Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii uliyonipa niweze kuchangia hizi taarifa za Kamati ya PAC, LAAC na PIC ambazo zimeripoti juu ya taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, kwa ajili tu ya kumbukumbu Mheshimiwa Getere alikuwa WEO, naona tumefuatana Ma- WEO hapa na mimi nilikuwa WEO wa Kata ya Ngoboko, kwa hiyo tuko hapa.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana na kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati zote hizi tatu, hoja zao walizoziwasilisha hapa Bungeni zimesheheni mambo mengi zimesheheni uchambuzi mkubwa juu ya taarifa na juu ya matumizi ya fedha za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nikianza na taarifa ya PAC labda kwa sababu nimepitia haraka. Kuna mambo makuu matatu ambayo sijayaona na nilitarajia niyaone kwenye taarifa hii. Deni la Serikali, Kamati ya PAC wanajua kwamba deni la Serikali kwa mujibu wa takwimu zilizowasilishwa kipindi kile zilionesha kwamba Serikali imekopa zaidi ya kile kilichoruhusiwa na Bunge. Kwa hiyo tulitarajia kwamba kama sehemu hii ya deni la Taifa ingewasilishwa, wangeweza kuwa wameeleza vizuri juu ya mkanganyiko huo.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, jambo ambalo nilitarajia kwamba wangeweza kulieleza vizuri kwenye taarifa hii Kamati ya PAC ni suala la malimbikizo ya kodi za makinikia shilingi trilioni 360, ambazo maelezo yanatolewa kwamba fedha hizi zimeshasamehewa zote, lakini maelezo mengine yanatolewa fedha hizi hazijasamehewa. Hili nalo nilitarajia kwenye taarifa ya PAC lingekuwa limeandikwa vizuri, lingelielekeza hili Bunge kujua hatma ya hili eneo.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu nililotegemea lielezwe vizuri ni eneo la uhamishaji wa bei ya mauziano ya bidhaa na huduma baina ya makampuni yenye mahusiano ya kimataifa, transfer enterprising ambako katika taarifa ya CAG ya mwaka 2019/2020 na mwaka 2020/2021 ilionesha kwamba katika hili eneo hatukusanyi mapato yanayostahili. Kwa hiyo nilitarajia Kamati hii ingeweza kushughulika na haya maeneo, lakini bahati mbaya sana sikuweza kuyaona kwenye taarifa yao.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo nataka kuchangia hapa ni suala la malipo yaliyofanywa na Serikali kwa Kampuni ya Symbion Power LCC. Serikali imelipa bilioni 360 kwa hii kampuni kwa maana ya dola milioni 153.43. Mkaguzi anatueleza na Kamati imetueleza kwamba makubaliano haya yalifanyika bila kujumuisha kodi wala gharama zingine. Sasa maswali ya kujiuliza ni kwa nini Serikali illipe bilioni 350 kwa Kampuni ya Symbion Power bila kuangalia Symbion Power inadaiwa kodi kiasi gani na Serikali, bila kuangalia gharama ambazo Symbion Power anahusika kuilipa Serikali na je, kulikuwa na udharura gani haraka tu baada ya makubaliano Mei, 2021 ya kulipa hizi fedha, kwa nini zililipwa haraka palepale na kama zililipwa kwa dharura namna hiyo, nani aliidhinisha fedha hizi? Kwa maana Bunge hili lilikuwa tayari limeshaidhinisha bajeti ya mwaka 2020/2021, sasa ilipofika Mei zimelipwa bilioni 350 na Serikali kwa Kampuni ya Symbion Power. Hizi fedha zilitoka wapi? Nani aliziruhusu wakati Bunge hili lilikuwa limeshapitisha bajeti tayari?

Mheshimiwa Spika, katika huo mwaka wa fedha tulikuwa na miradi mingi ya maendeleo iliyokuwa inatakiwa kutekelezwa. Serikali iliwezaje kulipa fedha hizo wakati bajeti ya Serikali ilikuwa imeshapitishwa? Hata hivyo, Mkaguzi hapa anatuambia kwamba hapa kulikuwa na usimamizi mbaya wa mkataba. Hawa waliosimamia mkataba vibaya mpaka nchi yetu wameisababishia kulipa bilioni 350 ni akina nani? Mbona hawajatajwa? Waliosababisha mpaka tukala hasara hii kwa Serikali hii ya wananchi maskini, bilioni 350 imesababishwa na mtu kusimamia mkataba mbaya, aliyeusimamia huu mkataba mbaya ni nani mpaka tukalipa shilingi bilioni 350 na kwa nini huyo mtu hatajwi? Aliusimamamia vipi huo mkataba vibaya?

