Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie fursa hii kukushukuru wewe mwenyewe, Naibu Spika, Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Bunge ya Bajeti pamoja na wajumbe wa Kamati lakini pamoja na Wabunge wote waliochangia katika hoja hii ya leo ambayo nahitimisha muda huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote baada ya hayo nitamke kwamba hoja zote zilizotolewa kuanzia hoja zilizotolewa na Kamati, hoja zilizotolewa na Wabunge, hoja zilizotolewa na Mawaziri, tumezipokea sisi kama Wizara na tuwaahidi kwamba zitafanyiwa kazi na tutakapokuja na draft nyingine ya Mpango ambao utakuja kwa hatua nyingine tutakuwa tumejumuisha na maoni hayo ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo nikuombe na Waheshimiwa Wabunge watuamini na hatutaweza kuiongelea hoja moja baada nyingine kwa sababu hoja hizo zilizotolewa ni nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo machache tu ambayo nitaomba uridhie niyagusie ni yale ambayo yanahitaji ufafanuzi yale ambayo tumepewa maoni na tumepewa ushauri tutachukua na kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na eneo hili hili ambalo limejadiliwa muda siyo mrefu ambalo lilikuwa linaongelea masuala ya madeni kwa wastaafu. Kwanza kwa mtu akisema Serikali haina nia njema na madeni haya ya wastaafu itakuwa ni bahati mbaya sana na atakuwa hata hajazingatia kwamba hata hilo deni kiini chake kilitoka wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, madeni haya ambayo tunaongelea leo mengine ilikuwa ni hiyari ya Serikali tu kwamba tunaenda kuwalipia watumishi wetu na yalichukuliwa Serikali ilikubali kubeba mzigo ili iwalipie watumishi wake. Katika hilo si kwamba tangu muda ule hamna kinachofanyika Serikali imeshafanya ni vile kwamba kulikuwepo na accumulation kubwa lakini Serikali imeshafanya na imefanya kwa kiwango kikubwa tu ambacho kinastahili kupongezwa na ukichukuliwa jinsi ambavyo Serikali inafanya inatakiwa iweke matumaini kwamba hili ni jambo ambalo linaenda kukamilika na katika suala la muda tutaweza kufika katika hatua nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika siku ambazo si nyingi sana tayari PSSF walishapewa bilioni 500 kwa ajili ya jambo hilo hilo na NSSF walishapewa bilioni 100 na katika kipindi cha ndani ya miezi mitatu kwenda minne iliyopita tuliongezea bilioni 50 nyingine kwa ajili ya masuala hayo hayo ya kuwalipa wazee. Na hata hii tuliyosema tunafanya noncash bond labda hii taaluma na yenyewe labda iwe na shida watu hawajui hii ni float ya kwanza tume-float ya kwanza kwa kiwango hicho na siyo ya mwisho tuna float ya kwanza kwa kiwango hicho na siyo ya mwisho. Tuna float ya kwanza tunaitekeleza halafu tuna-assess imefanyikaje tuna-assess deni halafu baada ya hapo tunaendelea na utekelezaji ule ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wengine wanaolalamika sana ni vile tu Bunge lako si kiwanja cha utani ingekuwa kiwanja cha utani hawa wangekuwa watani zangu ningeweza kukwambia wao wanadaiwa nini hata wao binafsi waone suala la madeni huwa likoje na hata sasa wanatamani uwaruhusu hata gratuity. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapoongelea haya mambo kwa mwingine ambaye anafanya jukumu kubwa tusiwe tunasahau undani wa mzigo wenyewe unavyokuwa Serikali imeshafanya jambo kubwa na itaendelea kufanya jambo kubwa na katika kipindi ambacho tayari Serikali imechukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hatua ambazo zimewabadilishia maisha wazee hao ni jambo kubwa ambalo limefanyika ambalo halipaswi kubezwa ilikuwa ikitokea Bunge inaendelea kama hivi unakuta wazee wengine wako misikitini wengine wako makanisani wengine wako tu wamehifadhiwa mahali hivi. Lakini baada ya utaratibu huu wa kuanza kutoa hizo fedha tena kwa mtiririko tena kwa ukaribu karibu jambo hili limeanza kubadilika pakubwa na tunaamini baada