Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi, lakini juu ya hayo namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kukamilisha uchaguzi. Nawashukuru wapiga kura wa Biharamulo na Watanzania kwa ujumla kwa kukamilisha zoezi hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea nina maneno machache ya utangulizi. Siku moja nilikuwa kwenye benki moja ambayo sitaitaja jina, nikakumbana pale kwenye meza ya huduma kwa wateja na mzee mmoja ambaye alikuwa na malalamiko yanayofanana na ya kwangu. Yeye anasema ameweka kadi kwenye ATM, karatasi ikatoka kwamba pesa zimetoka, lakini pesa hazikutoka, nami nilikuwa na tatizo kama hilo. Alipowaeleza wale wahudumu, wakaja kama watano wanaeleza namna ambavyo mfumo wa computer unafanya transaction na maelezo mengi ya kitaalam. Yule mzee akawaambia vijana sikilizeni, mimi kama mteja wa benki yenu nina kazi mbili tu, nina kazi ya kuweka pesa na kutoa pesa. Hiyo habari ya mchakato unakwendaje, transaction system kazungumzeni huko halafu mje na pesa. Kwa nini nasema hivyo? Watanzania hawa ambao wanalitazama Bunge hili nao wana kazi tatu…
MBUNGE FULANI: Hawasikii hao!
MHE. OSCAR R. MUKASA: Vyovyote, watafahamu na watasikia, kuna namna watasikia. Wana kazi ya kufanya kazi, wana kazi ya kulipa kodi na wana kazi ya kudai huduma kwenye sekta mbalimbali basi, hawana kazi nyingine. Kazi hizi za kwamba kanuni iko hivi na nini ni muhimu, lakini mwisho wa siku wao wanataka matokeo.
Leo Mheshimiwa Zitto Kabwe, sijui kama yupo, huwa namheshimu sana, lakini leo amenishangaza. Amefanya…
Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimu sana rafiki yangu Zitto ni Mbunge makini. Nakwambia wewe Mwenyekiti, namheshimu sana Mheshimiwa Zitto, ni Mbunge makini na ninyi mnafahamu; lakini leo na siku chache zilizopita nimeshangaa kidogo na namwomba asiendelee kunishangaza.
MHE. OSCAR R. MUKASA: Kwamba Ijumaa Bunge lilipoahirishwa nimefanya hesabu ya haraka haraka, nakubaliana kabisa kwamba kazi ya wapinzani ni kuisimamia Serikali na hawakuja hapa kuishangilia, hilo linafahamika kabisa. Hata hivyo, kazi hiyo lazima ifanyike kwa namna ambayo ina maslahi kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ijumaa lilipoahirishwa Bunge, kwa hesabu ya haraka haraka, kwa kutofanya kazi kuanzia saa tano ile mpaka muda uliopaswa kufanywa zimepotea kama milioni thelathini na tatu. Zimepotea kwa sababu mmoja wa Wabunge alitaka kuonesha namna anavyoweza kusoma Kanuni. Ungeweza kuonesha unavyosoma Kanuni, lakini ukawaacha Watanzania salama kwa kutotumia hela yao vibaya. Watanzania wanatarajia matokeo, lakini Wabunge wenzangu wa CCM na mimi nakuja kwenu. Tuna kazi ya kuisimamia Serikali, nje ya Bunge kwenye vikao vyetu na tuna kazi ya kuisimamia Serikali hapa ndani. Kilichotokea Ijumaa na yaliyotaka kutokea leo ni dalili kwamba kazi yetu Wabunge wa CCM hatujaifanya kwa kikamilifu. Huo ndio utangulizi kwa Wabunge wa CCM na Wabunge wa Vyama vya Upinzani. Watanzania wanatarajia matokeo, hawali Kanuni, hawali Sheria. Nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kuchangia Mpango wa Maendeleo, napenda kuwa na kipaumbele kimoja ambacho ni mtambuka. Kipengele ambacho ni mtambuka, kwangu ni namna gani jitihada zetu za kukuza uchumi zinaendana na maendeleo ya uchumi. Ni namna gani chochote tulichokiandika kwenye mipango hii kinakwenda kugusa maisha ya mwananchi wa kawaida. Tukijenga reli, tukazungumzia barabara, tukazungumza yote hayo, kama hayagusi maisha ya mwananchi wa kawaida, Watanzania hawatuelewa, tutakuwa tunaimba wimbo wa kila siku ambao hauna tija