Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kwanza kuweza kuchangia taarifa ya Kamati ya Sheria Ndogo. Kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Spika kwa kututeua kuwa kwenye Kamati hii ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili nimpongeze Mwenyekiti wa Kamati hii ya Sheria Ndogo kwa kufanya kazi nzuri ya kusoma hotuba ya Kamati hii ya sheria ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kusema kwamba wajibu wa kutunga sheria za nchi hii ni mamlaka ya Bunge lako tukufu, na wajibu huu wa kutunga sheria tumepewa kama Bunge kwa mujibu wa Ibara ya 4 na Ibara ya 64 ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na wajibu huu sisi kama Bunge tunao wajibu wa kuulinda kwa wivu mkubwa pale ambapo Bunge linakasimu haya madaraka kwa mamlaka zingine kutunga kanuni mbalimbali za kuendesha taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kama ambavyo taarifa imesomwa hapa, Bunge lako kwa mujibu wa Ibara ya 97 inayo Mamlaka ya kukasimu madaraka ya utunzi wa sheria ndogo kwa mamlaka zingine za Serikali, na miongoni mwa hizo mamlaka ni pamoja na Wizara mbalimbali na taasisi mbalimbali za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kumekuwa na shida kidogo siku za karibu, Bunge likitunga sheria mama ndani ya Bunge na kutoa mamlaka au kukasimu madaraka kwa mamlaka zingine kutunga kanuni, mamlaka hizi nyingine zimekuwa zikitunga kanuni ambazo wakati fulani zinakinzana na dhamira ya Bunge lako tukufu. Kwa sababu mamlaka ya utunzi wa sheria ni ya Bunge zinapokwenda kutungwa kanuni zingine na hizo mamlaka zikileta mkanganyiko kwa wananchi lawama zinakuwa ni kwa Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa kuanza tu naomba nitoe wito na rai sana mamlaka za Serikali zinazokasimiwa mamlaka na Bunge kutunga kanuni mbalimbali za uendeshaji wa shughuli zihakikishe zinatunga kanuni ambazo zinasaidia wananchi wetu kufanya kazi vizuri kwenye maeneo yao. Kwa sababu kumekuwa na kero nyingi kwenye kanuni na sio sheria za Bunge. Kwa mfano Bunge lako tukufu hapa ndani lilitunga sheria ya Bunge ambayo ni sheria ya watu wa EWURA ikitoa mamlaka kwa Wizara kutunga kanuni kuratibu uendeshaji bora wa vyombo vya usafirishaji wa abiria. Lakini kwenye utunzi wa kanuni kwenye mamlaka husika imekwenda kutungwa kanuni ambayo inaitwa The Land Transport Licensing Private Hire Regulations, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kanuni hii, kwenye kanuni ndogo ya 15(d) kanuni imeweka utaratibu kwamba wanaomiliki leseni za vyombo vya moto vya usafirishaji wa abiria kwa mfano wakiwemo watu wa bodaboda, watu taxi na kadhalika na watu wa bajaji, kila mmoja afunge mita kwenye chombo chake cha moto, ifungwe mita kwa ajili ya kukokotoa nauli za abiria. Kamati yako inajiuliza unafunga mita kwenye bodaboda kukokotoa nauli gani ya abiria. Kwa hiyo, sisi kama Bunge tunadhani waliokwenda kutunga hizi kanuni wanaweza kwenda kuleta kero kwa wananchi, na ikienda kuwepo kero inakuwa ni lawama kwa Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa hiyo kwakuwa Bunge lako lina mamlaka ya kufuatilia utunzi wa kanuni hizo, na kama zimetungwa kinyume na utaratibu au haziwezi kuwa na ufanisi mzuri Bunge lako linayo mamlaka ya kuitisha kanuni hiyo na kuirekebisha na ndio maana taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria Ndogo inaliomba Bunge leo hii, kwenye moja ya maazimio yake ni kwamba tunataka mamlaka husika ikarekebishe na kufuta makosa haya ambayo yamekwenda kujitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili, Bunge hili linapotoa maazimio kwa mamlaka ambazo zinatunga sheria ndogo mwaka jana mwezi Novemba Bunge liliazimia hapa ndani kwamba baadhi ya makosa ambayo yalionekana kwenye kanuni au sheria ndogo yakarekebishwe, lakini kama ambavyo taarifa imesomwa hapa leo, tangu mwaka jana mwezi Novemba hadi leo mwezi Septemba hizi kanuni hazijarekebishwa, tafsiri yake ni nini. Azimio la Bunge halijafanyiwa kazi. (Makofi)

Naomba kutao rai kwa niaba ya kamati ya Sheria Ndogo, maagizo ya Bunge Kwenda kurekebisha kanuni sio hisani, ni maelekezo ya Bunge na ni lazima yatekelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo jambo lingine ambalo pia limesemwa kwenye taarifa ya Kamati kwamba Bunge limetunga sheria mama kuweka adhabu kwa watu mbalimbali ambao watakiuka taratibu kwenye sheria ya The Energy and Water Utilities Regulatory Act Namba 414; kwenye kifungu cha 8 cha sheria hii kimetoa adhabu ambayo ni kiasi cha shilingi 300,000 au kifungo cha miezi 15 na kikaitaka mamlaka husika wa watu wa maji wanapokwenda kutunga kanuni zao za kuratibu vizuri zoezi hili la shughuli za maji wamekwenda kutuma kanuni ambayo imeongeza adhabu baada ya Bunge ambalo limeweka adhabu ndogo ya shilingi 300,000 wao wameweka shilingi 3,000,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge limesema adhabu isizidi miezi 15 kwa maana ya kifungo, wao wamekwenda kuweka miezi 15. Tunaomba kutoa rai tena kwamba tunaomba mamlaka zinazokasimiwa utunzi wa kanuni na sheria ndogo wazingatie maelekezo ya Bunge kwa ustawi wa nchi na wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba kuunga mkono hoja taarifa ya Kamati kwamba tunaliomba Bunge likubali na kutoa maazimio kwamba kwa kuwa hizi dosari ni kubwa na zipo kwenye taarifa ya Kamati, tunaomba ifikapo mwezi Novemba, 2022 marekebisho haya yakafanyiwe kazi. Na mwisho kama ambavyo taarifa imesema marekebisho ya mwisho yafanyike mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Bunge mfano mwaka jana hapa kupitia serikali na mapenzi mema ya Mheshimiwa Rais tumepunguza hata faini kwa watu wa boda boda kutoka shilingi 30,000 hadi shilingi 10,000 ili bodaboda wetu wafanye kazi vizuri, wafanye kazi kama Watanzania wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini inapofika mahali kunakuwa kuna kanuni ambazo badala ya kusaidia kazi nzuri ya bodaboda zinakwenda kuanzisha utaratibu wa kufunga mita, naomba Bunge hili lisikubali na lazima haya mambo yafike mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho naliomba sana Bunge lako tukufu, sisi kama Wabunge na wawakilishi wa wananchi tuendelee kufuatilia kanuni zote ambazo zimekuwa ni kero kwa wananchi wetu, na sisi kama Kamati yako ya Sheria Ndogo kwa niaba ya Bunge hili tukufu tutaendelea kufanya kazi hii, ili kusudi wananchi wetu waendelee kufanya kazi nzuri za uzalishaji kwa ajili ya maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa upekee sana naomba mamlaka zote ambao wanatunga sheria ndogo wasitunge sheria za udhibiti tutunge sheria za kuwezesha wananchi kufanya majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)