Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata nafasi ya kuweza kuchangia katika azimio hili na kuridhia itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya kuiongezea mamlaka Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wote tunavyofahamu, Jumuiya ya Afrika Mashariki ilianzishwa mwaka 2001 Julai, lakini katika kuimarisha utengamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, nchi wanachama ziliweza kuanzisha na kuridhia itifaki tatu; Utifaki ya Uanzishwaji wa Umoja wa Forodha mwaka 2004, Itifaki ya Uanzishwaji wa Soko la Pamoja 2010, na Itifaki ya Uanzishwaji wa Umoja wa Sarafu Mwaka 2013. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki chote kunapotokea dosari katika utekelezaji wa itifaki hizi, basi Mahakama za nchi wanachama wa Afrika Mashariki na hasa kwenye nchi ambapo dosari imejitokeza, ndiyo zilikuwa zina mamlaka ya kuweza kusikiliza mashauri hayo. Hata hivyo, kwenye mkataba wa uanzishwaji wa Afrika Mashariki Ibara ya 9 vimeanzishwa vyombo na taasisi mbalimbali za kiutawala kwa ajili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na miongoni mwa taasisi hizo ni pamoja na kuanzishwa kwa Mahakama hii ya Afrika Mashariki. Mahakama hii pamoja na kuanzishwa kwake, kwenye mkataba wa huu wa uanzishwaji Afrika Mashariki imepewa mamlaka ya kutafsiri ule mkataba wa uanzishwaji wa Afrika Mashariki, yaani The East Africa Community Treaty.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ibara hiyo, au kwenye ule mkataba mama wa uanzishwaji wa Afrika Mashariki, Mahakama hii haiukupewa mamlaka ya kutafsiri itifaki hizi tatu nyingine zilizoanzishwa. Yaani Itifaki ya Kuanzisha Customs Union, Itifaki ya Kuanzisha Soko la Pamoja (common market) na Itifaki ya Uanzishwaji wa Umoja wa Sarafu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Ibara ya 27 ya Mkataba wa Uanzishwaji wa Afrika Mashariki Ibara ndogo ya (2), ibara hii imetoa mamlaka kwa nchi wanachama kuridhia itifaki kwa pamoja ya kutoa mamlaka zaidi kwa Mahakama hii ya Afrika Mashariki kusikiliza mashauri zaidi (extended jurisdiction), kwa kiswahili kidogo inakuwa inachanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa Ibara hii ya 27, Ibara ndogo ya (2) ina maana nchi wanachama wa Afrika Mashariki wanaweza kuiongezea Mahakama ile ya Afrika Mashariki. Sasa kwa muhktadha huu, nchi wanachama tarehe 20 Februari, 2015 kwenye Mkutano wa Kawaida wa 16 wa Wakuu wa Nchi, Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki waliweza kwa pamoja kupitisha azimio la kuiongezea Mahamaka ya Jumuiya ya Afrika Mashariki mamlaka ya kushughulikia masuala ya biashara, uwekezaji na sarafu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mujibu wa taratibu za jumuiya yetu hii ya Afrika Mashariki, nchi zinavyoleta azimo kama hili, ili sasa azimio hili liweze na nguvu na Mahamaka hii iweze kuongezewa mamlaka, ni lazima nchi wanachama na zenyewe ziweze kuridhia itifaki ile ambayo inakusudia kuanzishwa. Ina maana sasa, ndiyo leo hii tunaona Serikali imeweze kuona azimio la itifaki hii ili nasi kama nchi, kama wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki tuweze kuunga mkono itifaki hii na mwisho wa siku mamlaka za Mahakama hii ya Afrika Mashariki ziweze kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hatua tuliyofika ni muhimu sana kwa sababu kuridhia kwa itifaki hii kutawezesha kutatua migogoro ya kibiashara na uwekezaji ambayo inajitokeza katika utekelezaji wa itifaki hizi tatu nilizozitaja; Itifaki ya Uanzishwaji Umoja wa Forodha, Itifaki ya Uanzishwaji wa Soko la Pamoja na Itifaki ya Kuanzisha Umoja wa Sarafu. Kwa hiyo, nawaomba sana Wabunge wenzangu waweze kuwa sehemu ya kuridhia na kuunga mkono hoja hii iliyoletwa na Serikali kwa maana ina umuhimu mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, tukienda mbali zaidi, jumuku hili au hatua hii tuliyokuwanayo ni sehemu ya kuweza kurahisisha kuongeza utengemano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa maana ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo awali tunaona kwamba Mahakama za Nchi Wanachama ndizo zilikuwa na mamlaka ya kuweza kusikiliza mashauri yanayotokana na changamoto za itifaki hizi nilizozitaja, lakini sasa hivi tunataka kuipa Mahakama ya Afrika Mashariki jukumu la msingi la kutafsiri siyo tu mkataba wa uanzishwaji wa Afrika Mashariki, bali na zile itifaki tatu. Sasa katika sheria, sisi tunaona hatua hii itasaidia sana katika kuleta maendeleo sawia katika jurisprudensia ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo tu kwamba tutakuza jurisprudensia au tutaleta maendeleo zaidi ya jurisprudensia katika ukanda wa Afrika Mashariki, lakini kwa sababu hii Mahamaka itaanzishiwa sub-registries; ina maana kwenye hizo sub-registries, huduma itawafikia wananchi katika Jumuiya yote ya Afrika Mashariki na pia kutakuwa na fursa mbalimbali za ajira, kwa sababu sub-registries zikianzishwa au hii Mahakama ikiwa ina majukumu zaidi, kazi zikiwa zipo nyingi zaidi, ina maana kutakuwa na nafasi nyingi za kuajiri kada mbalimbali ikiwemo kada ya Majaji. Kwa hiyo, hili suala linatunufaisha kwa njia tofauti tofauti ikiwemo katika suala la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia machache hayo, naomba tena niendelee kuwasisitiza Waheshimiwa Wabunge wenzangu waweze kuunga mkono hoja hii iliyopo mbele yetu ili sisi kama nchi, Tanzania tuweze kuwa sehemu ya kupitisha itifaki hii ili Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki iweze kuwa na mamlaka zaidi ya kusikiliza mashauri mbalimbali katika Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)