ya hatua hii kubwa ambayo Mheshimiwa Waziri anaifanya kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kukamilisha masuala ya kikokotoo tutaongeza zaidi kasi na tutaenda kulifanyia jambo hili ambalo lilikuwa tatizo kuwa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine hiki kinatajwa tu kwamba CAG amesema deni ni trilioni 19 hii ni namba na watu wale wale CAG yule yule aliposema madeni yanayodaiwa na TRA ni trilioni 360 walisema hii haiwezekani kwamba hizi ni namba tu CAG kazitaja tu kwenye hii hapa namba hii hii wanaona hiyo ndiyo namba tu. Lakini niwaambieni kila kitu kinachoitwa deni yanafanyika verification na yale ambayo yameshakuwa verified yanafanywa malipo na hilo ni jambo ambalo litafanyika na litakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningeomba nilisemee kwa uzito mkubwa unaostahili ni hili ambalo na Mheshimiwa Naibu Waziri ameshalielezea, sitaelezea katika angle ambayo tayari ameshafafanua hili jambo la deni la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo la deni la Taifa tuna orodha ndefu sana ya miradi ambayo imeshafanyika na niwaombe watanzania hasa hasa sisi Wabunge ambao ni viongozi tusianzie mbali sana twendeni tu tuanzie wakati deni la Taifa liko katika kiwango tuseme cha trilioni 10 tuanzie hapo hapo halafu tuanze kuangalia katika mwaka 1995 tuseme tuangalie katika mwaka 1995 deni lilikuwaje halafu tuangalie pia na miradi ambayo ililetwa na fedha zilizokopwa kipi tulitakiwa tukifanyie uamuzi katika mwaka huo ambapo tunaongelea deni la Taifa likiwa dogo, hatukuwa na mikoa ambayo imeunganishwa kwa barabara za lami yaani kutoka Singida kuja Dodoma hapa tulikuwa tunahitaji siku nzima. Kutoka Singida kwenda Arusha tulikuwa tunahitaji siku nzima, kutoka Mwanza kwenda Dar es Salaam tulikuwa na option ya kupita nchi mbili kutoka Kagera kwenda Dar es Salaam tupite nchi mbili, kutoka Dar es Salaam kwenda Lindi tulikuwa tunahitaji wiki kabisa. Kutoka Dodoma hapa walioingia vipindi viwili vitatu kutoka Dodoma hapa kwenda Isimani hapa ilikuwa lazima uende kwanza Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wengine ni wadogo sana hawajui haya yaani ukitaka kusafiri begi kwanza mabasi yenyewe begi lilikuwa linakaa kwenye carrier halafu mnapofika yeye aliyemsafiri na yule utingo wote hamtofautiani ndivyo ilivyokuwa sasa analysis iliyofanyika ni je, tuchukue makusanyo ya fedha tujenge barabara zetu tufungue uchumi halafu tukishafungua uchumi ule utuletee fedha tuendelee kulipa madeni ndiyo uamuzi uliofanyika. (Makofi)

MWENYEKITI: Halafu Mheshimiwa Waziri yale mabasi yalikuwa yameandikwa ukiingia mle ndani kwamba kila abiria tunza mzigo wako wa ndani ule wa kwenye carrier utingo atajua endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndivyo ilivyokuwa kwa hiyo ukatakiwa ufanyike uamuzi wa makusudi tu kwamba je tuendelee na hali kama hii hii halafu na deni letu liwe dogo au tuchukue fedha tutengeneze miundombinu tufungue nchi yetu halafu miundombinu hiyo ituletee fedha tulipe deni tunalokopa. Ndiyo uamuzi uliofanyika sasa hivi baada ya njia kuwa zimeshafunguliwa sana karibu kila eneo na hii nimeongelea tu barabara lakini ni maeneo mengine mengi kwenye umeme hivyo hivyo sehemu ya robo ya nchi ndiyo ilikuwa na umeme kwingine kote ilikuwa giza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo kwenye umeme hivyo hivyo na sekta zingine taja na sekta taja kwenye afya taja kwingine kote uamuzi ukafanywa kwamba je, tubakie na deni dogo halafu na miundombinu yetu yote hafifu au tukope tufungue miundombinu halafu baada ya hapo tulipe? Ndicho kilichofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna orodha ya miradi inaelekea karibu 1000 ambayo imejengwa siwezi hata kuanza kuutaja mmoja mmoja lakini kwa sababu sisi ni viongozi kila mmoja aanze kupekua mmoja mmoja ambao ana maslahi ya kutaka kufahamu aone umejengwa kwa