Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya Afya. Kipekee sana nimshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kweli amekuwa akitekeleza na kupeleka fedha nyingi sana kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo, namshukuru yey pamoja na wasaidizi wake wote.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita zaidi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kama nilivyotangulia kusema, Mheshimiwa Rais pamoja na wasaidizi wake wamepeleka fedha nyingi kwenda kutekeleza miradi ya hospitali, vituo vya afya, zahanati, kujenga shule na mambo mengi yanafanyika katika maeneo yetu, nasi sote ni mashahidi wa yale ambayo yanatekelezwa katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, nini matarajio kama nchi? Matarajio ni kuona kwamba miradi ile inatekelezwa kikamilifu na inakuwa na thamani ya fedha iliyopelekwa katika hayo maeneo. Kwa bahati mbaya sana katika baadhi ya maeneo, hasa kwenye Halmashauri za pembezoni, ili miradi ile iende ikakamilike vizuri, lazima kuwe na rasilimali watu wa kutosha. Ila kwa bahati mbaya Halimshauri zetu za pembezoni kuna upungudu mkubwa sana wa rasilimali watu kiasi ambacho utekelezaji wa miradi ile unakuwa chini ya kiwango. Ukienda unakosa watu wa manunuzi, unakosa ma-engineer, unakosa wahasibu na mambo kadha wa kadha. Kwa hiyo, matokeo yake miradi mingi inatekelezwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Spika, labda nikupe mfano wa uchache au upungufu wa watumishi katika baadhi ya Halmashauri. Ukienda kwenye ripoti ya CAG, ziko Halimashauri nyingi ambazo zimebainisha upungufu wa watumishi ikiwemo Kasulu DC, kuna uhaba wa watumishi 163 sawa na 52% tu. Ukienda Nanyamba Mji kuna upungufu wa watumishi 932; ukienda Halmashauri ya Kilwa, walimu peke yake, kuna upungufu wa walimu 735; Ukienda Newala DC kuna upungufu wa watumishi 1,087 waliopo ni 1,088 tu; ukienda kwenye maeneo mengi kwenye kata hakuna Maafisa Maendeleo ya Jamii, sehemu ambayo tunapeleka fedha nyingi sana zile za mikopo ya 10% lakini hakuna wasimamizi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika baadhi ya Halmashauri hakuna Wakaguzi wa Ndani, hawapo. Pia Maafisa Manunuzi kwenye Halmashauri zetu nalo ni changamoto, wengi waliopo ni wale walioazimwa na Halmashauri na wanakosa sifa. Sasa matokeo yake ni kwamba miradi mingi, kwa sababu hawa watumishi ambao tunawakosa ndio ambao wangtakiwa kusimamia miradi hiyo kwa ukamilifu, miradi imekosa thamani halisi ya fedha kama vile ambavyo tulikuwa tunatarajia.

Mheshimiwa Spika, rasilimali watu ndiyo uti wa mgongo kwenye utendaji wa hizi Halmashauri. Kwa mfano, umepeleka fedha hiyo asilimia 10 ili iende kwenye hayo makundi ya akina mama, vijana, pamoja na watu wenye ulemavu, lakini hakuna mfuatiliaji kule. Zile fedha zinaenda kuzama, kwa sababu zitapelekwa, lakini nani wa kuwaelimisha? Hayupo. Nani atasimamia? Hayupo. Kwa hiyo unakuta fedha nyingi zinapotea.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali, kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 ni Shilingi bilioni 47.1 hazijarejeshwa. Hizi ni fedha nyingi ambazo zingefanya kazi nyingi sana katika Halmashauri zetu. Ukirudi miaka mitano nyuma, ni zaidi ya Shilingi bilioni 100 zimeshindwa kurejeshwa, zimezama.

