Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni ya leo nami nichangie hoja iliyo mbele yetu. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha sisi wote kuwepo hapa tukiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo vibaya kuendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyoiheshimisha Tanzania. Hatuna cha kumlipa mama yule zaidi ya kumwombea dua. ndugu Watanzania tuendelee kumwombea dua Mwenyezi Mungu ampe umri mrefu ili aendelee kuiheshimisha Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita zaidi kwenye Kamati ya Miundombinu kwa sababu nahudumu kwenye Kamati hiyo. Kwa hiyo basi, mchango wangu ni kusisitiza yale ambayo Kamati wameyazungumza. Hapa niseme, naipongeza sana Kamati yangu ikiongozwa na Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Selemani Kakoso kwa kazi kubwa tuliyoifanya mpaka kufikisha Kamati kuweza kuleta taarifa hii hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msisitizo wangu, naomba niiambie tu Serikali, tunayo sera. Nianze na sera ya kuunganisha mikoa ya Tanzania kwa barabara za lami. Sera hii kama haitekelezeki, siyo dhambi tukaiondoa kama ambavyo tuliondoa sera ya kujenga kituo cha afya kila kata, tukasema tunaenda kujenga kituo cha afya kwa mujibu ya mahitaji. Vile vile kwenye sera hii, kama tunaona hatuwezi kuifikia, basi tuiondoe kuliko kuendelea kubaki hapa wakati utekelezaji wake bado unasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hivyo kwa sababu, leo kuna baadhi ya mikoa bado kabisa haijawahi kuunganishwa kwenye mikoa hii, lakini tayari tumechangia kwenye kuunganishwa wilaya kwa wilaya kwa barabara za lami. Mfano mzuri Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Morogoro bado haujaunganishwa kwa kipande cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulisisitiza ni kuhusu Sheria ya Manunuzi ya Umma. Kama kuna jambo linatukwamisha Watanzania kwenye hizi Taasisi zetu ni za Umma kufanya biashara au kwenda na ushindani, ni kwa sababu ya Sheria ya Manunuzi ya Umma. Nitoe hapa mfano wa TTCL. Shirika hili lilitakiwa kununua mitambo iliyokuwa imeachwa na Celtel, lakini kwa sababu tu sheria hairuhusu kununua mitambo ya Secondhand, ile mitambo ilinunuliwa na watoa huduma wengine na wanaitumia. TTCL tumeshindwa kuinunua kwa sababu kwenye sheria zetu hairuhusu Taasisi ya Umma kununua vifaa secondhand. Hili jambo naomba liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko huko kwenye TTCL, wao wanachukua fedha kutoka UCSAF kwa ajili ya kupeleka minara kwenye sehemu ambazo hazina mvuto wa kibiashara, lakini wale TTCL pamoja kwamba wamepewa miradi hiyo, utekelezaji wao upo chini sana ukilinganisha na watoa huduma wengine. Leo hii Vodacom akipewa shilingi milioni 200, kesho anaingia dukani, ananunua vifaa, anakwenda kutengeneza mradi. TTCL akipewa shilingi milioni 200 ataanza kutangaza tender miezi mitatu; Sijui Bodi ya tender ikae miezi miwili. Mpaka kuja kupata mkandarasi tunachukua miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nalo siyo jema. Kama kweli tunataka kusaidia hizi taasisi zetu za Umma zifanye biashara, basi hatuna sababu ya kuacha kufanya mapitio Sheria yetu ya Manunuzi ya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninaloweza kushauri ni kuhusu TAZARA. Wakati TAZARA inaanzishwa umuhimu mkubwa ilikuwa ni Wazambia walikuwa wanaihitaji zaidi kuliko Watanzania. Lakini leo baada ya maendeleo ya kiteknolojia Wazambia wameshaonesha nia kwamba hii TAZARA hawaihitaji tena, yaani siyo muhimu tena kwao, siyo kipaumbele tena kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni nini; matokeo yake sisi Watanzania hatuwezi kuweka mtaji pale kwa sababu ukishaweka mtaji pale unakuwa ni mtaji wa nchi zote mbili. Tena sheria yenyewe inaitaja TAZARA kama Zambia ndio wana share kubwa kuliko Tanzania.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Kuchauka.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi baada ya hayo naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)