Mheshimiwa Spika, Mkataba huu ulikuwa unaisha tarehe tarehe 18/09/2015, lakini ulikuja kuuhishwa na makubaliano ya tarehe 15/9/2015, siku tatu kabla ya mkataba kufika mwisho. Mkataba huu ulihuishwa kwa dharura namna hiyo kulikuwa na shida gani kwa sababu Bunge la wakati huo lilikuwa limeshaambiwa kwamba huu mkataba umefika mwisho na hautaendelea.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani shilingi za Watanzania bilioni 350 kulipwa bila kufanyika uhakiki wa kutosha. Najiuliza hizi kodi za Serikali, yaani huyu Symbion Power analipwaje kwa sababu cha kwanza kama yeye alikuwa anatudai shilingi bilioni 350, sisi tulikuwa tunamdai kodi, kodi zetu ni shilingi ngapi tunazomdai? Leo anakuja kulipwa shilingi bilioni 350, nchi hii ya maskini, kweli kabisa?

Mheshimiwa Spika, suala la Tatu, ni malimbikizo ya kodi ambazo zilikuwa zinashikiliwa na Mamlaka ya Rufani za Kodi (TRAB na TRAT) yapatayo Trilioni 360. Serikali ilituambia hapa Tarehe 24 Januari, 2020, Serikali ilifuta madai haya, kwa maana Serikali tukawa hatudai tena. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, taarifa ya CAG ya Mwaka 2019/2020 inatambua kuwa Serikali inadai Shilingi Trilioni 360, ilipofikia taarifa ya CAG ya mwaka 2020/2021 CAG anasema: ‘‘inaonesha kuwa kesi za makinikia zipatazo 45 zenye thamani ya Shilingi Triloni 5.595 ziliamuliwa na Mamlaka za Rufani za Kodi, TRAB na TRAT’’. Kodi hizo zilipoamuliwa, Serikali ikaagizwa kufafanya majadiliano na makampuni hayo yaliyotakiwa kulipa hizo kodi. Kwa hiyo, inaonekana kwamba katika Mahakama hizi, ziliamua kati ya Trilioni 360 ziliona nchi yetu inastahili kulipwa, kwa maana ya Mahakama Trilioni 5.595.

Mheshimiwa Spika, Serikali ikafanya majadiliano na makampuni hayo yanayotakiwa kulipa ili wakubaliane namna ya kulipa. Kampuni la kwanza ambalo linatajwa kwenye Taarifa ya CAG ni Kampuni la North Mara Gold Mine; Kampuni ya Pili ni Pangea Mineral Limited; Tatu ni Bulyanhulu Gold Mine na Nne ni ABG Exploration. Kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya Mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, nikafuatilia ripoti za viongozi waliokuwepo kama waliweza kulisamehe hili deni. Nikafuatilia taarifa ya vikao vyote ambavyo Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliwahi kukaa na Barrick juu ya jambo hili. Nikafuatilia taarifa za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kama aliwahi kuzungumza jambo lolote kuhusiana na kusamehewa kwa kodi hizi.

Mheshimiwa Spika, hotuba zote za Viongozi hawa nimezisikiliza, hakuna mahali popote ambako wamesema fedha hizi zimefutwa. Mahakama iliagiza kampuni ya madini pamoja na Serikali yajadiliane namna ya kulipa Trilioni 5.595. Aliyeenda kufuta kodi za Watanzania hizo ni nani? Serikali lazima ituambie ukweli juu wa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu suala hili lipo kwenye taarifa ta CAG ukurasa wa 60 mpaka 63, Mheshimiwa CAG alete taarifa juu ya jambo hili ili Watanzania wajue hitimisho na ukweli wake juu ya fedha zao. Nchi hii maskini haiwezi kuingia kwenye makubaliano ya kwenda kusamehe kodi kubwa zote hizo, halafu tukaendelea kwenda kutoza kodi kwa wananchi, kodi ndogondogo tunaendela kutoza, halafu wafanyabiashara wakubwa kama hao wanasamehewa na nani? Kwa ajili ya nini? Tulishaelezwa kule mwanzo hizi kodi zilipatikanaje! Watu walikuwa wanatengeneza mahesabu ya aina mbili, mahesabu ya kulipia kodi na mengine ya kukwepea kodi na kuonyesha uhalisia kule kwao wanaporipoti, tuliona ukweli huo! Sasa aliyeenda kusamehe alisema nini? Kwamba mlifanya vizuri tu kutupunja, tumewasemehe. Alienda kusamehe akisema nini katika nchi maskini kama hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umesema vizuri sana leo, kwamba sisi tunaisimamia Serikali na Serikali leo itoe kauli juu jambo hili, tulimalize. CAG akachukue documents zote, kama kweli Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alisamehe hili deni, kama kweli Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alisamehe hili deni. Tuletewe hapa ili tuweze kufanya maamuzi zaidi kama Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la Nne ni kuhusu TRA, Kamati hapa imetueleza, inasema kwenye eneo la malimbikizo ya kodi yasiyo na kesi. Amesema vizuri hapa Mtendaji wa Kata mwenzangu ameeleza vizuri sana, kwamba hivi tutasemaje sasa, tuna Taasisi yetu inayohusika na ukusanyaji wa mapato ya Serikali, inafika mahali kwa mwaka mmoja kodi ambayo haijakusanywa na hazina kesi Mahakama ni Trilioni 3.87. Katika Taasisi inayokusanya hata Trilioni 20 haifikishi. Trilioni 3.87 hazijakusanywa na hazina Mahakamani, sasa hii Taasisi yetu inachangamoto gani? Wanaeleza kwamba malimbikizo haya yameongezeka kwa asilimia 95 ya madai ya kodi.

