Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, naona jina langu linakupa shida kidogo naitwa Edward Franz Mwalongo, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini. (Makofi)
Kwanza kabisa naomba nianze kwa kuwapongeza Mawaziri, Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini naomba nikiri mbele ya Bunge lako walinitunukia nishani ya mtetezi wa watoto wa kike na Waziri wa Afya alitangaza mbele ya Bunge lako na tarehe 8 Machi, 2016 waliniita Dar es Salaam, wakanitunukia nishani ile. Nashukuru sana na naomba Wabunge wote watambue kwamba nishani ile nimepewa na ninayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, umesema tusiongelee habari ya zahanati vijijini, ni ngumu sana kutenganisha. Ni ngumu kwa sababu mazingira tunayotoka yana mahitaji hayo, lakini wananchi wetu wanategemea tuliseme hili katika Wizara ya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nianze na tatizo la watoto wenye uzito mdogo, japokuwa hali ni mbaya sana katika Halmashauri zetu na umesema tusiseme lakini tunaomba tuseme. Halmashauri ya Mji wa Njombe ilitegemewa kuwa na wanaojifungua 190, lakini kwa sababu mazingira yametokea kwamba Halmashauri ile imezaa Halmashauri zingine na idadi ya watu imeongozeka, hospitali ile sasa imekuwa ya mkoa, imekuwa na wanaojifungua sasa wanafika 4,580.
Mheshimiwa Spika, katika 4,580 wanaozaliwa kama watoto wenye uzito mdogo ni 202, lakini wanaofariki sasa inatia huruma. Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii alisema tupige hesabu ya coaster. Kwa hiyo, pale Halmashauri ya Mji wa Njombe, tuna kosta zaidi ya tatu wanakufa kila mwaka watoto 82, ni jambo la kusikitisha sana. Nimeona kuna mpango wa Wizara wa kusaidia namna gani ya kuokoa maisha ya watoto hawa. Naomba Waziri atapokuwa anapanga mambo yake, atukumbuke Njombe kwa ajili ya kuokoa watoto wanaozaliwa na uzito mdogo.
Mheshimiwa Spika, ukienda pale hospitali inasikitisha, kile chumba ambacho kinatumika kutunzia wale watoto hakijulikani kilikuwa ni store au kilikuwa ni nini na hali ya hewa ya Njombe ni baridi sana, vifaa vyenyewe ni duni na pamoja na wataalam nimesoma kwenye kitabu cha Waziri cha hotuba yake anasema Njombe kuna mtaalam mmoja. Mtaalam mmoja kwa kweli kuhudumia watoto 82 kwa mwaka, hiyo shughuli ni pevu kweli kweli. Kwa hiyo, naomba Wizara itakapokuwa inafanya majumuisho itoe angalau maneno ya imani na maneno ya kuwafanya Wananjombe waone kwamba, Serikali yao imewakumbuka.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine nirudie tena masuala ya afya ya mtoto wa kike. Mtoto wa kike ndiye mama wa kesho, harakati nyingi sana zinamwangalia mama, kwamba mama akijifungua, mama anapata matatizo, lakini haziangalii mtoto wa kike kwa sababu mtoto wa kike akiwa na afya bora ndiyo mama wa kesho mwenye afya bora. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa mimi nimefarijika sana jinsi akinamama walivyoichukua ajenda ya kusaidia watoto wa kike kupata stahiki zao, kupata dhana za kujisitiri. Sasa cha msingi na kikubwa tuone tunafanyaje, sawa Serikali imeshapata taarifa na yenyewe inajitahidi, lakini baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameanza kushauri jinsi gani Serikali ifanye.
Mheshimiwa Spika, Mbunge mmoja jana alishauri kwenye vyuo kwamba mkopo unapokuwa ni mkopo kwa mtoto wa kike basi uongezewe. Gharama ya ile bidhaa wala sio kubwa kwa chini kabisa ni shilingi 20,000 kwa mwaka, kwa chini kabisa. Ni shilingi 1,500 kwa mwezi. Kwa hiyo, naungana na Mbunge yule kwamba kwenye mikopo ya shule, basi tuangalie kwamba watoto wale wa kike waweze kuongozewa hicho kiwango.
Mheshimiwa Spika, nimeangalia kwenye kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba Bima ya Afya wanataka kujitathmini na bima ya afya wana bima ya afya kwa watoto wa shule. Mtoto mmoja wa shule bima yake ya afya ni shilingi 50,400. Tuombe sasa basi watakapokuwa wanajitathmini bima ya afya, kwa mtoto wa kike mwanafunzi ihusishe bidhaa hiyo, hayo ndiyo matunda ya uhuru na hayo ndiyo matunda ya ustaarabu kwamba sasa tunaendelea, katika bima ya afya kuna package hii ya mtoto wa kike, lakini vilevile kama nilivyosema huko juu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, suala lingine ni tatizo la wauguzi. Kuna shida kubwa sana ya wauguzi hospitali nyingi hazina wahudumu wa kutosha, lakini Wizara inasema ina mpango wa kuboresha vyuo na kadhalika. Ningependa kushauri kwa ziada kwamba hebu tuone sasa, hebu tushuke chini, tunayo Bodi yetu ya Mikopo, Bodi ile imeng‟ang‟ana tu haifanyi hata utafiti, inakopesha tu watu wa university, kule university wanaosoma course nyingine hazina hata ajira.
