Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo nami kuwa sehemu ya wachangiaji kwenye siku ya leo. Kwanza naanza kwa kuwapongeza sana Mawaziri wa Ofisi ambazo zinawasilisha taarifa zao kwenye Kamati ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa namna ambavyo leo wamewasilisha taarifa zao na wameweza kujibu changamoto mbalimbali ambazo Wajumbe tumeweza kushirikiana nao. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nichangie maeneo mawili tu. Eneo la kwanza, naishukuru Serikali juu ya fedha za miradi mbalimbali ambayo imepelekwa kwenye maeneo yetu. Hata hivyo, fedha hizi Wabunge wengi wamezungumza hapa, zinaweza zikaenda kwenye maeneo mbalimbali katika nchi hii lakini zikienda kwa uwiano ulio sawa zinaweza zikashindwa kufikisha malengo ya kumaliza matatizo ya wananchi kwenye maeneo tofauti ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo yana changamoto mbalimbali za ujenzi kutokana na umbali wa kupata bidhaa zinazoweza kutufanyia shughuli za ujenzi kwenye maeneo hayo. Tunapopeleka fedha kote zikifanana kunakuwa na changamoto mbalimbali za kuweza kufanikisha miradi hii, na badala yake tunaacha manung’uniko na wananchi wengi wakiona kwamba miradi mingine inakuwa haijakamilika; au kuzipa Halmashauri majukumu mengine makubwa ya kuangalia ni namna gani wanaharibu bajeti nyingine za kutoka kwenye own source na kumalizia miradi iliyobaki.

Mheshimwia Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vyema Serikali ikaendelea na utaratibu wa kuangalia gharama halisi ya mahitaji ya kuweza kukamilisha miradi kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nami nataka nichangie leo, ni hili eneo la asilimia 10 ambazo zinakwenda kutoka katika maeneo mbalimbali ya makundi ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Mfuko huu ni mzuri sana na unakwenda kumaliza matatizo mengi ya wananchi hasa pale kwenye kupata mitaji ya kuweza kufanya shughuli zao ili waweze kujikimu kimaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo zipo changamoto mbalimbali tukiwa kwenye Kamati, TAMISEMI wamejaribu kuzieleza. Changamoto hizi zinakwamisha baadhi ya jitihada na malengo ya mfuko huu. Kwa mfano, utakuta kuna baadhi ya maeneo kuna vikundi vimeundwa, vina watu wenye rika tofauti. Ni wamama lakini wana rika tofauti, lakini kwenye vikundi vyao humo kuna wababa nao wako kwenye sehemu hiyo. Ila kwa mujibu wa mwongozo uliopo, wanalazimika wale wababa wakae pembeni, wapewe wamama, japo kwenye kikundi chao hicho miaka yote na siku zote wanazalisha bidhaa zao wakiwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ijaribu kutazama namna bora ya kuweza kusaidia; lengo la huu mfuko ni kuinua kipato cha wananchi kwenye maeneo yetu. Sasa tunapokuwa tunakwenda tukiangalia maeneo fulani fulani inaweza ikapunguza ile nguvu ya kufikisha huduma hii kwa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwenye rika pia la vijana. Vijana wamepewa pale kuanzia miaka 18 mpaka 35. Hebu tuangalie kwa ukweli, sisi sote ni Wabunge, tunafahamu. Majimboni kwetu, ukiangalia rika linalozalisha au lililojikita kwenye kufanya biashara mbalimbali, linapita hili eneo na ndio wenye mahitaji makubwa sana ya mitaji. Kwa hiyo, naishauri Serikali irudi iangalie mfumo ule vizuri, iangalie ile sheria ili ikae vizuri. Kwa sababu hili kundi la vijana, wengi wanashindwa kuzichukua hizi fedha kwa sababu rika lao wengine ni dogo; miaka 18 mpaka 20 wengine bado wako katika mazingira ya shule, lakini wanayoihitaji mitaji hii ili waweze kukuza biashara zao na kutunza familia zao wako zaidi ya hili rika la miaka 35. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikajielekeza, kwa sababu dhamira ya kuuanzisha mfuko siyo tu ikakae kule ikawe kama ni maigizo fulani, lengo ni kutatua matatizo ambayo wananchi wanayo. Tunalo rika la kati linaloanzia miaka 35 mpaka 45 ambalo ndilo limejikita kwenye biashara ndogo ndogo, ndiyo limejikita kwenye kilimo, ndiyo lina shida kubwa sana ya kupata mitaji yao. Kwa hiyo, Serikali ni vyema ikaangalia upya, ije na namna ambavyo inaweza ikalisaidia hili kundi kubwa; na sio kazi ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hata Mheshimiwa Rais amezungumza kwenye zile fedha za UVIKO ambazo amepata, ameelekeza baadhi ya fedha kwenda kwa Wamachinga. Hebu tujiulize, wamefikiriwa wale kwa sababu lile kundi ni kubwa na lilikuwa halina sehemu linaweza likapata fedha kama isingekuwa kufikiriwa kupangiwa fedha hizi. Naamini kwa kutumia own source inawezekana kabisa asilimia 10 ingewasaidia hawa na wangekuza mapato yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kuna vikundi vya vijana ambavyo vipo vijijini, lakini wengi wanapewa fedha; wakishamaliza kupewa fedha, unaweza kukuta baada ya siku mbili tatu wamegawana, wamemaliza shughuli, hawana cha kufanya. Mimi nafikiri Serikali ingetoa mwongozo maalum, wapewe vikundi ambavyo wana jambo wanafanya ili wakaongeze tija kwenye jambo lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukienda kwenda bonde la watu wa Ruvu, watu wanalima; vijana wanalima kule. Ni vyema mkawaangalie wanaolima bila kujali rika lao, wawezeshwe ili walime kwa ubora, wavune wafanye biashara wapate kukidhi mahitaji ya maisha yao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiriakwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisikia kengele, basi kwa machache haya, naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)