Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuja kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata jumla ya wachangiaji 13 kwenye hoja yetu na niwashukuru sana wote waliochangia kwa umakini mkubwa na ufasaha mkubwa kiasi kwamba hoja imeeleweka vizuri kwa wote na imeonesha ufanisi mkubwa. Kipekee niwashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri Mheshimiwa Damas Ndumbaro na Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa majibu ya mwisho hapa ambayo yamezidi kuweka sawa sawa hoja nzima na kujibu zile hoja ambazo Wabunge wamezionesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapochambua sheria hizi ndogo tunachoweza kusema hapa ni kwamba tunaweka mazingira safi ya utawala bora, kama alivyosema mmoja ya wachangiaji Sheria Ndogo hizi zinawahusu sana wananchi wote siku kwa siku, ni sheria kama sheria nyingine zina nguvu sawa na sheria nyingine na niseme labda wakati mwingine kuzidi sheria nyingine, kwa sababu ziko huko chini kwenye grass root watu walipo na zinatumika kila siku iwe kwenye usafi wa mazingira kwenye kutunza miti na mazingira kwa ujumla uvuvi boda boda yaani ndiyo zinazohusika hasa katika maisha ya kila siku ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hizi zina nguvu sana kwa sababu zinatoa faini zinatoa vifungo kwenda jela kwa fidia ndogo unaweza kwenda jela, zinaweka mazuio na mipaka mbalimbali, zinahalalisha mambo mbalimbali na kuharamisha mambo mbalimbali kwa hiyo zina nguvu nyingi kama sheria nyengine za nchi, hakuna tofauti kwamba ile neno kwamba Sheria Ndogo basi ni Sheria Ndogo siyo ndogo ni sheria zenye nguvu kama sheria nyengine.

Kwa hiyo, zikitungwa hovyo hovyo zinaathiri sana maisha ya watu ya kila siku na tunayopitia kila siku hivyo inabidi zitungwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba inatoa maelekezo mbalimabli na mamlaka mbalimbali sheria zitungwe vipi, kwa hiyo siyo sahihi kwa Sheria Ndogo kuja na mazingira ambayo yanakinzana na Katiba. Kwa mfano, amesema mchangiaji mmoja hapa Mheshimiwa mmoja amesema Katiba inatoa haki na wajibu wa kufanya kazi kwa mtu yoyote awe kampuni awe mtu binafsi, lakini wanasema kwamba ukitaka kufanya biashara ya samaki sharti uwe kampuni sasa hii inakiuka Katiba, siyo sahihi kuwepo na lazima ishughulikiwe na ifanyiwe masahihisho. Mfano mwingine anasema Mhifadhi wa Misitu anaweza kusitisha kibali cha kushughulika na mazao ya misitu na hana kikomo hana ukomo inaweza kuwa miaka 10 miaka 20 yaani daima dumu anakufutia tu kibali, sasa hii siyo sawa inakinzana na masharti ya Katiba na Sheria nyingine zinazohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongea Wabunge wengi kuhusu Sheria ya Ombaomba katika Wilaya ya Chunya, wameeleza vizuri ni sheria ambayo kwa kweli ni ya kibaguzi, unambagua mtu kwa ulemavu siyo jambo zuri, unamwambia apelekwe Mkoa wa kwao akabidhiwe kwa RAS na RAS ampeleke kwa RAS wa kwao, sasa RAS huyu ampeleke wapi na kwao ni wapi ameuliza Mheshimiwa mmoja. Je, ina maana Chunya pale hakuna raia ambao ni ombaomba ambao wanafanya kazi za ombaomba pale pale, kwa hiyo Sheria hii ni ya kibaguzi na haifai kuendelea kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Tanganyika wamesema lina kina kirefu zaidi ya mita 1,000 lakini samaki anaweza kuishi kwenye mita 150, unaporuhusu tu mita 20 ndiyo wavue hizi nyingine mita 130 avue nani? Samaki kama walivyosema hazina mipaka znaweza kwenda Congo zinawaza kwenda nchi nyingine jirani na watu wakafaidi kule na sisi tunajinyima uchumi ambao ni mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema Waheshimiwa Wabunge kwamba inasikitisha kwamba sheria hizi zinatumika huko kabla kuja Bungeni, kwa kweli hili ni jambo la msingi sana, bahati mbaya ni nyingi sana, ni nyingi kweli kwa maelfu kwa maelfu sasa ukisema zije kabla zitakuwa hazitumiki zitachukua muda mrefu sana kutumia kwa huko kwa wananchi, lakini kwa kweli ni jambo zuri