Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. kwanza nami niungane na wenzangu kuipongeza sana Kamati yetu chini ya Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Kitandula. Lakini pia kuzipongeza Wizara zetu hizi mbili; Nishati na Madini, kwa kazi kubwa ambayo inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa jambo kubwa sana ambalo amelisimamia, kwamba miradi mikubwa iliyoanzishwa huko nyuma katika Awamu yao ya Tano atahakikisha kwamba inakamilika. Na hapa nauzungumzia Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania lazima tujitambue. Kuna wakati tunaweza tukawa tuna malengo makubwa, mazuri ambayo yametupa heshima katika nchi yetu. Halafu baadaye kwa sababu moja au nyingine, kwa sababu labda pengine uongozi mmoja haupo umekuja uongozi mwingine, watu wengine wanaweza kufikia kujaribu kutuchezea kwa kutushauri tofauti ili tushindwe kwenda kule tulikotaka kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Rais amedhamiria na ametangaza hadharani, nawaomba Wizara ya Nishati tafadhali tusimuangushe Mheshimiwa Rais wetu. Tuhakikishe mradi huu wote kwa pamoja tunashirikiana, timu iliyopo sasa na hata ile iliyokuwa mwanzo, kama kuna jambo ambalo wao wanalifahamu mshirikiane kuhakikisha kwamba tunakwenda vizuri. Sisi hatuangalii sura ya mtu, tunaangalia umeme upatikane katika Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tuhakikishe kwamba power master plan inatekelezwa inavyotakiwa, kadri umeme unavyozalishwa wakati huo huo na miundombinu mingine ya ujenzi wa line ikamilike sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza kwa sababu umeme usipozunguka kwenye mita ina maana wizara nyingine pia zitapata shida. Tuwapongeze kupita EWURA, REA inapata fedha, Wizara ya Maji wamenyamaza hapo wapongezwe wanapata fedha, lakini vilevile Mfuko wa Barabara unapata fedha kupitia wizara hizo, kupitia mafuta. Kwa hiyo tusishangae tu kwamba bei za mafuta ni kubwa wakati kuna tozo tumeweka huko ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hata Wizara ya Ardhi sasa inapata fedha kupitia LUKU, kwa hiyo wote huo ni mchango wa Wizara hizi. Sasa nini ninachotaka kusema. Wizara ya Nishati hasa kwenye masuala ya umeme, Shirika la TANESCO siyo la kibiashara kama tunavyoliona, ni shirika ambalo ni la kihuduma. Kwa hiyo hata tunapopanga bajeti zetu tuhakikishe tunapeleka fedha za kutosha kwa sasa fedha nyingi ukiangalia Wizara inaonekana ina bajeti kubwa sana, lakini nenda kwenye miradi ile mipya katika masuala ya matengenezo fedha inayokwenda ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuhakikisha kwamba TANESCO wafuatilie upotevu wa umeme usio wa lazima ambao siyo wa kiufundi. Kwa mfano, wizi wa umeme, umeme unaopotea kutokana na nyaya chakavu, hilo walifanyie kazi, lakini sisi Wabunge kwa pamoja kama kweli tunataka kufikisha huduma hii kwa watu wetu kwa ukamilifu, Wizara hii itengewe fedha za kutosha kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu. Vile vile kwa ajili ya kuwekeza kwa ajili ya hawa wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa hawana umeme, hasa vijijini ambako wanaanza kujishughulisha na kutengeneza ajira kupitia viwanda na kazi ndogondogo za kiumeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukatika kwa umeme kuna sababu nyingi, sababu mojawapo alizosema za kuzidiwa kwa mitambo, ukiangalia system ya umeme haipo kwenye uzalishaji tu yaani generation; kuna uzalishaji, kuna hizi transformer ambazo zinaweza kutoa umeme, kupandisha kwenda juu au kuushusha, lakini vilevile nyaya zenyewe. Pia kuna changamoto hata namna ya kuboresha hiyo miundombinu. Watu wa Ardhi wanapotenga maeneo ya viwanja vyao unakuta ni mara chache sana wanatenga maeneo ya kuweza kujenga vituo vya umeme au njia za kupitishia line za umeme. Kwa hiyo, unakuta hata namna ya ku-improve inakuwa ni shida. Niwaombe Wizara hizi kushirikiana ili kuhakikisha kwamba wote wanatoa support kwa Wizara zingine ikiwemo kupeleka umeme kwenye Stangold, haiwezekani watumie mafuta wakati umeme unaweza ukasaidia. Ahsante sana. (Makofi)