kiwango gani umejengwa kwa financing gani? Imefungua nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata masuala tu ya umeme wenyewe umeme si nguzo za umeme, umeme ni uzalishaji wenyewe wa umeme imefanyika njia hizo hizo mpaka sasa hivi watu karibu nchi nzima walishazoea masuala ya umeme watu karibu nchi nzima walishazoea masuala ya mawasiliano ya simu hayo yote ni analysis za kufanya uamuzi halafu likafanyika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani wakati tunasoma ilikuwa umeme unakatika ukiwaka mnashangilia kama goli la simba maana yake simba siku hizi ikifunga dakika zimeshaenda watu wanashangilia mpaka nyumbani. Watu wanashangilia kumbe umeme tu umerudi umeme. Kwa hiyo, tathmini ikafanyika uamuzi ukafanyika na madeni haya yameongezeka lakini pia miundombinu iliyojengwa na fedha hizo imeongezeka tusifanye tathmini ya deni tu kama vile tumebambikwa tufanyeni tathmini ya deni huku tukifanya na tathmini ya miradi ya fedha hizo ambazo zimefanywa kutokana na deni hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wengine wanaenda mbali zaidi hizo ndiyo cheap politics wanaenda wanasema Serikali ya Awamu ya Sita imeingia tu kwa miezi sita imeshakopa zaidi ya bilioni tisa. Jamani ndugu zangu hivi hata ibada hamfanyagi, hamuogopi hata Mungu? Mkopo wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Sita mkopo wa kwanza wa mama ni hii trilioni 1.3 ambayo imetoka IMF na kwa mazungumzo yanayoendelea utakuwa mkopo ambao una masharti nafuu kuliko mikopo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo mkopo wa kwanza na mpaka sasa Serikali ya Awamu ya Sita haijakopa mkopo wowote wenye masharti ya kibiashara bado haujakopa labda mkopo wa kwanza utakuwa wa kukamilisha loot ya tatu ya nne na ya tano. Sasa hata hilo ni jambo ambalo tunatakiwa tufanye tathmini tu je, tuache tu kufunga hiyo loot three, loot four na loot five? Kwa kuogopa deni? Au tupitishe bakuli maana yake hata Yanga tulishaacha kupitisha bakuli tunachukua mzigo mkubwa tunamalizia loot hiyo hapo tunaanza inayoenda Kigoma tunaanza inayoenda Kalemi tunakamilisha zote tunafungua fursa za biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni miradi ya msingi ambayo unafanya analysis kama uchukue deni au uache ubaki umeufunga uchumi wako haya ni mambo ya msingi Serikali yetu haijawahi kukopa kwa ajiili ya kulipa mishahara wala kwa ajili ya kujaza mafuta kwenye magari inakopa kuweka miradi ya wananchi ambao wananchi wenyewe tumeshawatengenezea kiu kila mwananchi anataka jambo lifanyike zuri zaidi katika eneo lake na hii niwahakikishie watanzania tuko kwenye mwelekeo ambao ni sahihi na wengine walikuwa wanasema hata kwamba Serikali imetumia reserve zilizoachwa. Reserve zilizoachwa hazijaguswa na zimeongezeka sana sasa hivi tunaumiza vichwa ku-control mfumko wa bei kwa sababu pia fedha zinapokuwa nyingi sana inabidi muangalie na kwenye policy aspects za kuangalia mfumko wa bei ukoje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda mwaka 2015 reserve zilikuwa dollar bilioni 4.3 wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia wakati Serikali ya Awamu ya Tano inamaliza ilishaongeza reserve kutoka bilioni 4.3 kwenda bilioni 5.04. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Machi 2021 wakati Serikali ya Awamu ya Sita inaingia, tayari imeshapandisha kutoka bilioni 5.03 kwenda bilioni 6.4 hizo ndiyo reserve zetu tulizonazo ni zaidi ya miezi sita ya uagizaji wa bidhaa tuko juu kabisa mbali na kiwango kinachotakiwa katika standard za kimataifa. Na ukienda kwenye tathmini angalieni IMF wanatutathmini vipi, angalieni Benki ya Dunia inatutathmini vipi halafu ndiyo hapo muweze kuangalia ni kitu gani ambacho kinaweza kikaangaliwa ili uweze kutoa hoja kama mtu unataka kutoa hoja katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya ni mambo ambayo watu wanatakiwa wayafanyie