza, Dola 150,000 za Kimarekani na ambazo tunazilipa Watanzania kupitia kodi zetu. Kwa hivyo, tunatarajia wataalamu wetu wanapo¬-design hii miradi wasitutie hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hili napenda kuchangia kuhusu uendeshaji sasa wa hiyo lane ambayo sisi tumekopa, kama nchi. Juzi hapa nimeona kwenye vyombo vya habari kwamba, BRT ile lane inakodishwa kwa kampuni ya nje. Bahati mbaya sana BRT is not rocket science. Siyo sayansi ya kurusha roketi kwenda mwezini ama kwenda kwenye sayari nyingine, ni kitu rahisi sana, lane iko pale unaweka basi juu yake, Dereva analiendesha, linasimama kwenye vituo vyote, watu wanapanda na kushuka. Kwenye sehemu ya tiketi unaweka tu mfumo, ukishaweka ule mfumo immediately unaanza ku-charge. Leo hii analetwa mwekezaji wan je kuja kuendesha BRT, mwisho wa siku akipata faida anaondoka na pesa zake zote kupeleka nje ya nchi. Nini maana ya local content tunayoizungumza kila siku? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao waendeshaji wakubwa wa mabasi hapa Tanzania na mabasi yanaenda sehemu mbalimbali. Mtu anaendesha mabasi 50 hadi 100 yanatoka Dar-es-Salaam yanakwenda Bara kwenye Mikoa mbalimbali na wanaweza hizo operations. Kuna u-special gani kwenye kuendesha mabasi katika Jiji la Dar es Salaam? Hiyo ni nukta ya kwanza. Nukta ya pili, Dar es Salaam kulikuwa kuna usafiri dedicated wa UDA mpaka mwaka 1983 ambapo Serikali iliamua kuwaruhusu waendeshaji binafsi kwa sababu UDA ilionekana kushindwa kubeba mzigo wa uchukuzi katika Jiji la Dar es Salaam. Baada ya waendeshaji binafsi kuingia, mwanzo wa daladala kuingia, leo hii Dar-es-Salaam tuna mabasi takribani 7,000 yanayochukua watu kutoka sehemu moja kwenda nyingine na yanamilikiwa na takribani watu 5,000 mbalimbali.

SPIKA: Dakika moja, malizia, kengele ya pili ilishagonga.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, pamoja na ajira ambazo zinatolewa kwa wanaoagiza yale mabasi kuyaleta hapa nchini, wanaofanya ukarabati wa mabasi kwa maana ya gereji na mafundi gereji, lakini pia Mama Lishe wanaouza chakula kwa hao makondakta, ma-tanboy, pamoja na mafundi wanaofanya kazi kwenye hizo gereji, sheli mbalimbali ambazo zinapata watu wenye daladala wanaweka mafuta, zote hizi kwa ujio wa BRT maana yake hizi ajira zote zinakufa. Na hizi ajira zikifa ni takribani ajira 20,000 mpaka 30,000 hizi ajira zikifa tulitarajia basi walao yale mafao ya uwekezaji tulioufanya kwenye BRT basi yabaki hapa nchini na yasichukuliwe na mtu ambaye anatoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa nini Serikali haikuweka utaratibu wa kumlazimisha operator atakayetoka nje atakapokuja hapa nchini basi lazima awe na partnership ya lazima na kampuni ambayo leo hii inaendesha BRT? kwa nini hayakuwekwa hayo masharti? (Makofi)

SPIKA: Haya, ahsante sana.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.