Mheshimiwa Spika, mkopeshaji mwingine yeyote kwa mfano mkopeshaji wa kawaida, anapomkopesha mtu anaangalia jinsi ya kulipa. Leo hii Bodi ya Mikopo inahangaika kudai madeni ya wanafunzi ambao walisoma siku za nyuma, hapa kuna watu wanasoma vyuo vya afya, ajira Serikalini ipo. Bodi ya Mikopo basi ishuke chini, kama ni sheria basi waielete humu ndani tuibadilishe. Ikopeshe basi kwa kuanzia tu wanaosoma vyuo vya afya ili kusudi vijana hawa wanaosoma vyuo vya afya, wasome vizuri, wasome haraka na Serikali iwaajiri waweze kulipa hiyo mikopo.
Mheshimiwa Spika, liko suala la Bima ya Afya, naomba nipate ufafanuzi kwamba jana hapa Bima ya Afya imeshambuliwa kweli kweli. Ninavyofahamu kazi ya bima ni kufidia gharama, bima sio kazi yake kununua dawa. Ina maana kwamba, katika ile hospitali anatakiwa awepo mtoa dawa ili kusudi bima ifidie ile gharama.
Mheshimiwa Spika, niwaombe sasa Bima ya Afya na wenyewe wawe watafiti. Wamekubali kimsingi kwamba usipopata dawa hospitali utapata dawa kwenye duka. Hebu maduka yale waliyoingia nayo makubaliano yawepo hospitali pale pale ili kusudi mtu asiondoke kutoka pale hospitali kwenda sehemu za mjini kutafuta dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hii itawasaidia wahudumu wa afya wafanye kazi kwa amani na itawasaidia wateja wao waweze kupata huduma vizuri kwa sababu Bima ya Afya wenyewe wanaonekana kwamba, ndio wahalifu na ndio wanyang‟anya fedha za wananchi kwa sababu wamepokea fedha na huduma haikupatikana, lakini sasa kwa kuwa bima ya afya wana-package ya kukopesha vifaa vya afya, wana-package ya kukopesha ujenzi wa zahanati na nini, waone sasa kama inawezekana, wakopeshe hata Halmashauri sasa package ya dawa, ili kusudi sasa Halmashauri ziweze kutoa zile dawa ili wao kama bima wafanye kazi yao vizuri.
Mheshimiwa Spika, liko suala la Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi. Kwa mtazamo wangu naona kwamba vyuo hivi sasa kwa kweli sioni kama kuna ulazima wa kuendelea kuwa Wizara ya Afya, tuvipeleke VETA ili kusudi viweze kuhudumiwa vizuri zaidi. Vyuo vile vina hali mbaya, havina vifaa vya kazi, havina wataalam, pale Njombe tuna Chuo cha Maendeleo ya Wananchi, nakumbuka Mkuu wa Chuo aliyestaafu alikuwa ni Mwalimu wa Kiswahili.
Mheshimiwa Spika, pia pale kwenye Halmashauri ya Wanging‟ombe kuna Chuo cha Wananchi Urembwe, Mkuu wa Chuo aliyepo pale ni Mwalimu wa Kifaransa. Mimi kama fundi sielewi kabisa kwamba inakuwaje watu hawa wanakuwa ndiyo wakuu wa vyuo vya taaluma kama hizo, lakini je kuna ulazima wa kuendelea kuwa na vyuo hivi katika Wizara ya Afya? Kama ni sheria basi wailete tuibadilishe, vihamie VETA na VETA isimamie. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa utaratibu wa kawaida vile vyuo ukivipeleka VETA, VETA hawataaka kuvipokea kwa sababu vina hali mbaya mno. Kwa hiyo niombe Wizara ilitathmini hilo na ione, isiendelee kubeba mzigo ambao haubebeki, tunayo VETA ambayo ni mamlaka inayoshughulika na mafunzo ya ufundi study, itaboresha vile vyuo na Serikali itasaidia kuboresha vile vyuo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia naomba nitoe darasa kidogo. Jana hapa kuna Mheshimiwa Mbunge mmoja alisema yeye ni muhanga wa bima ya afya. Kiswahili ni sehemu ya bidhaa tuliyonayo kama Watanzania, neno muhanga linatumika kimakosa, muhanga ni kujitolea. Sasa wewe huwezi kujitolea ukawa muathirika wa bima ya afya na niwaombe hata waandishi wa habari wapo, wasaidie jamani neno muhanga ni kujitolea. Watu wengine wanakosea wanasema wahanga wa ajali, wahanga wa mafuriko; hakuna muhanga wa ajali, wala muhanga wa mafuriko. Hawa wote ni waathirika. Waathirika wa mafuriko, waathirika wa ajali na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo niseme nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba niokoe muda.