Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi kuweza kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji katika ripoti hii ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie fursa hii kuwapongeza sana Mawaziri wote pamoja na Wizara zao na Serikali kwa ujumla kwa kuwa na nia safi kabisa ya kutunga sheria kulingana na mazingira na mabadiliko ya nchi na dunia kwa ujumla yanayoendelea kutokea kila siku. Ni ukweli usiopingika Tanzania ni kama sehemu moja wapo ya dunia ni wazi hatuwezi kuishi bila kufuata sheria na kanuni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hata kama Bunge hili tutaazimia kwamba tuondoe sheria zote za nchi hii, bado tutaendelea kuishi katika zile scope za sheria za kimaumbile, kwa sababu binadamu toka azaliwe anaongozwa na sheria. Kwa maana hiyo hii inaonesha wazi umuhimu wa sheria katika maisha ya binadamu ni sawasawa na umuhimu wa maji hatuna namna ya kuweza kuziepuka sheria na kanuni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la msingi kabisa la kuzingatia katika utunzi mzima wa sheria tuelewe ya kwamba sheria siku zote ndizo ambazo zinakuja kuonesha ule uhalisia wa maisha ya wananchi yaliyowazunguka, kwa hiyo, sheria zinatakiwa na sheria ndizo zitakazokuwa zinaongoza maisha na matendo halisi ya nchi na raia wanaoishi katika sehemu hiyo, lakini suala la kujiuliza; je, ni kwa namna gani sheria hizi zinaakisi na zinafikia malengo halisi ya utunzi wa sheria zilizokuwa bora?

Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli sisi kama Kamati tumeweza kupitia sheria nyingi na kusema kweli niipongeze Serikali kwa kazi wanazoendelea kuzifanya, lakini changamoto haziwezi zikakosekana, utaona kwamba mantiki walizokuwa nazo Wizara na Mawaziri wetu katika utunzi wa hizi kanuni na sheria ni nzuri na unaweza kuikuta kanuni ile kwa asilimia 100 inawezekana inakidhi matakwa na mahitaji ya jamii husika, lakini ikakosa ubora kutokana na kipengele kimoja tu au vipengele viwili ikaitoa maanani sheria yote ikaonekana haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika utaratibu huu ni vizuri zaidi kwa watunzi wa kanuni na sheria kuzingatia mazingira na matakwa halisi ya sheria na jamii nini inachohitaji kwa wakati huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano ningependa sana nilizungumzie ule usawa na uhalisia wa sheria na kanuni tulizoweza kuzipitia na mazingira halisi ya Watanzania tunayoishi. Nichukulie mfano ukiangalia mfano Sheria Ndogo ya Afya na Usafi wa Mazingira ya Halmashauri ya Itigi kipengele namba 14(3) kinaeleza wazi kwamba abiria yeyote atakayetupa taka nje ya basi la abiria basi itachukuliwa kosa hilo limefanywa na dereva, kondakta au mmiliki wa basi hilo, ukiangalia mantiki ya kutunga hiyo sheria unajua wazi kwamba lengo ni kuweka usafi wa mazingira katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la usafi wa mazingira katika nchi ni suala la Kikatiba ni wajibu wa kila mtu, ukiangalia Ibara 27(1) ni wajibu wa kila Mtanzania kuweka mazingira safi na salama. Tunajua dhamira ilikuwa ni nzuri lakini nani wa kuadhibiwa? Hakuna utaratibu duniani kosa lifanywe na mtu ‘A’ baadaye aende akaadhibiwe na mtu ‘B’ hiyo sheria itakosa maana, hivi kweli kosa kafanya abiria itakuwaje aende akaadhibiwe kondakta au mmiliki wa basi? Kwa nini? Tutoke na tukimbilie kumtafuta mmiliki wa basi, wakati mmiliki wa basi, dereva au kondakta katekeleza majukumu yake kuhakikisha usafi unadumu na unatekelezeka katika gari yake pengine kaweka dustbin na vifaa vingine vitakavyoweza kusababisha usafi usitoke nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini abiria mwenyewe tu akaamua kufungua kioo akatupa taka nje, leo hii unaenda kumkamata nani dereva, uwajibikaji katika sheria na usawa uko wapi? Sasa ukiangalia katika mazingira kama hayo haitokuwa hiyo sheria ina uhalisia katika utekelezaji, kwa sababu ni mwiko katika sheria kuadhibiwa mtu kwa kosa ambalo hakustahiki kuadhibiwa nalo hakuna kitu kama hicho duniani na haya itakuwa tuseme kwamba Tanzania tunatunga sheria za kwamba aliyefanya kosa mtu mwingine baadaye anakwenda kuadhibiwa mtu mwingine maana yake lile lengo la sheria halitofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu lengo la sheria ni kumfanya yule ambaye amefanya kosa kupata adhabu ili kutoa funzo kwa wengine wasirejee makosa kama yale, sasa leo kosa kafanya baba umeenda nyumbani baba umemkosa unamkamata mama na watoto haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ikiwa katika nchi hii tukitunga sheria za namna hiyo, tusema kwamba tunatunga sheria kwamba anayefanya kosa siye anayehusika moja kwa moja katika adhabu tunazidiana kwa niaba hivi kweli nchi inaweza kutawalika, sio kweli kabisa kitu cha namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kusema kweli katika hali kama hii tuangalie