Mheshimiwa Spika, matokeo yake ni kwamba Halmashauri na wale ambao tuliwatarajia waende tukawainue kiuchumi wanakosa kuinuliwa kiuchumi kwa sababu hizo fedha ambazo tulitarajia zirudi zikawasaidie watu wengine hakuna mtu wa kuelimisha na kutoa elimu ya kutosha pamoja na usimamizi wa hayo makusanyo kule kwenye maeneo ya kata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye suala la manunuzi, kama ambavyo Mjumbe ambaye ametangulia kusema, fedha nyingi katika Halmashauri zetu zinaenda upabde wa manunuzi, lakini hakuna watu wa manunuzi. Kwa hiyo, unakuta Mkurugenzi anakwenda kumwazima; natolea tu mfano, mwalimu, mtu ambaye hana sifa ya kutosha kwenye eneo hilo, ndiye anaenda kusimamia manunuzi. Ukienda kwenye ripoti ya CAG, kiasi kikubwa cha fedha kimepotea kwa sababu ya kukosa watu wenye sifa wa kusimamia manunuzi ya Umma. Wanafanya manunuzi lakini hayafuati taratibu na kanuni ambazo zimeandaliwa na PPRA.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kukosekana kwa ma-engineer katika Halmashauri zetu; tulienda kwenye Halimashauri mojawapo kwenye mkoa huu ambao tupo, tulimkuta mtu ambaye alikuwa anasimamia ujenzi wa bwalo pamoja na bweni, alikuwa ni Mwalimu. Kwanini alikuwa anasimamia Mwalimu? Amewekwa pale kwa sababu ya ukosefu wa engineer pale Halmashauri. Kwa hiyo, kawekwa yeye. Tulikuta miradi ile kwa kweli ilikuwa inasikitisha sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali kwa sababu fedha hizi zinatokana na kodi za wananchi, lakini lengo ni kutoa huduma kwa wananchi pale ambapo miradi itakamilika vizuri. Naiomb Serikali basi, ijitahidi kuajiri watumishi ambao wataenda ku-cover gap lililopo kwa sasa ili miradi iwe na thamani ya fedha ambazo zinapelekwa kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine, nilizungumzia suala la upungufu wa walimu katika baadhi ya maeneo, vile vile, ukosefu wa watumishi katika vituo vya kutolea huduma za afya nao ni mkubwa. Naiomba Serikali ifike mahali sasa tuajiri watumishi ambao wana utashi wa kuishi kwenye maeneo husika au wale ambao wanatoka kwenye maeneo yao. Kwa sababu ipo changamoto kubwa, mtumishi anapoenda kwenye eneo ambalo jiografia yake inakinzana na yeye, anakaa kwa muda mfupi, anataka kutoka. Nafahamu kwamba Tanzania ni yetu sote, kila mmoja anatakiwa kuishi popote, lakini ipo hiyo changamoto sana ambayo tunai-experience site. Mtu anaenda kuripoti na anataka arudi, matokeo yake upungufu hauishi kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuweke muda maalum kwa mtumishi kuhama, yule ambaye amepata ajira. Muda ambao haupungui miaka mitatu ili angalau tu-retain wale ambao wapo. Otherwise haya maeneo ya pembezoni ya Mamlaka za Serikali za Mitaa yataendelea kubakia bila kuwa na watumishi na hali inazidi kuwa mbaya kwa sababu lengo ni watumishi wawepo ili huduma zikaweze kutolewa ipasavyo. Watumishi wanapokosekana, huduma pia zinakosekana.

Mheshimiwa Spika, lingine naomba pia Serikali ibaini upungufu kwa kila Halmashauri za pembezoni, ili wakati wa kutoa ajira, basi kipaumbele kiwe ni yale maeneno ambayo yana upungufu mkubwa. Kwa sababu haiwezekani kila siku baadhi ya maeneo watumishi wanakuwa wachache. Imekuwa kama ni wimbo, kuna maeneo yana watumishi wengi na mengine yana watumishi wachache. Sasa hao ambao ni wachache, utoaji wa huduma inawawia pia vigumu. Kwa hiyo, tufanye Sensa ya makusudi, tubaini hali ilivyo ili linapokuja suala la ajira, basi watumishi wapelekwe au tutoe kipaumbele katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limejitokeza kwenye ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2020/2021, ni tatizo la fedha kutopelekwa benki zinazokusanywa kwa mfumo wa POS. Hii ni changamoto kubwa na imejitokeza katika maeneo mengi. Kwa mwaka 2020/2021 peke yake ni Shilingi bilioni 17 hazikupelekwa benki. Tafsiri yake rahisi tu ni kwamba hizo fedha zimeingia kwenye mifuko ya watu, lakini zingekuwa zimewekwa benki zingefanya mambo ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, sasa tunakwamisha kwa sababu kwenye bajeti Kuu ya Taifa inabajetiwa pia na fedha zinazotokana na makusanyo kutoka Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Kwa hiyo, unakuta bajeti kuu ya Taifa haitimii kwa sababu kuna fedha huku nyuma ambazo zimewekwa kwenye mifuko ya watu ambao siyo waaminifu. Naiomba Wizara ambayo inasimamia TAMISEMI kuweka mfumo ambao ni madhubuti utakaodhibiti hili suala za fedha kutopelekwa benki.