tathmini fedha zingine za miradi mikubwa hii zingine zimetoka Awamu ya Tano zimeingia Awamu ya Sita zingine zilitoka Awamu ya Nne zikaingia Awamu ya Tano hatupaswi sana kuangalia tu mambo ya fedha tunatakiwa tuangalie fedha hizi zimefanya nini unajua ingekuwa jambo la msingi sana watu wangekuwa wanasema hii fedha hamjaitumia katika eneo ambalo linaleta manufaa. Hilo ndiyo jambo la msingi kuongelea ongelea fedha tu hii watani zangu hapa sijui ni akina nani unakuwa kama Wanyaturu wanaogopa kupanda karanga kwamba nalalaje ndani halafu karanga ilale nje kumbe unavyopanda karanga ndiyo utavuna nyingi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwekeze tunatakiwa tujadiliane kuhusu tumewekeza sahihi au si sahihi hiyo ndiyo itakuwa akili ya watu wenye maarifa ya kuwaza nchi inaelekea upande gani. Siyo kila siku watu wanawaza wanaangalia namba tu halafu na wengine wanawatisha wananchi wetu kwamba unajua zitaanza kugawanywa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat anatoa macho hapa, ahsante endelea Mheshimiwa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie fedha zilikowekezwa, na jambo lingine zuri zaidi na hata Mbunge wa Mtama Mheshimiwa Nape alitoa pendekezo, pendekezo hilo sisi tunachukua kama Wizara tutafanya tathmini halafu tuangalie kama tunaweza tukaongea na taasisi halafu tufanye refinancing tuangalie tufanye refinancing ni kitu ambacho watu huwa wanafanya. Unaweza ukakopa ulikuwa na mradi una uharaka ukakopa halafu masharti yakawa yako juu sana unaangalia kama unaweza ukapata refinancing kwa mfano kama hivi tunasema tumepata fedha hizi trilioni moja na zaidi zikawa hazina riba halafu grace period miaka 10 ukiwa na fedha nyingi za aina hiyo unaondoa zile ambazo ulikuwa na grace period ya miaka miwili na riba ya asilimia 9 halafu unakuwa na fiscal space ambayo unaweza ukatekeleza shughuli zingine za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo yanaweza yakaweka ahueni kwenye upande wa deni lakini pia ikatusaidia kuendelea ku-finance miradi ya maendeleo ambayo wananchi wetu wanahitaji kuendelea kuona maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amesema tutafungua mikoa yote ambayo bado haijamaliziwa kufunguka wapi huko Mpanda kwenda Kigoma kwenda Rukwa kwenda Tabora wapi huku Lindi maeneo yale ambayo yanauzalishaji mkubwa Mtwara yanauzalishaji mkubwa wa korosho lakini barabara hazifikiki wapi huku kwenye mbao na maeneo mengine huku Ruvuma maeneo mengine kule Manyara na mikoa mingine mingi kwenda Simiyu huko na maeneo mengine mengi Ifakara huku maeneo mengine yote yale ambayo yanatuletea uzalishaji mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amesema yaangaliwe yawekwe kwenye mpango ili tuweze kufungua uchumi unajua tunapofungua uchumi tunagusa mpaka kwenye kilimo, tukifungua barabara tunagusa mpaka kwenye uzalishaji upande wa kilimo haya yote tunaenda kuyaangalia ili yaweze kufanyika kuleta tija kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwa ajili ya muda niweze kuliongea na lenyewe Mheshimiwa Naibu Waziri ameshaliongelea upande mmoja nitaongelea upande mwingine ni upande wa kilimo. Eneo hili la kilimo na Waheshimiwa Wabunge tunakubaliana wote sisi hatupingani na mawazo ya Wabunge, lakini kitu kimoja tu tunachosema ambacho tumekuwa tukijadili sana na Wizara ya Kilimo na tunaendelea kuwa na uelewa wa pamoja ili tuweze kusonga mbele na tunaongelea kilimo kwa ile dhana pana ambayo inaweka na mifugo inaweka na uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, safari ya sekta hizi siyo fupi ni safari ndefu tu ambayo tumekubaliana tu kwamba tunaanza wapi katika huo mwelekeo wetu. Kati ya maeneo haya ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kesho ama keshokutwa nadhani hata sasa hivi tunavyoongea Mheshimiwa Naibu Waziri ameniambia kuna kazi ambazo zinaendelea lakini na Waziri tulikuwa