la kufikirika ni la kufikirisha kwa sababu zikitungwa sheria mbovu anaelaumiwa ni Bunge nani anaelaumiwa, mtunga sheria ni mmoja ni Bunge wale wengine wote wamekasimiwa delegated awe Mkurugenzi awe ni shirika gani amekasimiwa na Bunge, Bunge ndiyo mwenye lawama kama sheria hiyo itaonekana kwamba ina kasoro au mapungufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapomruhusu mtu ambae ni interested part ana maslahi binafsi kwenye sheria fulani, halafu hashiriki humo tunafahamu kwa mfano katika Halmashauri Madiwani hawaruhusiwi kushiriki zabuni za ujenzi wa barabara mle za ndani kwa sababu wana maslahi binafsi, sasa unaporuhusu hawa wasimamizi wa mazingira washiriki kwenye ile kazi ya kusimamia mazingira ina maana umeruhusu conflict of interest mgongano wa maslahi, haiwezekani lazima sheria kama hiyo ifanyiwe kazi ya kurekebishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa hapa na tumeiona kwenye uchambuzi wetu, uvuvi katika Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika, mwenye chombo ana leseni mvuvi ana leseni, chombo chenyewe kina leseni na huyu mvuvi akihama kazi kwa mwenye chombo akaenda chombo kingine leseni ile inaisha nguvu haina kazi tena, akienda kwa chombo kingine alipie leseni nyingine na anaelipa ni mwenye chombo, sasa ni mateso ambayo tunawapa wenye vyombo na kuwaongezea gharama ambazo hazina maslahi wala hazina faida kwa nchi yetu, tunawatesa, tunawakosesha mapato tunawakosesha kazi na siyo jambo ambalo lina busara yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makosa ya uchapaji unapochapa sheria ovyo ovyo unainyima uhalali wa sheria, mkienda Mahakamani Wanasheria utaangushwa chini mara moja, kwa sababu watakwambia hii umeitungia chini ya sheria gani? uliyoweka umekosea! Kwa hiyo lazima uwe makini unapoandika sheria iwe ndogo iwe kubwa isikinzane na Sheria Mama au sheria nyingine kubwa au ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema Mheshimiwa mmoja hapa sheria Kubwa inaweza ikawa inasema faini ni Shilingi Laki Moja, Sheria Ndogo inasema faini Shilingi Laki Moja na Hamsini, hii ni kinyume kabisa na utaratibu wa utungaji wa sheria na haifai kuwepo, ni lazima hiyo ifutwe mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema na walivyosema Wabunge wengine sheria hizi zinahusu maisha ya wananchi wetu, wananchi wenzetu ya siku hadi siku, lengo lake ni kukuza utawala wa sheria, utulivu, amani na ustawi na maeneleo na si kinyume chake, siyo vinginevyo, amesema Mbunge mmoja kutoka Kilimanjaro pale nyumba ya mungu unasema samaki wasivuliwe chini ya nchi tatu, amesema kwa miaka 20 hao samaki hawajawahi kuwepo, sasa unashangaa unajiuliza hawa waliotunga sheria hii hawajui mambo haya walitunga kwa sababu gani? Unasema nchi tatu ndiyo kiwango cha chini lakini sasa hawajawahi kufika kwa miaka 20, kwa hiyo unakusudia nini unapotunga sheria ya namna hiyo na ili iwe nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unazuia mtu kukata mti ambao aliupanda mwenyewe, sasa unashangaa kapanda mti mwenyewe ili aufaidi apate matunda yake unamzuia kuukata umekusudia nini? Kwa hiyo badala ya kusaidia watu kuwahimiza, hawatungi sheria ya kusema pandeni miti au boresha mazingira wanasema usikate mti ambao umepanda mwenyewe, kwa hiyo inazidi kuleta shida katika usimamizi wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rai yetu Kamati ya Sheria Ndogo kwamba sheria mbovu iwe Sheria Ndogo hasa hizi sheria ambazo sisi tunashughulika nazo zisiwe Sheria katika sheria za nchi hii zifutwe na zirekebishwe pale ambapo inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninalishukuru sana Bunge lako Tukufu kwa kuchangia na kwa Wabunge kuchangia kwa umakini mkubwa na kwa weledi mkubwa sana na kwa ufanisi wa hali ya juu sana, michango yao imekuwa ya manufaa makubwa na imesaidia kuweka jambo hili vizuri na hoja imezidi kueleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.