Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya. Pia niwapongeze Wajumbe wa Kamati zote mbili kwa kazi kubwa ambayo wameifanya ya kuleta mapendekezo na ushauri wa namna ya kufanya katika mambo haya ambayo tunayajadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nipongeze Wizara zinazohusika na mjadala tunaoujadili hapa, hususan Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa usimamizi mzuri wanaoufanya huko kwenye halmashauri zetu, lakini pia Wizara ya Utawala Bora kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kusimamia Utumishi na kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo kama sitampongeza Mheshimiwa Rais kwa pesa nyingi alizotuletea kwenye halmashauri zetu hususan pesa zilizotokana na mkopo nafuu maarufu kama pesa za Mama Samia ambazo zimefanya kazi kubwa ya maendeleo huko Wilayani kwenye elimu, afya na maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi zinaendana na ushauri ambao nataka niutoe hasa kwenye Wizara ya TAMISEMI na Utawala Bora kwenye namna ya kufanya majukumu yaende vizuri huko kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyosemwa awali katika Ibara ya 145 ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, majukumu ya usimamizi yameshushwa kwenda kwenye Serikali za Mitaa. Katika Serikali zetu za Mitaa zipo hizi halmashauri za Wilaya, Majiji na Manispaa, wasimamizi wakuu wa halmashauri hizi ni Mabaraza ya Madiwani. Mabaraza la Madiwani ndiyo yametamkwa kama wasimamizi wakuu wa halmashauri zetu na Serikali za Mitaa, lakini kwa jinsi hali inavyokwenda tunaweza tukajikuta tunatengeneza mipango huku juu tukiiteremsha huko chini haifanikiwa vizuri kwa sababu hawa wanaosimamia hizi halmashauri zetu bado hatujawawezesha kiasi cha kutosha ili waweze kusimamia vizuri halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka hapa kwenye Bunge la Bajeti tulizungumza kuhusu kuhamisha malipo ya Madiwani yatoke kwenye halmashauri kwa mapato ya ndani na yalipwe na Serikali Kuu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Viongozi wa Serikali kwa kulikubali suala hili. Limesaidia kwa kiwango kikubwa sana ingawaje bado malipo yale ni madogo, lakini limesaidia sana. Sasa hivi kuna tatizo moja kwenye halmashauri huko kuhusu posho za vikao vya Madiwani, Wakurugenzi wengi wanafanya kazi hizo kwa kutumia vichwa vyao na siyo utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umefikia wakati nikitoa mfano wa Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba, sasa hivi viko vya Baraza la Madiwani, Madiwani wanaenda tu ili liende kwa sababu Madiwani wote wanaotoka Jimbo la Sumve ambalo halina hata Makao Makuu ya Wilaya hawalipwi pesa ya kulala, wanalipwa pesa anaambiwa Diwani aende kwenye kikao cha halmashauri amalize kikao arudi nyumbani, ukimuuliza Mkurugenzi anasema kuna wakara. Hizi nyaraka za Serikali zinazozungumza kuhusu posho za Madiwani, nimejaribu kuzipitia nimekuta zipo nyaraka karibu tisa na inaonekana nyingine sijaziona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tuwasaidie hawa Madiwani imefika wakati Bunge hili la Serikali tuamue kutoa utaratibu wa aina moja unaosimamia maslahi ya Madiwani ili halmashauri zetu ziweze kusimamiwa na watu ambao wana uhakika na wanachokifanya, vinginevyo sasa hivi Madiwani wanaenda kwenye vikao kutimiza wajibu tu wanawahi warudi nyumbani. Sasa wasimamizi wa halmashauri wasipokuwa na uhakika na wanachokifanya mwisho wa siku ndiyo mwanya wa wizi na ubadhirifu tunaendelea kuuona unaendelea kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka kushauri, Serikali na Bunge tutoe maelekezo ya aina moja, yanayofanana nchi nzima ya namna ya kushughulikia maslahi ya Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)