tumekaa meza pale akasema anashughuli nyingine ambayo anatakiwa aifanye inayohusiana na masuala ya kilimo, lakini akasema angekuwepo humu Bungeni angetamani aseme neno moja tu ahaa amesharudi huyu hapa Waziri wa Kilimo. Aliniambia neno moja analotamani kusema yaani tofauti ya sasa na muda mwingine Wizara ya Kilimo, Wizara ya Kilimo sasa haijaomba fedha ikakosa na anatarajia kwamba mpaka anamaliza mwaka huenda akawa amepata asilimia 100 ya bajeti huyu hapa yupo amesema hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba inawezekana kwa mwaka huu sasa Wizara ya Kilimo ikawa na asilimia 100 ya bajeti tofauti na ilivyokuwa 12, 20, 13, 20. Hiyo ni hatua ya kwanza tumewapatia fedha hata kama ni kidogo zile walizoomba, lakini hatua ya pili tumesema tutatenga fedha kwa ajili ya mbegu. Maana yake Mheshimiwa Waziri amesema transformation anayotaka kufanya siyo tu ya kiutawala kwenye Wizara ya Kilimo anataka hasa kwenye sekta yenyewe. Kwa hiyo la kwanza ni mbegu na sisi tumesema tunavyoanza kutengeneza bajeti hii tuta- accommodate bajeti ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu tumeongea na Mheshimiwa Waziri tukasema kwenye umwagiliaji kuna angle mbili, angle ya kwanza tunaweza tukavuna maji, duniani kwote wanatumia pia umwagiliaji wa kuvuna maji. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu ameshanunua mitambo kwa ajili ya kuchimba mabwawa. Tumeongea na Waziri na ile Idara ya Umwagiliaji wafanye tathmini kwenye mitambo ile ya kuchimba mabwawa je, kwa bwawa la umwagiliaji ni mitambo gani bado inakosekana? Walete tathmini tuiongeze na hiyo, kwa sababu wakulima wetu wengine siyo wakulima wa ma-estate makubwa ni wakulima wa mashamba ya kawaida ambayo yanaweza wakatengeneza mabwawa ya umwagiliaji wakamwagalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo mifano ya maeneo ambayo watu wameweza kumwagilia na wakaweza kubadilisha maisha yao. Kwa hiyo hili ni jambo lingine ambalo Rais wetu ametuelekeza tukae na wenzetu tufanye tathimini na yale ambayo yatahitajika tutafanya hivyo ili umwagiliaji uweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umwagiliaji mwingine ni ule umwagiliaji mkubwa wa kuweka mabomba ya kutoa maji kutoka eneo la mbali kupeleka eneo lingine la umwagiliaji. Haya tumesema taasisi ile ya umwagiliaji wakae na Wizara ya Maji tutakapokuwa tunafanya miradi mingine mikubwa ya maji, tutakapokuwa tunatekeleza miradi mingine mikubwa ya maji labda kutoka Mto Ruvuma kwenda Ruvuma yenyewe kwenda mpaka Lindi na Mtwara au kutoka Tanganyika kwenda Katavi, kwenda mpaka Rukwa waangalie teknolojia za kisasa za kutengeneza miundombinu hiyo pawepo na lane zinazopeleka maji ya matumizi ya nyumbani, pawepo la lane zinazopeleka maji ya umwagiliaji. Tuone kama kuna namna ya engineering hiyo ambayo inaweza ikafanyika ambayo inaweza ikawa cost effective na ikatusaidia kuweza kutekeleza hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumesema tutayaangalia haya mazao ambayo ni mazao makubwa katika nchi yetu kuna mazao yalishawahi ku- peak mpaka worldwide yakawa yanajulikana ikafika mahali yakawa yameshukashuka tumesema tutayaangalia, tutaangalia pia refinancing yake, mifano imeshapatikana katika maeneo ambapo pembejeo zimeweza kuwa refinanced kutoka katika utaratibu wa ndani ya mazao yenyewe. Tumesema hayo yote tutayaangalia tuone ni namna gani tunaweza tukaweka utaratibu ambao utatusaidia katika uhakika wa masuala haya ya pembejeo na jambo hili ni jambo ambalo linawezekana na litawezekana kwa mazao yote hayo na tunatambua Bodi hizi zimekuwa na viporo viporo vingi hivyo hivyo na TFC yote haya tutakaa na wenzetu tuone ni namna gani tutafufua haya maeneo ili tuweze kuendelea na yaweze kupiga hatua kubwa zaidi na wakulima wetu na wananchi wetu waweze kupiga hatua kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya tunayoyasema kwenye upande wa