kwao, wakati wao kazi yao ni kuona maisha yao yanabadilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mifano, ukurasa wa 27 wa hiki kitabu cha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo unazungumzia namna ya kufunganisha maendeleo ya viwanda na maendeleo ya watu. Wanaonesha dalili hizo kwamba wanataka kusema hivyo, lakini ukienda kwenye maandishi kwa ndani, kwenye maudhui yenyewe, maeneo mengi huoni namna ambavyo Mpango huu unakwenda kugusa maisha ya mtu wa chini kabisa, nitatoa mifano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara, tumezungumza barabara, lakini utaona hapa tunazungumza barabara kubwa tu; za Mikoa, barabara za Wilaya, lakini ndugu zangu nikumbushe kitu kimoja. Barabara kubwa ya lami ina maana, lakini kama kule kijijini anakoishi mwanandhi, ndani Kijiji cha Kalenge, Kijiji cha Kitwazi hakufikiki hata kwa baiskeli, hata kwa pikipiki, maana ya barabara kubwa inapungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetarajia tuone namna gani sasa tunaweza kuweka mipango ya kushuka chini. Wakati tunajenga barabara kuu zinazotuunganisha na mikoa umefika wakati sasa hata barabara zile zinazotoka (feeder roads) zinazokuja kukutana na barabara hizo ionekane wazi kabisa kwenye mpango kwamba sasa mwelekeo wetu ni kwenda kugusa mawasiliano ya barabara kwa mwananchi aliye kijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu, ukiangalia kwenye elimu hapa kwenye utekelezaji na kwenye vipaumbele, utaona tunaongelea maabara, madarasa, lakini mwalimu tunasahau kwamba ndiye mfanyakazi wa umma wa nchi hii ambaye anafahamika anapofanya kazi, lakini hafahamiki anaishi wapi. Hatuzungumzii nyumba za walimu, hatuweki mkakati nyumba za walimu miaka nenda rudi, tunazungumza mambo ya maabara. Ni mazuri, lakini ukipita kwa mwalimu utakuwa umegusa mengine yote kwa upana na kwa namna ya kwenda kubadilisha maisha ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye barabara, nimeshangaa sana kwamba pamoja na kwamba nimezungumzia habari ya feeder roads, nashangaa sana kuona kwamba siioni barabara ya kutoka Bwanga kwenda Kalebezo, barabara inayounganisha Mkoa wa Geita na Mkoa wa Kagera na nchi jirani ya Rwanda; barabara ambayo inakwenda kwenye Wilaya mama ya Rais anayeongoza nchi hii. Alikuwa mgombea wa Ubunge mara mbili pale Bihalamuro, lakini Mikoa hii ya Geita na Kagera kama haitaunganishwa na nchi jirani kwa kiwango kinachostahili tunaua biashara pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, afya, unaona pale kwenye utekelezaji wanaongelea tu hospitali za rufaa, ni vizuri kabisa. Hata hivyo, hospitali za rufaa bila kuweka nguvu kwenye zahanati na vituo vya afya hatutagusa maisha ya watu. Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili ya Dar es Salaam au ya Bugando ni muhimu iwepo lakini haina maana kama mtu hawezi hata kupata mahali pa kupata huduma ya kwanza ili aambiwe nenda rufaa. Ni lazima mpango huu ujikite kwenye zahanati na vituo vya afya kwamba sasa tunakwenda kuwagusa ili wakishindwa kutibiwa pale ndipo waende kwenye hospitali kuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujumbe wangu ni kwamba, mipango yote tunayoiweka tuwe na kipaumbele mtambuka ambacho kinasema chochote tunachokifanya lazima kionekane wazi kwamba kinakwenda kugusa maisha ya mtu wa chini, vinginevyo maana yake inapungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nawaombea kila la kheri Waheshimiwa Wabunge wa CCM tuisimamie Serikali, lakini na Wabunge wa Upinzani tuibane Serikali kwa namna ambayo inaleta tija kwa wananchi. Nawashukuru sana. (Makofi)