Mheshimiwa Spika, hii taasisi yetu ina shida gani, kwa sababu hata tungeongea namna gani, hatuwezi kuyaleta maendeleo ya Watanzania kama hii taasisi haiwezi ikafanya kazi sawasawa. Trilioni 3.87, hizi ni zile kodi ambazo hazina kesi Mahakamani, kuna kodi ambazo zina kesi Mahakamani, ukizijumlisha zote hizo karibia asilimia 30 ya mapato hatuyakusanyi! Sasa kama hatuyakusanyi, tuta-survive namna gani? Maendeleo tuliyoyaahidi na kwenye Ilani ya Uchaguzi na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, tutaujenga na tutalipa na nini? Madeni tunayokopa leo tutayalipa na nini? Kama hatuwezi kukusanya kodi, tukaweza kulipa madeni, tukaweza kujenga, tukaweza kuhudumia Serikali.

Mheshimiwa Spika, ifike mahali sasa tuwe tunaambiwa ukweli, eneo hili la Taasisi yetu ya TRA kama inalo tatizo ambalo lenyewe lipo juu ya uwezo wake kwa nini tusiambiwe kama Bunge tuamue? Kuna mambo mengine tu wanalalamika, mara watumishi wachache, hivi kweli kabisa anayepanga watumishi unaweza ukaamua Taasisi inayolipa watu mishahara yote na yenyewe ikawa na upungufu wa watumishi kabisa kabisa ukawa na nia njema na Watanzania hawa?

Mheshimiwa Spika, TRA ikose fedha ambaye analipa mishahara ya watu wote, TRA anapeleka fedha za maendeleo kote, ambaye anatulipia Deni la Taifa, huyo naye awe na upungufu wa watumishi? Kama kuna matatizo yaliyojificha kwa TRA, kama ni udhaifu wa TRA uwekwe wazi, kama kuna udhaifu wa TRA ambao upo juu ya uwezo wao, Bunge hili linahitaji kufanya maamuzi, tufanye maamuzi leo, tuiwezeshe Taasisi hii na tuchukue hatua kwa wale ambao wanaturudisha nyuma.

Mheshimiwa Spika, leo tunazungumza malimbikizo ya kodi yasiyokuwa na kesi yamefikia trilioni 7.54 jumla…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mpina, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Simbachawene.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba Mheshimiwa Mbunge anayechangia Mheshimiwa Mpina, ameshalizungumza hili jambo hili Bungeni mara kadhaa. Pengine Mheshimiwa Mpina ili aweze kutenda haki na kwa sababu yeye ni Mwanataaluma wa eneo hili ni vizuri akaelezea vizuri kinachotokea katika masuala ya rufaa za kodi. Kunapokuwa na mgogoro, kodi ikawa inabishaniwa kati ya Mlipa Kodi na TRA kile kiasi ambacho hakibishaniwi mfanyabiashara anayetakiwa kulipa huwa kinalipwa na Serikali inachukuwa kiasi chake. Kinachobaki ambacho kina-dispute kinaingia kwenye mgogoro, kwa hiyo ni kwa sababu ni maisha ya shughuli mbalimbali zinazoendelea na wafanyabiashara, kuna uwekezaji, kuna mambo mbalimbali, huendelea kwa sababu ni suala la mgogoro na ni suala la haki.

