Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia katika hoja hizi zilizokuwa mbele yetu. Pamoja na mambo mazuri na ushauri mzuri ulitolewa na Kamati uliowasilishwa na Mwenyekiti, ningependa niendelee kuzungumzia masuala mawili, jambo la kwanza, suala la UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejitahidi sana kama Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Samia katika kupambana na masuala ya UKIMWI. Afua za UKIMWI zimeendelea kupatikana, lakini ripoti ya Kamati na takwimu za Serikali zinaonesha kwamba, vijana hasa walio kati ya miaka 15 na miaka 24 ndio walioathirika zaidi na maradhi haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana 28,800 kwa mwaka, tena vijana hao ni kati ya miaka 15 na miaka 24, ndio ambao wanaongoza kwa kuathirika. Sasa mimi ningependa nishauri nini pamoja na haya; ningetamani sana Serikali yetu pamoja na Watanzania wote turejeshe nguvu ya kupambana na masuala ya UKIMWI katika ngazi ya familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ngazi ya familia hatuzungumzi sana uwazi kuhusiana na namna ambavyo UKIMWI unaweza kuambukizwa. Ndio maana tunazungumza sana katika kuhakikisha watu wetu hawapati virusi vya UKIMWI kwenye familia kwa kuwashauri wasitende vitendo vile ambavyo vinasababisha kuambikiwa kwa UKIMWI. Moja ya njia kubwa ya kupata virusi vya UKIMWI ni kutenda ngono isiyokuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dini zote, dini ya Kiislamu, ngono kabla ya wakati ama ngono nje ya ndoa ni dhambi, Dini ya Kikristo, sina mashaka na dini zote. Ngazi ya familia tumekuwa tunawakataza sana watoto wetu kushiriki vitendo vya ngono kwa ku-refer tu maelekezo yale yaliyotoka katika vitabu vyetu vitukufu, lakini shetani yupo kwa ajili ya watu wema. Sasa hawa vijana wetu ambao tunawaambia kwamba, msishiriki ngono, mkishiriki ngono mtapata dhambi tu, shetani yupo kwa ajili yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nadhani katika ngazi ya familia sasa tuwe wawazi kidogo. Tuwaeleze watoto wetu kwamba, ngono ni dhambi, lakini kwa sababu wengi wanashiriki tuwaambie basi siku ukishiriki ngono shiriki ukiwa umevaa condom, maana utakuwa umepata dhambi, lakini umelinda afya yako, kuliko akapata dhambi na asilinde afya yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaweza ikanusuru vijana wetu. Kwa siku moja vijana 80, kwa mwezi mmoja vijana 2,400, kwa mwaka mzima vijana 28,000 hali ni mbaya. Sasa tukiendelea kutumia dini peke yake katika kuwakataza vijana wasishiriki tukiamini itatosha peke yake kuwakinga, hapana haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, dini mpinzani wake mkubwa ni shetani. Jambo zuri sana kushiriki jambo la kimapenzi kwa mtu yeyote aliyekuwa juu ya miaka 18 kwa ridhaa yake sio kosa kwa mujibu wa sheria zetu. Sasa katika ngazi ya familia tuwe wawazi, tuwaambie ukitenda utapata dhambi, lakini shetani akikupitia ama kama ukimfuata shetani halafu mkaenda mkatenda, vaa mpira ili kuhakikisha kwamba, hujiambukizi virusi vya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia niongezee katika masuala ya maradhi yasiyoambukiza. Ningetamani niungane na Kamati katika kuishauri Serikali, umefika wakati sasa wa kuunda Tume Maalum ya Kupambana na Maradhi Yasiyoambukiza kama tulivyounda Tume Maalum ya Kupambana na UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote humu ndani na Watanzania karibu wote hakuna familia ambayo haijaathirika na maradhi yasiyoambukiza. Kama hakuna mtu mwenye maradhi ya moyo kuna mwenye maradhi ya kisukari, kuna mwenye uzito uliopitiliza. Sasa tuishauri Serikali ione sababu ya kuunda tume maalum kupambana na maradhi haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maradhi yasiyoambukiza sio tu ni hatari, lakini ndio maradhi ghali zaidi kuyatibu katika familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja hii. (Makofi)