ile mantiki ni nini na kipi kinachotakiwa kufanywa ili sheria zetu ziweze kusadifu mazingira halisi na kugusa wale walengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliishie hapo nchi yetu kwa asilimia kubwa raia wake ni wakulima na wafugaji. Wakulima wanaishi sana katika sehemu za kijiji, vijiji vingi ndivyo ambavyo unaweza ukawakuta wakulima; ukienda katika Ibara ya 4(1) ya sheria ndogo ya Ada na Ushuru ya Halmashauri ya Itigi utaona wameweka baadhi ya masharti ambayo yanawataka wakulima wanapotaka kulima lazima wafuate kalenda ya Halmashauri, sio wazo baya lakini unajiuliza how come inaweza kutekeleza hii sheria kwamba sisi sote tulime kwa kufuata kalenda ya Halmashauri, ipo wapi hiyo kalenda ya Halmashauri. Namna gani una uwezo wa kuifuata wapi ipo, je, ni namna gani mwananchi anauwezo wa kuielewa imeandikwa, imebandikwa sehemu, imetangwazwa yaani unapatwa na maswali mengi ambayo yanauwezo wa kukosa majibu katika application yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuiandika ni rahisi, tamu kumeza, lakini ngumu kutafuna yaani kuitamka tu hivi kuiandika inawezekana kuwa rahisi, lakini namna gani katika utekelezaji wake ndipo shida inapokuja. Unaposema kwamba tufuate kalenda ya Halmashauri, tukienda katika aspect za utekelezaji kilimo unaweza ukakuta katika mazingira tuliyokuwa nayo mtu analima vile anavyojisikia, hakuna mtu anayelazimishwa kwamba bwana wewe uende ukalime analima kwa wakati wake na anavuna kwa wakati wake. Sasa ukisema kwamba tufuate hiyo kalenda, hiyo kalenda unapata maswali inaanzaje katika mazingira kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu analima yeye mwenyewe anavyojisika, anavuna yeye mwenyewe anavyojisikia, lakini hakuna sheria hata moja inayoenda kumlazimisha mtu kwamba lazima alime kwa eneo la ukubwa wa kiasi fulani, kwa maana hiyo itakuwaje tuki-impose kifungu cha sheria kinachotaka wakati wa kulima lazima ufuate kalenda ya Halmashauri, haiwezekani, itakuwa hilo ni jambo gumu. Unajiuliza hivi Halmashauri wana kalenda ya mvua? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake unaweza ukajiuliza mvua wanakalenda nayo wanajua ni exactly wakati gani mvua ina uwezo wa kunyesha. Hivi katika mazingira ya kawaida tunayoishi wale raia wa kawaida vijiji huku hivi taarifa hata hawana leo hii mnamtungia sheria za namna hiyo tunajua mantiki ni nini, lakini tuangalie ule uhalisia wa hiki kitu ambacho tunachotaka kwenda kukisimamia, pengine tukikosa kukiwekea mazingira mazuri basi hata utekelezaji wake utabakia katika maandishi tu lakini uhalisia utakuwa haupo kwa sababu kuna mazingira mengine mtu analima pengine kutokana na kipindi hiki nalima mazao haya na ardhi yangu nalima hiki hana kalenda huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwingine anaweza akasema kwa kipindi hiki nina uwezo wa kufanya jambo moja, mbili, tatu au ana uwezo wa kuanzisha kilimo cha umwagiliaji, hili kalenda ya Halmashauri ina nafasi gani katika suala hilo, lakini ukiachilia hapo katika wakulima vile vile kuna suala la wafugaji Ibara 3 ya hiyo kanuni na hiyo vilevile haikuacha imewekea masharti ambayo ni magumu kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano hiyo kanuni inamtaka mfugaji yeyote atayekuwa anafuga wanyama katika Halmashauri ya Itigi ni lazima idadi ya mifugo itaamuliwa na Halmashauri, Halmashauri ndio itakayokupangia wewe, wao ndio mabwana wakubwa itakupangia idadi ya mifugo utakayotakiwa kufuga. Kiukweli kabisa ukisoma hiyo sheria unajua mantiki ni nini tunajua kabisa ni matumizi bora ya ardhi pengine, lakini ukienda katika application vipi inaweza kutekelezeka, vipi inaweza ukaenda kum-control mfugaji amenunua eneo lake huko kijijini anafuga kuku wake, wewe utampitiaje mfugaji mmoja mmoja wa kuku halafu um-control. Hivi kweli inaweza kutekelezeka mtu anafuga kuku wake, njiwa, kwa sababu hiyo sheria ukija kutafsiri hilo neno wanyama, wanyama inajumuisha mjumuiko mpana zaidi maana yake ngo’mbe, kuku, bata, njiwa hata kunguru na mende pia vilevile ni Wanyama. Kwa sababu sheria imejumuisha, je, ana uwezo wa kufuga na nani? Ni binadamu na mende siku hizi wanafugwa na binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa namna gani ukiangalia unaweza kuchukua kama ni vitu vidogo vidogo lakini ukiangalie yule anayeiandika anaenda kuisimamia ni tofauti, sasa yule anayekwenda kuisimamia inawezekana akaja na mtazamo tofauti na yale malengo yaliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa masuala kama hayo ni vizuri yakawa under control, ni vizuri kwakuwa hizi sheria nyingi za Halmashari zinazotungwa takribani zote zinakuwa zinafanana sasa ili kuepuka matatizo kama haya ni vizuri watunzi wetu wa sheria wakawa wanaangalia ile mifumo inayoongoza katika utungaji bora wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)