Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kutumia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waheshimiwa Mawaziri wote ambao walijadili Itifaki hii na kupendekeza iletwe Bungeni kwa ajili ya kupitiwa na kujadiliwa na kufanyiwa maamuzi, kwa sababu maamuzi yao ndiyo yamefanya tuwe na mjadala huu leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wenyeviti wa Bunge na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa kupokea Itifaki hii, kuijadili na hatimae kutoa maelekezo kwa Serikali kama ambavyo imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge Saba ambao wamechangia michango yao mbalimbali, niruhusu niwataje kwa sababu ni wachache sana. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Abdullah Ali Mwinyi - Mwanasheria msomi, kwa kutoa darasa la mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki leo. Naamini wale wagombea wetu wangekuwepo hapa leo, wangejua nini wanatakiwa kwenda kufanya wakienda kule Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Mollel, ametupa darasa la historia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki toka mwaka 1917 mpaka hii tuliyokuwa nayo leo. Pia ameelezea kwa ufasaha sana ni kwa nini tumechelewa kufika hapa ili kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote. Ninamshukuru Mheshimiwa Zainab Katimba, kama ambavyo amesema Mheshimiwa Jerry Silaa, wamejipanga pale leo kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri. Ninamshukuru sana Kaka yangu, Wakili Msomi, Mheshimiwa Tadayo Joseph, nae ametoa mchango mzuri sana na amesisitiza kwamba hii sasa inakwenda kuleta ushindani wa haki ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki katika mawanda ya kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana pia Mbunge jemedari, Mheshimiwa Aida Joseph Khenani. Mimi namuita Mbunge jemedari kwa sababu aling’oa mbuyu na ndiyo maana yuko hapa na tumeona mchango wake. Nimwambie tu Mheshimiwa Aida kwamba asiwe na wasiwasi, Mahakama hii haiendi kupora au kupoka mamlaka ya Mahakama yoyote, ila inakwenda ku-supplement pale ambapo tumekuwa na pengo na kumekuwa na tafsiri tofauti katika Itifaki hii, hatimaye kwenda kuongeza confidence kwa wafanyabiashara wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Jerry William Silaa, kwa jina maarufu Meya Mstaafu, nae ametoa mchango wake mzuri sana katika kuhakikisha kwamba Itifaki hii inafika vizuri. Ninamshukuru mchangiaji wa mwisho, Mheshimiwa Olelekaita, ni rafiki yangu sana, Mwanasheria Msomi, na yeye amechambua vizuri sana ikiwemo kuidadavua Ibara ya 5 ya Mkataba wa Kuanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo imesemwa, Jumuiya ya Afrika Mashariki inabebwa na nguzo muhimu Nne. Nguzo ya Kwanza ni Umoja wa Forodha, ili kuhakikisha kwamba masuala ya forodha yote katika Jumuiya yanakwenda sawa. Nguzo ya Pili ni Soko la Pamoja. Nguzo ya Tatu ni Umoja wa Sarafu, Nguzo ya Nne ni Shirikisho la Kisiasa ambalo bado halijakamilika katika uanzishwaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa madhumuni na majukumu ya nguzo hizi ambayo kimsingi ni kuongeza mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, suala la migogoro ni la kawaida. Suala la umuhimu na matakwa ya kutafsiri Itifaki mbalimbali ni la kawaida. Kwa hivi sasa Itifaki hizo zimekuwa zikitafsiriwa na nchi zenyewe, hivyo kuleta mgongano wa hapa na pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango ya Waheshimiwa Wabunge imesema bayana kabisa, sasa tunakwenda kutoa tofauti hiyo. Hivi sasa kuna uwezekano kwamba kifungu kimoja cha itifaki kikatafsiriwa tofauti Tanzania, kikatafsiriwa tofauti Kenya, kikatafsiriwa tofauti Uganda, kikatafsiriwa tofauti Rwanda, Burundi na South Sudan kutegemeana na Majaji waliokaa kwenye nchi hiyo wameangalia vipi, ili kuondoa mgongano huo ndiyo maana Mahakama hii ilipendekezwa iongezewe mamlaka yake. Kwa hiyo, hiki tunachokwenda kukifanya ni kuongeza mtangamano, tunaimarisha Jumuiya na kuondoa migogoro ambayo ilisababisha jumuiya hii kuvunjika mwaka 1977.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu zaidi tunakwenda kuleta confidence kwa wafanyabiashara wetu. Tunakwenda kuongeza confidence kwa wawekezaji katika Ukanda huu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwamba wakiwekeza fedha zao, wakifanya biashara, kuna chombo madhubuti cha pamoja chenye uhakika cha utatuzi wa migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mahakama hii iko Tanzania ni fursa kwetu sisi ambao ni wenyeji, tunaenda kuongeza ajira zaidi na kuifanya Tanzania iweze kung’ara zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Itifaki hii ni muhimu, na kwa kuwa imejadiliwa sana na Waheshimiwa Wabunge na kuungwa mkono kwa kiasi kikubwa sana, niruhusu sasa niliombe Bunge lako Tukufu baada ya maelezo hayo yote niliyoyatoa, baada ya kupokea taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, na baada ya michango thabiti ya Waheshimiwa Wabunge, kwa mujibu wa Ibara ya 63(3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kama ambavyo imefanyiwa mabadiliko, naomba sasa Bunge lako Tukufu katika Mkutano wake huu wa Nane, likubali kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki (The Protocol to Operationalize the Extended Jurisdiction of The East African Court of Justice).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.