Mheshimiwa Spika, katika kundi la hao wanaodaiwa wengine waloshafunga makampuni, wameshindwa kufanya biashara, hapa mnasema tuvutie wawekezaji, hapa mnasema tuhakikishe kwamba wawekezaji wanapata mazingira mazuri, ni katika mazingira hayo ambayo yamepelekea hata baadhi ya wawekezaji kuondoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali makini kama hii ambayo tunatafuta pesa kila siku, hatuwezi tukaacha kudai kodi, hatuwezi tukaacha kudai mapato ambayo Serikali inataka kuyapata, lakini sasa tunapokutana na mgogoro ambao kile kiasi kinachobishaniwa kinabaki katika mgogoro lakini kile cha msingi kinakuwa kimelipwa. Kwa hiyo, hakuna hakuna fedha iliyoachwa makusudi ila kuna kesi. Kesi ni suala la haki jamani, hauwezi kusema leo hii kwa sababu ni Serikali mmeacha. Isionekane hivyo, kwa hiyo ielezwe vizuri. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mpina unaipokea taarifa hiyo?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, taarifa yake siipokei na sababu ya kutokuipokea ingekuwa haya maelezo yake yanakubalika angeyapeleka kwa CAG, CAG angetuandikia hapa Kamati inasema malimbikizo haya yanatokana na kutokushughulikiwa ipasavyo kwa madeni ya kodi mathalani mwaka 2020/2021. Hawa Mawaziri wetu wasome taarifa, wasiwe wanapoteza muda wetu hapa tunapochangia hapa Bungeni. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naendelea kusisitiza malimbikizo ya Trilioni 7.54 na hizi hazina kesi Mahakamani, TRA walitakiwa kukusanya, nikaeleza kwamba kwa mwaka mmoja wamefeli kukusanya malimbikizo ya Trilioni 3.87, mwaka mmoja wa 2020/2021. Kama tutaenda namna hiyo, utakusanya kodi ya nani, kama tutaenda hivyo, tutaijenga nchi yetu kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba mambo makubwa kama haya yakiletwa hapa Bungeni, yakielezwa kwa ufasaha, Bunge lako litaelewa na litajua hata lichukue hatua gani.

Mheshimiwa Spika, kama muda unaniruhusu nimalizie suala la mwisho. Suala la mwisho ni suala la utoaji mikopo asilimia 10 ya akina mama, vijana na Wenye Ulemavu. Wenzangu hapa wamechangia na bahati nzuri Kamati ya LAAC imelizungumza suala hili, ninachotaka kushauri ni kwamba sasa hivi tunavyoenda hili eneo ni kubwa, Taasisi inayosimimia ambayo siku hizi inaitwa Division ya Maendeleo ya Jamii, haina uwezo wa kulisimamia jambo hili. Idara Zetu za Maendeleo ya Jamii hazina watu competent wa mambo ya fedha, hazina watu competent wa kusimamia mikopo, unaenda kumchukua Afisa wa Maendeleo ya Jamii asambaze mkopo wa Bilioni Mbili, asambaze mkopo wa Bilioni Kumi, asisimamie, azikusanye, azilitele, akaunde vikundi na akopeshe tena.

Mheshimiwa Spika, jambo hili tulianzisha vizuri lakini kadri tunavyoenda zipo halmashauri mapato yao kwa mwaka ya own source yanafikia hata Bilioni Ishirini. Kwa maana hiyo, ukichukua asilimia kumi yake kwa mwaka wanapata bilioni Mbili, ukichukua kwa miaka Saba tu, wanafikia kile kimo cha kuanzisha benki cha Bilioni 15. Sasa kama ndivyo ilivyo, kwa nini tusianzishe utaratibu wa hizi fedha zikakusanywa, tukaingia na benki ambazo zinapatikana maeneo ya karibu, NMB na CRDB, tukaweka masharti ambayo hayaathiri malengo na maksudi yaliyowekwa na Serikali. Mikopo hii ikaanza kupitia kwenye Benki, lakini mchakato wake wa awali utakanywa na hii Idara yetu ya Maendeleo ya Jamii na fedha hizo zikaanza kutolewa kwenye Benki, ambako kuna competent personnel waliosomea mambo ya utoaji wa mikopo, kule kuna watu wanaoweza kuifuatilia mikopo hii.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunashuhudia changamoto nyingi, sehemu zingine upendeleo mkubwa, wanapewa kundi la watu hela yote ya Halmashauri inachukuliwa na watu wawili watatu inaisha, sehemu nyingine fedha hawakusanyi, unakuta asilimia 20 tu ya marejesho leo miaka mitatu, miaka mingapi. Kwa hiyo, kwa changamoto hizi za upendeleo na uwezo wa kusimamia kodi zenyewe na idara zetu na upungufu wa watumishi tulionao, hili eneo hatuna uwezo wa kulisimamia vizuri. Ningeshauri tuende kwenye MOU na benki zinazoweza kuhudumia suala hili, najua linaweza kufanyika vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, zipo taasisi kama PASS ziliweza ku-guarantee watu wetu kwenye kilimo, wanafunzi vijana na kadhalika zina-guarantee, sasa Serikali na yenyewe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)