Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza, nami nitumie fursa hii kukushukuru wewe. Pia kipekee niipongeze Kamati yangu ya Katiba na Sheria kwa namna ambavyo inasimamia na kutekeleza majukumu yake ya Kikamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende katika mchango wangu mfupi kwa taarifa ambayo imewasilishwa mbele yetu. Mimi nitajadili mfumo wa utoaji wa haki nchini. Kwanza naomba niipongeze Mahakama kwa namna ya kipekee wanavyojitahidi katika masuala mazima ya utoaji wa haki na uendeshaji wa kesi Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali ya pongezi hizi, bado zipo changamoto, bado yapo malalamiko mengi kwa wananchi juu ya mhimili wetu huu wa Mahakama katika masuala mazima ya utoaji wa haki na usimamizi wa kesi ama uendeshaji wa kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu, wananchi hawawezi wakalalamika tu juu ya Mahakama hii, maana yake ni kwamba kuna sababu za msingi ambazo zinawafanya wailalamikie Mahakama. Mimi kama Mbunge naomba nichukue fursa hii kuiomba Serikali sasa, ipo haja na sababu za makusudi za kuongeza watendaji katika Mahakama yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini tutakapotumia nafasi hii ya kuongeza watendaji katika Mahakama, itakuwa ni sababu ya kupanua wigo, itakuwa ni sababu ya kurahisisha usikilizaji wa kesi na utoaji wa hukumu kwa kipindi kifupi baada ya kesi kusikilizwa. Kama tutafanya hivyo, tutawasaidia na kuwapunguzia kero wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifahamike kuna watu wanatoka masafa ya mbali kwenda katika Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya na katika Mahakama za Mikoa kusikiliza kesi ama hukumu za kesi zao, lakini wanapofika katika Mahakama zile wanaambiwa leo Jaji ama Hakimu ana kesi nyingi, kwa hiyo, warudi wanapangiwa tarehe nyingine. Hiyo tarehe ikifika, wanapangiwa tarehe nyingine. Mwananchi yule maisha yake ni duni, maisha yake ni magumu, anatoka masafa ya mbali, anakuja bila mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nadhani ili kutatua changamoto hii, ipo haja Wizara ya Katiba na Sheria sasa kufikiria upya namna ya kuwaongezea maslahi Mahakimu hawa. Utakapowaongezea maslahi Mahakimu hawa tutapunguza kero na malalamiko kwa wananchi. Itakuwa ni sababu ya kuepuka vishawishi kwao na watafanya kazi kwa ufanisi, weledi na watatenda haki kiukweli kabisa na wananchi hawatalalamika. Katika hilo, naamini vishawishi vipo na zipo namna za kutatua vishawishi hivi na njia pekee, tuwaongezee maslahi watendaji wa Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni la msingi, ni moja tu; kwenye Magereza zetu kumejaa mahabusu. Mahabusu ni wengi mno! Sasa kama Mahakama, kama Wizara au kama Serikali itafanya jambo la kusudi, kwenda katika Magereza yale kutafiti na kuhakiki ni mahabusu wangapi ambao wamo ndani ya Magereza yale, halafu wakafanya utaratibu; wale ambao wanaona kwamba ipo haja ya kuwatoa, wakawa wapo uraiani na upelelezi wa kesi zao unaendelea, basi nadhani ipo haja ya kufanya hivyo ili kupunguza mzigo kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale mahabusu wakiwemo mle Magereza Serikali inatoa fedha kwa ajili ya kuwalisha; na wale wanapotoka baadaye Serikali ama Mahahama inapowaambia ninyi mmetoka, hamna kesi. Wamekaa miaka mitatu, minne, nane. Wakija uraiani, maisha kwao yanakuwa ni magumu, wanakosa uaminifu na ushirikiano na jamii inayowazunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali, wafanye jitihada za makusudi na za kipekee kabisa, kufanya uhakiki Magerezani. Ambao tunaona wanafaa tuwatoe nje, wakati wa wako nje upelelezi wao unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)