kilimo nimesema ni hivyohivyo na sub- sectors zingine ambazo zinaangukia katika eneo hilo, tutafanya hivyo kwa mifugo, tutafanya hivyo kwa uvuvi kwa sababu ni sekta hizo kubwa ambazo zinabeba eneo kubwa la wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kufanya hii transformation kwenye hii sekta ya kilimo tutakuwa na risk mbili; risk ya kwanza sustaining kuendelea kupanda kwenye rating hizi za kipato cha kati, kipato cha kati cha chini, kipato cha kati cha juu itakuwa ni ngumu sana kwa sababu watu wenye eneo kubwa ambao wanatakiwa wafanyiwe hiyo tathimini ya kipato kwa mtu mmoja watakuwa bado wapo mbali na utaratibu wa kuweza kupata kipato kikubwa kwenye shughuli ambazo zinawaingizia kipato. Kwa hiyo tunalenga kufanikisha hili ili kipato cha mtu mmoja mmoja kiweze kupanda kwa sababu population iliyokubwa ipo eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tunalolenga katika eneo hili la kukuza hizi sekta tulizozitaja ni ili tuweze kukipeleka kizazi cha leo katika shughuli za uzalishaji. Kuna Mbunge mmoja alisema hamna utafiti ambao umeshafanyika kwenye hili eneo, niwahakikishie utafiti umeshafanyika majibu tunayo na siku si nyingi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu ama Waziri Mkuu mwenyewe atatoa tamko linalohusiana na matokeo ya utafiti wa eneo hilo. Kati ya maeneo ambayo yamekuwa na yanaajiri watu wengi tena ngazi hii ya vijana ni eneo hilo hilo ambalo mmoja wa msemaji alisema halijafanyiwa tathmini nani hilo hilo ambao linahusisha mpaka upande wa kilimo, upande wa vijana wanaojiajiri wamachinga na hilo ni eneo ambalo tutaliangalia vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo kitu kingine ambacho tunakilenga kwenye upande wa kilimo ni kwa ajili ya ajira, tunataka tupeleke hii generation ya kileo iweze kufanya shughuli hizo za kilimo, mifugo pamoja na uvuvi. Tusipo-transform hizi sekta hii generation ya kisasa haitaweza kufanya hizo shughuli. Katika maeneo mengi ambayo kilimo ama mifugo ama uvuvi unafanywa kwa zile traditional ways katika maeneo ambayo kilimo kinafanywa kwa njia ya zamani sana kizazi cha leo hakishiriki kwa asilimia kubwa katika hicho kilimo. Kwa hiyo, inabakia kama ngoma ya kienyeji hivi inafanywa na wazee wa zamani ndiyo wanaweza wakakuimbia ukaona kumbe hii ndiyo ngoma ya kabila letu. Kwa maana hiyo tuta-transform ili tupeleke kizazi cha leo hii shughuli ili tuweze kuwa World’s largest exporter wa zao fulani tunahitaji na kizazi cha leo kishiriki katika uzalishaji wa shughuli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo na kwa upande wa machinga taarifa njema inakuja hii ya utangulizi mmeshaipata na Mheshimiwa Rais anania njema sana kwenye jambo hili na yeyote ambaye atalifuatilia kwa umakini na baada ya muda fulani ataona kwamba Mheshimiwa Rais anataka awabadilishe wamachinga kutoka kwenye kutumikishwa wao wenyewe wapate mtaji waweze kusimama wafanye hizo shughuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ya sasa hivi walichokuwa wanafanya anatembea na bidhaa za watu kwa sababu hatuwezi tukawafikia hata tukitenga hizo asilimia ngapi ngapi hizo hatuwezi kuwafikia. Sasa tukiwa na uwezo wa kuwafikia, mmeona Dar es Salaam wameshaanza, maeneo mengine wameshaanza wanatengeneza SACCOS zao tunaamini wakishakuwa katika maeneo ambayo yatafikiwa wataweza kupata fedha kwenye SACCOS zao, wataweza kutembea na bidhaa zao, wataweza kuuza bidhaa zao na tunaendelea kuangalia na Waziri wa Ardhi yupo hapa, eneo moja ambalo tutaliangalia kwa umakini na Mheshimwa Rais ndivyo alivyoelekeza ni kuwaweka katika maeneo ambayo ni very strategic ili yule mtu aliyekuwa anaenda kwenye eneo lile ambalo ana-first target yake anavyomaliza hiyo first target yake asitake kusafiri kwenda mbali sana kwenda kumtafuta huyo mtu mwingine mwenye bidhaa ndogo aweze kumfikia na yeye hapo hapo, lakini kwenye utaratibu ambao umepangiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivi vitu vingine watu wengine unaweza ukadhania kwamba wao ndiyo wanawahurumia lakini kumbe wao ndiyo hawawahurumii hawa vijana wetu kuna maeneo mengine wanafanya hata katika mazingira sana lazima tuyabadilishe. Mimi nilipita eneo lingine mvua ikija yao, jua likija lao, lakini kama tunaenda tunaendelea tuwabadilishe kuzingatia tu wawe katika eneo ambalo haliathiri wao kufikika kwa wateja wao ambao wanawategemea katika kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kutambua michango ambayo Waheshimiwa Wabunge wameisema eneo lingine ambalo lilitajwa kwa kiwango kikubwa lilikuwa la riba ufafanuzi wake ni mrefu na niendelee kusema kwamba hayo ni maoni yametolewa sisi tutaendelea kukaa na wataalam wetu kuyafanyia kazi, lakini pia tutaendelea kuchukua hatua ambazo zitatupeleka kwenda kufanikisha riba hizo kuwa rafiki ili ziweze kuleta tija. Eneo hili la riba na lenyewe lipo trick kidogo, lakini kama ambavyo Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo akiwa Mwanza na ameendelea kutoa maelekezo akiwa ndani ya Serikali tunaamini kwamba tutalifanyia kazi na litaweza kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge kazi hii inayofanyika na kule tunakoelekea huu ni mpango ambao tunajadiliana, lakini pia tunajadiliana maeneo ambayo tumeyafanyia kazi. Hata hapa tulipotaja tumetaja machache tu, yale yote ninyi mlioyataja yapo na mengine sisi tumeyataja kwa maandishi yote tutaendelea kuyafanyia kazi na tutayaweka kwenye utaratibu wa kuyaboresha kwa maana ya kwenye Mpango, lakini pia tutaboresha kwa maana ya utekelezaji wake ili tuweze kuhakikisha kwamba mpango unaofuata unafanya kazi kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaenda pia kutekeleza miradi mikubwa moja mmetoka kumsikia Waziri wa Nishati, lakini ipo pia miradi mingine mikubwa ambayo tunategemea itaweza kutengeneza impact kubwa kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii mikubwa itakavyotekelezwa bomba la mafuta, LNG pamoja na miradi mingine hii ambayo ni mikubwa na ya kimkakati inayoendelea, yote hii itaendelea ku- inject fedha kwenye uchumi wetu na hata hilo alilosema mdogo wangu wananchi wanataka fedha mfukoni, yaani hata hii fedha tu ambayo mkienda huko Majimboni watendaji wetu watawaambia kwamba katika kipindi cha muda mrefu hawajawahi kupokea fedha nyingi hivi kwa wakati kwa mara moja kwenye miradi mingi hivi, mwisho wa siku fedha hizo zitakwenda kwa wananchi, kwa sababu ndiyo watakaojenga madarasa, ndiyo watakaojenga vituo vya afya, hata wale wakandarasi watakaochukua kazi hizo watatengeneza ajira za watu watakao ingia katika kutengeneza iwe darasa, iwe kituo cha afya au iwe madarasa ya shule zile za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni awamu ya kwanza tunaendelea nayo, tuna maliza hii tunaenda majengo mengine hiyo yote ndiyo itakayokuwa njia ya fedha kuendelea kuzipeleka kwa wananchi. Sasa hivi kila Wilaya hawataazimana mafundi yaani kila fundi aliyepo kwenye Wilaya yake atabaki pale pale kwa sababu shughuli zinaendelea kila Kata. Trilioni moja na zaidi inaenda kwenye kila Kata, kila eneo, kila Wilaya ya nchi hii na fedha hizo zitakuwa zinazunguka kwa wananchi mle mle na hayo yote yanaendelea kuchochea fedha ziwepo nyingi kwenye mzunguko kwa sababu hatutoi mkandarasi kutoka nje ya nchi kujenga darasa maana yake atakuwa wa humo humo, maana yake hiyo fedha itakuwepo humu hiyo itaongeza fedha katika mzunguko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, in long run pia tutaendelea kutengeneza ajira za kudumu kwa sababu hatuwezi tukajenga madarasa elfu 15 halafu Walimu wakawa wale wale, tutaongeza walimu hatuwezi tukajenga vituo vya hivyo vya afya vyote hivyo kila tarafa halafu yakawepo majengo tu, hatuwezi tukashusha X-Ray hizi zote kila wilaya CT scan kila Mkoa halafu pasiwepo na ajira