Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuhitimisha hoja yangu na nipende kusema kwamba nawashukuru sana Wabunge kwa michango mbalimbali mizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata wachangiaji wa kuzungumza kumi na kwasababu siyo wengi naomba niwataje; Mheshimiwa Edwin Swalle, Mheshimiwa Simai Sadiki, Mheshimiwa Amour Mbarouk, Mheshimiwa Kunti Majala, Mheshimiwa Dkt. Leonard Chamuriho, Mheshimiwa Judith Kapinga, Mheshimiwa Francis Mtinga, Mheshimiwa Luhaga Mpina na Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mheshimishimiwa Feleshi na Mheshimiwa Waziri Jenista Mhagama.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru sana kwa michango yao mizuri waliyoitoa ambayo kwa kweli imekuwa kwanza wanaunga mkono hoja yetu, lakini wanaboresha pale ambapo panastahili na panawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kazi za kutunga sheria ni ya Bunge, sheria zote, sheria mama, sheria ndogo zote ni ya Bunge, lakini Bunge limekasimu kazi hii kwa mamlaka mbalimbali kwa sababu ni nyingi sana, inahusu sheria zenyewe, sheria ndogo, sheria kubwa zenyewe, sheria mama. Amesema Mheshimiwa Mpina zile zote zimo waraka, matangazo, amri, kanuni ile nyingine proclamation zimo kwenye sheria ndogo, zote zimo zinahusu humu ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Bunge haliwezi kutunga sheria zote hizi peke yake likamaliza, lazima likasimu kwenye mamlaka mbalimbali Halmashauri, Wizara mbalimbali, idara mbalimbali ili kazi hii iweze kutendeka vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa lengo la sheria ndogo hizi zote nilizozitaja zikiwemo na waraka na nyingine hizo ni kusaidia kutekeleza sheria mama, kuzifafanua vizuri zaidi ili zieleweke vizuri, kurahisisha utekelezaji wa sheria mama, si kuzikwamisha au kuweka masharti ambayo yanaleta ukinzani kwenye sheria mama au yanakwamisha ufanisi na maslahi ya Watanzania na urahisi wa Maisha, ni kurahisisha sheria zenyewe ziweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunawaomba watungaji wale wa sheria ndogo wawe makini, kule kwenye mamlaka kwenye halmashauri kwenye wizara kuna wanasheria kule wanaweza kufanya kazi hii kwa umakini na waondoe hizi kero ambazo tumezibainisha hapa na Wabunge wamechangia kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano kama niliousema hapa sheria mama inasema kwenye kosa fulani adhabu ni shilingi isiyozidi shilingi 300,000 au kifungo kisichozidi miezi 15; sheria ndogo inakuja inasema kwenye kosa hilo hilo adhabu isiyopungua shilingi milioni tatu au kifungo kisichopungua miaka mitano. Sasa unashangaa hii sheria ndogo ya namna gani inakinzana na sheria mama na inaongeza adhabu kuliko ilivyosema sheria mama, hii siyo sawa sawa huu ni ukiukwaji ambao upo dhahiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Kamati inachofanya sisi tunachambua hizi na kubainisha mapungufu haya na makosa haya ambayo yamo na kuyarekebisha na kwamba tunawaambia wale warekebishe. Tatizo ni kwamba kama nilivyosema hapo mwanzoni tunawapelekea maelekezo hawaleti, ndiyo maana tumesema hapa angalau ikifika Novemba na Desemba tarehe 1 wawe wameleta. Sasa inavyoonesha kwamba itabidi tuanze kwenda kule kwenye hizo Wizara kuchunguza kwa nini hamjaleta, hili tuliwaelekeza hamjaleta mpaka leo watupe majibu; kama yanaridhisha kama hayaridhishi sisi tutawaambia maana yake inachafua taswira ya Bunge. Mwananchi akiumia kule analaumu Bunge halaumu ile mamlaka kule anasema Bunge hili namna gani imetunga sheria mbovu ambayo haitekelezeki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumemsikia Mheshimiwa Kapinga hapa anaongelea Bolt na Uber zimefunga kabisa biashara zao ambayo ilikuwa ni huduma nzuri, inagharama nafuu kwa mwananchi, unapiga simu dakika mbili umeshapata huduma, sasa hiyo imesimama; hii siyo kuboresha maslahi ya Watanzania au ufanisi wa maisha kuwa mazuri ni kukwamisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria ndogo hazina lengo hilo, wale wanaotunga hizo sheria wajitahidi kuzingatia sheria mama, kuwa na utu, kupenda maendeleo na si kukwamisha maendeleo. Wajitahidi kufanya hiyo kazi kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa maelekezo waliyoyatoa hapa kwanza wamekubali kwamba kuna dosari ndogo ndogo, nawashukuru sana kwa kazi waliyoisema kwamba wataenda kuifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme pia mwishoni kwa kumalizia kwamba dosari hizi si nyingi sana, zimepungua sana kadri tunavyokwenda mbele, mwanzoni zilikuwa nyingi sana sasa zimepungua na nitumie nafasi hii kuwapongeza wale ambao wanatunga sheria nzuri kwenye mamlaka mbalimbali huko kwenye halmashauri na sehemu nyingine wanajitahidi sana kufanyakazi nzuri ambayo ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.