Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Niwashukuru sana Wajumbe wote wa Kamati ya LAAC na Waheshimiwa Wabunge wote kwa maoni, mapendekezo na michango muhimu sana. Serikali imeichukua michango yote na tumeipokea kwa mikono miwili tutakwenda kuitekeleza moja baada ya nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nikianza na hoja ya matumizi ya fedha mbichi. Serikali ilishaweka utaratibu na miongozo kwamba ni marufuku taasisi yoyote ya Serikali kutumia fedha kabla ya kupeleka benki na tumeendelea kuboresha mifumo ya kielektroniki kuhakikisha mapato yote yanapelekwa benki na kutumika baada ya kupelekwa benki.

Mheshimiwa Spika, ni kweli baadhi ya watumishi bado wamekuwa na utaratibu wa kutumia fedha kabla ya kupelekwa benki na tutaendelea kuchukua hatua kuhakikisha tunadhibiti matumizi ya fedha mbichi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kufutwa kwa baadhi ya miamala. Serikali hivi sasa tumewekeza sana kuboresha mifumo ya kielektroniki, lakini tunakwenda kuiboresha kuweka system ambazo zitadhibiti wale operators wasiwe na access ya kufuta miamala kwa manufaa yao binafsi. Kwa hiyo, hili Serikali tumelichukua, tunakwenda kuweka mifumo hiyo kudhibiti wale ambao wana nia mbaya ya kutumia vifaa hivyo kufuta miamala.

Mheshimiwa Spika, pia tutaweka bureaucracy ili Maafisa Masuhuli wawajibike kufuta miamala na siyo kila operator awe na access ya kufuta hiyo miamala.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Force Account kuweka kiwango, ni kweli tuliweka utaratibu majengo ya ghorofa yanakwenda kwa Makandarasi, yale ya chini tunatumia Force Account. Hata hivyo, wazo ni zuri, tumelipokea, tutakwenda kuweka kiwango ambacho kitakuwa cha Force Account na kiwango ambacho kitakuwa lazima kitumie contractors. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Wahandisi, Rais wetu ameajiri kwa dharura Wahandisi 246 mwezi Oktoba, 2021 kwa ajili ya Halmashauri zote 184 na mikoa yetu yote na zoezi hili ni endelevu, tutaendelea kuboresha ikama ya Wahandisi ili wasimamie vizuri miradi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na udhahifu wa makusanyo ya mapato ya ndani, ni wajibu wa Halmashauri zote kuhakikisha wanakusanya mapato ya ndani kwa 100% na kuhakikisha fedha zile zinapelekwa kwenye miradi ya maendeleo ya wananchi yenye tija na kukamilisha miradi ile kabla ya kuanza miradi mingine. Kwa hiyo, tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge na Kamati na Serikali tumeanza kutoa maelekezo hayo kuhakikisha hili linatekelezwa na fedha hizo zinapelekwa kwenye miradi ya maendeleo ikiwemo 40%, 60%, na 10%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la Wakuu wa Idara kukaa kwa muda mrefu katika Halmashauri zetu; tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeanza kufanya tathmini nchi nzima kwa Wakuu wa Idara wote waliokaa kwa muda mrefu na tumeanza na Waweka Hazina, Maafisa Utumishi, Wakaguzi wa Ndani pamoja na Maafisa Mipango. Utaratibu huo ni endelevu. Tunataka tuhakikishe Wakuu wa Idara hawa overstay kwenye vituo vyao ili kuepusha kuwa na mazoea kufanya kazi na baadaye kuwa na mianya ya upotevu wa fedha za Serikali. Kwa hiyo, suala hili tunakwenda kulifanyia kazi na tutahakikisha tunafanya hili zoezi kuwa endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake niseme Serikali tumepokea maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge na tutakwenda kuyafanyia kazi ili kuhakikisha mamlaka ya Serikali za Mitaa zinatoa huduma na kupeleka miradi ya maendeleo kwa wananchi kwa kadri ya malengo ya Serikali kwa manufaa ya wananchi wenzetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, namshukuru sana na ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)