ya kudumu, ajira za kudumu na zenyewe zinaenda kutengenezwa tutaongeza na wataalamu katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hili jambo siyo la mara moja yaani hii maana ya ‘Kazi Iendelee’ hii siyo jambo la mara moja maana yake linaendelea, watu wengine baada hizi fedha kushuka nyingi hivi walidhani ni bajeti ya miaka mitano, yaani hii hapa ni bajeti inayoenda mpaka mwezi wa sita tu, na mama akasema ule mwaka mwingi unaofuata utakuwa kiboko zaidi na hivi tunavyoongea kuna fedha zingine zipo kwenye reserve. Kwa hiyo inayokuja itakuwa kiboko zaidi, sasa wewe chukulia madarasa ya mara hii ongeza ya mwaka kesho unakuja, ongeza vituo vya afya mwaka kesho nenda kwenye barabara hivyo hivyo fedha zinakwenda kwenye ofisi ya TARURA katika kiwango hicho, ongeza na mwaka mwingine, ongeza na mwaka mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi tu hapa mlioko hapa Waheshimiwa Wabunge niwaambie neno moja tu hili la kindugu kabisa, msingekuwa wakinamama mngepata kazi sana kwenye kugombea, lakini kwa kuwa ni wakinamama mkifika maeneo hayo mtakuwa mnasema mimi ndiyo Samia wa eneo hili mtapata kura, lakini ukweli wa mambo mtu yeyote asiyeona kazi anayofanya Mheshimiwa Rais, kwa sababu mlikuwa mnabishabisha atakuwa haitendei haki nafsi yake na atakuwa pia haitendei haki nchi hii. Kazi hii inayofanyika ni kazi ya kihistoria ni kazi ambayo inabadilisha maisha ya wananchi wetu. Kazi ya kihistoria ni kazi inayobadilisha maisha ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tukisharudi Majimboni kazi hii anayoifanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni kazi ya kihistoria na nikazi inayokwenda kubadilisha maisha ya Watanzania. Waheshimiwa Wabunge tukisharudi Majimboni kwa sababu madarasa yatakuwepo yakutosha, madawati zaidi ya laki sita halafu na Walimu tunaenda kuongeza nendeni muwashawishi hata wale ambao walishaacha masomo, wanafunzi wale ambao wengine wanatokea jamii za kifugaji kama zetu, waambieni warudi shuleni elimu yenyewe bila ada, madarasa hamna kubanana kwenye madawati, halafu hamna hata yule ambaye hajaelewaelewa hamna kukaa kwenye mawe maana yake zamani ilikuwa usipo fanyafanya vizuri hesabu wewe ndiyo unakosa nafasi ya kukaa, hii na Walimu tumesema wanaenda sambamba na majengo haya, hatutajenga majengo tu na Walimu katika kipindi hiki kifupi na Walimu wanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya aina hiyo siyo kazi ya kuibeza na kazi ya aina hiyo haijasimamisha miradi mikubwa na miradi mikubwa na yenyewe inaendelea, miradi mikubwa ya kimkakati inaendelea na kwenye shughuli za uzalishaji kama mpango tulioutoa na tumesema tutaunyumbulisha kwa sababu kwa wakati huu tulileta ili tupate maoni tumeshapata, tumepata maoni mengi sana na baada ya hapa tumeyapokea na timu ya wataalam tutaendelea kukaa, lakini pia Kamati yetu na yenyewe itaendelea kuchambua, tutaendelea kupata maoni zaidi tutakapokutana tunaamini tutatengeneza jambo lililo bora sana ambalo litatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ninalowaomba twendeni tukamsaidie Mheshimiwa Rais kusimamia fedha hizi kule zilipokwenda. Upande wa wizara tumesema tutaituma Idara yetu ya Ukaguzi wa Ndani ambao wapo kila eneo wasimamie effectively na siyo fedha hizi tu na fedha zingine zote ambazo zinahusu maisha ya Watanzania ambazo zinaenda katika miradi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini haya yote yatafanyika na yataweza kubadilisha maisha ya Watanzania na Watanzania watafurahia vizuri sana kazi anayofanya Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake anayoiongoza pamoja na ushauri mzuri ambao Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lako Tukufu wanatupatia ili kuweza kuboresha mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimeyasema hayo nakushukuru sana. Naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.