Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, hali ya kiuchumi ya familia nyingi za kitanzania zinafanana sana na kesi ya mtoto aliyetolewa mfano na Mheshimiwa mtoa hoja. Pia kesi ya mtoto ya mtoa hoja inafanana sana na kesi za watoto wengi ambao wapo katika majimbo yetu. Hii imenifanya nisimame hapa kwa sababu nimejitazama mimi mwenyewe ninatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni mtoto wa Katibu wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi enzi hizo, na ninakumbuka kipindi hicho wakati mimi nafaulu vizuri sana Form Six masomo yangu ya PCB, mama yangu mzazi ndio alikuwa mlezi wangu pekee na alikuwa hajalipwa mishahara yake ya karibu miaka miwili hivi.

Mheshimiwa Spika, nikitafakari hali ya mtoto ambaye amefaulu kwa Division One, kama ambavyo mimi nilikuwa nimefaulu kwa Division One kipindi namaliza na mzazi wangu hana uwezo; na nikitazama mazingira ya watoto wengi wa kitanzania; naona kuna haja ya suala hili kutazamwa kwa umakini zaidi kuliko linavyotazamwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo? Tunaelewa Wizara ya Elimu wanafanya kitu kinaitwa means tests ili kuwapata watoto ambao watapata sifa za kupewa mkopo na Serikali. Tunafahamu kama Taifa, tunapata changamoto ya kuongezeka kwa wahitaji wa mkopo kutoka kwenye Bodi ya Mikopo kila mwaka, kwani kila mwaka wanaongezeka.

Mheshimiwa Spika, sasa hatutarajii siku moja population itashuka kwa sababu ukitazama namba zilizotangazwa jana za sensa utaona pengine miaka 30 ijayo idadi ya jana itakuwa ime-double. Pengine tukawa na watu zaidi ya milioni 120. Sasa nini Serikali ifanye kama suluhisho la kudumu? Ni lazima ufanyike mchakato wa wazi wa njia za kupata wahitaji na wanufaika wa mfuko huu wa Bodi ya Mikopo, pia ipatikane namna ya kuwasaidia hawa ambao wanafikisha zile sifa ambazo zinahitajika. Vinginevyo, tutatengeneza bomu kubwa sana la watoto pamoja na wazazi wao ambao watakuwa wanailaumu Serikali maisha yao yote.

Mheshimiwa Spika, you can imagine mtoto ambaye amefaulu kwa division one kama ambaye ametolewa mfano na mtoa hoja, akikosa fursa ya kwenda kusoma Udaktari kama ambavyo alikuwa ametamani, you can imagine hiyo scenario crisis ambayo inajitokeza kwake na familia yake, lakini namna ambavyo watoto wengi watakufa moyo kutokana na hiyo. Pia yatatokea maswali ambayo tutapaswa kuyahoji kwamba je, tunatenda haki kwa watoto wa Taifa letu? Kwa sababu elimu ni haki ambayo inatolewa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pia kupata mkopo ni haki ya watoto ambao wamefaulu na wanakidhi vigezo. Tusipotoa haki hiyo kama Taifa, maana yake tunatengeneza kundi la watu ambao wataacha kuamini katika Katiba, wataacha kuamini katika Sheria, wataacha kuamini katika Serikali, wataacha kuamini katika Bunge, wataacha kuamini kwenye kitu chochote kile ambacho kiko morally right. Kwa sababu kama nimefanya kila kitu vizuri, nimefanya kila kitu sawa, nisipopata haki, kuna haja gani ya kuwa mtu mwema katika dunia hii? Ndiyo maswali ambayo watoto wengi na wazazi wengi watajiuliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe ni msomi wa Sheria, anaisema vizuri sana Mwanafalsafa Tom Tyler kwenye kitabu chake cha “Why People Obey the Law” ambacho alikiandika mwaka 1990, kwamba uhalali wa maamuzi yanayotolewa na viongozi, uhalali wa sheria zinazotungwa na Mabunge ya Mataifa utapatikana tu endapo sheria hizo, endapo Serikali zao, endapo Mabunge yao yatatoa haki kwa wananchi na wananchi wataona haki imetolewa na wata-enjoy matunda ya haki ambayo inatolewa na sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ili mifumo yetu ya Utawala Bora, ili Katiba yetu, sheria zetu ziendelee kuaminiwa, kuthaminiwa na kutumainiwa, ni lazima tutoe haki kwa watu wa Taifa letu. Haki ya msingi kabisa ambayo mwanadamu yoyote anapaswa kuipata, basi ni haki ya kupata elimu. Kuna haja gani ya kuzaa mtoto ukamlea vizuri, ukampa miongozo, akaenda shule, akasoma vizuri, na akafaulu, akakosa fursa ya kwenda kusoma masomo ya Chuo Kikuu kwa sababu nchi yake imeshindwa kumwekea mfumo mzuri wa namna ya kupata msaada wa kulipiwa ada na gharama nyingine za masomo yake?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pamoja na kwamba tunaelewa Serikali ina mzigo mzito wa kukidhi gharama za kusomesha watoto wa Taifa letu, ni lazima tuweke mfumo kwanza wa wazi; pili, unaokubalika; tatu, unaotekelezeka, wa kuwafikia wahitaji na wanufaika wote wa mikopo ya elimu ya kati na hata elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika, ilivyo sasa, mfumo tulionao hautoi haki kwa watu wengi na hivyo ninaunga mkono hoja ya mtoa hoja kwamba jambo hili liangaliwe upya na mwisho wa siku tupate suluhisho la kudumu, ahsante. (Makofi)