Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja za kamati mbili ambazo ziko mezani.

Kwanza nianze kwa kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini na kuniteua kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, inayoshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Rais kwamba nitafanya kazi yangu kwa bidii yote na kwa uadilifu wa hali ya juu ili kuhakikisha kwamba malengo ya Wizara hii yanatekelezwa kwa ufanisi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kupongeza Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa kuchaguliwa kuongoza muhimili huu muhimu lakini pia niwapongeze wenyeviti wa kamati hizi mbili kwa sababu nao wamechaguliwa hivi karibuni nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo naomba niishukuru kamati zote mbili kwa taarifa zao nzuri ambazo kwa hakika zimesheheni maoni na mapendekezo mazuri ambayo yanaonyesha jinsi gani wajumbe wa kamati hizi wana uweledi wa hali ya juu na wamechambua kwa kina masuala ambayo yanahusiana na kamati na mimi nazungumzia hususan yanayohusiana na eneo la Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana na kama alivyosema jirani hapa kimsingi yote ambayo wameyashauri ni mambo ambayo yanakwenda kujenga kuongeza tija katika utendaji wetu wa kazi kwa hiyo niseme kwamba tumeyapokea na tuwahakikishie kwamba yote tutayafanyia kazi kwa ukamilifu na tutatoa taarifa ya namna ambavyo tumefanyia kazi maoni na mapendekezo ya kamati nawashukuru sana wajumbe kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nizungumzie baadhi ya maeneo kwa uchache katika taarifa ya kamati ya Katiba na Sheria wamezungumzia suala la kiwanda cha viatu kule Kilimanjaro na kiwanda hiki ni muhimu kwa sababu kinachochea upatikanaji wa soko la ngozi kwa wafugaji wetu ina maana kwamba kadri kitakavyofanya vizuri basi tutaongeza na kipato kwa wafugaji wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali inaona umuhimu wa kiwanda hicho na tunashukuru kwamba wametushauri tuendelee kuongeza masoko jambo hilo tunalifanyia kuhakikisha kwamba tuna masoko endelevu na kwa kuanzia kiwanda tayari kimetangaza nafasi za mawakala watanzania ambao wako tayari kuwa mawakala wa kuuza bidhaa zinazotengenezwa na kiwanda hicho viatu pamoja na bidhaa nyingine za Ngozi. Kwa hiyo. niwahamasishe kwamba wachangamkie hiyo fursa kwa sasa hivi tunafanya uchambuzi wa maombi yaliyopokelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile tumeshauriwa tuhakikishe kwamba tunajitangaza kupitia maonyesho hilo Ofisi ya Waziri Mkuu itasimamia kuhakikisha kiwanda kinatumia fursa zote za maonyesho zinazokuwepo lakini hata kuja hapa kwa Waheshimiwa Wabunge kwa sababu Waheshimiwa Wabunge ni jeshi kubwa wanawakilisha watanzania. Kwa hiyo, akifahamu vizuri bidhaa hizi watakuwa mabalozi wazuri wa kusaidia kututangazia, kwa hiyo, hilo tutalizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo ambalo limezungumziwa pia sana ni kuhusiana na hii 4% inayokwenda kwa vijana fedha za halmashauri pamoja na mfuko wa maendeleo ya vijana kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeshauri kwamba Wizara ya Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na TAMISEMI tufanye ufuatiliaji wa hizi fedha zinazoenda kwa vijana. Hilo nalipokea na niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba hili lilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Rais alipoongea na vijana kwenye uwanja wa Nyamagana siku ya tarehe 15 Juni, 2021 kule Jijini Mwanza alizungumzia suala hili fedha zinazotolewa kwa vijana kwamba Serikali imekuwa ikitoa fedha kwa vijana lakini wakati mwingine vijana wanakuwa hawana taarifa sahihi za hizi fedha kwa hiyo wanakuwa hawanufaiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alihoji kwamba wale wanaonufaika wanafanyaje kufanya marejesho ili vijana wenzao waweze kunufaika. Ni dhahiri kwamba kauli ya Mheshimiwa Rais inatutaka sisi ambao tunahusika moja kwa moja na kusimamia vijana pamoja na TAMISEMI ambao inahusika na kutoa hizi fedha tufanye ufuatiliaji na kutoa miongozo na hata kutoa elimu kwa wale wanaopata hizi fedha tutoe elimu ya ujasiriamali na mafunzo ili kuhakikisha kwamba zinakuwa na tija na zinazunguka ili ziweze kwenda kuwakopesha vijana wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumzia ni changamoto ambazo baadhi ya vijana wanapata kuhusiana na fursa ambazo zinatolewa za kukuza ujuzi. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametupatia bilioni 9 kwa ajili ya kukuza ujuzi na kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge baadhi ya vijana wanapata changamoto kwa sababu wako mbali niwaambie kwamba Serikali ni sikivu jambo hilo tumeshaanza kulichukulia hatua wale wanaofanya mafunzo ya kilimo kitalu nyumba tunawalipa shilingi elfu 10 kwa siku kuwawezesha kwenda kuhudhuria na wale ambao wanapata mafunzo ya uzoefu kazini tunawalipa 150,000 kwa mwezi na tutaendelea kufanyia kazi changamoto hii na kuangalia namna bora zaidi ya kuhakikisha tunafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimalizie kwa kuunga mkono hoja kwa kamati zote mbili nashukuru sana kwa ushauri tutaufanyia kazi. (Makofi)