Mheshimiwa Spika, fedha hizi siyo za leo kwa sababu huu ni mwaka wa pili, kw sababu ni za mwaka 2020/2021, Shilingi bilioni 17 hazijaenda benki hadi leo. Wamechukuliwa hatua gani ambao wamehusika? Mpaka sasa baadhi ya maeneo unakuta bado. Kesi nyingi ziko TAKUKURU, wengine wamepelewa Polisi, lakini kile ambacho tulikuwa tunataraji, kwa sababu lengo letu lilikuwa tupate zile fedha zikatoe huduma kwa wananchi. Kwa hiyo, inachelewesha pia utoaji huduma kwa wananchi kwa sababu fedha zimeingia kwenye mifiuko ambayo siyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba TAMISEMI, ule mfumo wa kielektroniki wa TAUSI uanze kufanya kazi ili tuweze ku-monitor haya mambo mengine amabyo yanaweza pia kurekebishika.

Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine ambalo Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali amelibainisha kwenye Hesabu ya 2020/2021, nalo ni suala la vitendea kazi kwa watumishi. Nimeongea hapa kuhusu Maafisa Maendeleo ya Jamii, lakini pia tuna ma-engineer wanaosimamia miradi, tuna wahasibu, wakusanya mapato, wanahitaji vitendea kazi ili waweze kufika kwenye maeneo ambako wanaweza kutoa hizo huduma au kukusanya mapato. Halmashauri nyingi hazina vitendea kazi kwa watu hao. Unakuta internal auditor yupo pale, anatakiwa kumkagua Mkurugenzi, Mkurugenzi hampi usafiri; kwa sababu akimpa usafiri, maana yake anaenda kumtafutia yeye changamoto. Kwa hiyo, hapewi usafiri, kiasi kwamba sasa unakuta kazi ya internal auditor inakuwa ngumu sana, namna gani atafika akakague miradi ili aje abainishe yaliyopo huko site? Anashindwa kwa sababu hana vitendea kazi.

Mheshimiwa Spika, naiomba Wizara tuangalie Halmashauri, tuwawezeshe waweze kufika kwenye maeneo. Engineer yupo, anatakiwa akakague miradi, na sasa hivi miradi ipo mingi kwenye kata zetu, lakini engineer yupo Halmashauri, hana usafiri wa kumfikisha huko site. Matokeo yake sasa, kwa sababu yeye hawezi kufika kwa wakati, basi ana-delegate, anawaambia walioko site kama ni watu wa Afya, kama ni watu wa Elimu au nani, wasimamie hiyo miradi wao, lakini wao tukumbuke kwamba hawana ujuzi wa majukumu ambayo wanapewa. Matokeo yake ni miradi inazidi kuharibika kwa kukosa vitendea kazi vya kuwafikisha maeneo mbalimbali ya kusimamia miradi kule site. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine niseme kidogo ni suala la wahasibu. Nilitangulia kusema kwamba wahasibu ni wachache, lakini unakuta maeneo mengine wahasibu hawa wamepitwa na wakati, kwa maana ya kwamba mifumo inabadilika kila siku ya ufungaji wa hesabu za mwaka, lakini wahasibu hawa hawana mafunzo ya namna ya kufunga hesabu hizo za mwaka. Matokeo yake inapofika ufungaji wa hesabu za mwaka wanapita, wanahaha kwenye maeneo mbalimbali kutafuta watu wa kuwafungia hesabu zao. Ni suala ambalo linapoteza fedha nyingi za Halmashauri, kwa sababu wangekaa kwenye vituo vyao wakafunga wenyewe hesabu zao ingepunguza hizo gharama za kupita wanazunguka kutafuta watu waweze kuwafungia hesabu zao za mwaka. Kwa hiyo, hili ni tatizo ambalo lazima Wizara zinazosimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa walione, waone namna nzuri ambayo watatoa mafunzo kwa wahasibu ili waendane na utaratibu na mfumo mpya unaotumika sasa wa ufungaji za hesabu hizi za Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, wengine ambao wanafanya wao wenyewe, wanasema poteleambali tunafanya, unakuta hesabu zao ni mbaya, hata CAG anashindwa kuisoma hiyo hesabu ya Halmashauri husika na matokeo yake wanaipa hati ambayo siyo yenyewe, lakini ni kwa sababu tu ya upungufu wa ujuzi kwa wahasibu ambao wapo katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii. Ahsante sana.