Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adhimu kuweza kusimama leo katika Bunge lako Tukufu hili, ikiwa ni mara ya kwanza kwangu mimi kuweza kusimama na kuzungumza na mimi kutoa mchango wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ningependa kuanza na kutoa shukurani kwa sababu, mimi ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili. Ningependa kuwashukuru kwanza wapiga kura wangu wa Jimbo la Konde kwa kunichagua kwa kura nyingi sana, walinipa ushindi wa asilimia 72 katika uchaguzi ambao ulifanyika wa marudio nawashukuru sana. Pia ningependa kushukuru chama changu, Chama cha ACT-Wazalendo kwa kuniamini na kuni- support mpaka kufikia ushindi huo ambao leo nimepata heshima kubwa ya kuwa Mbunge katika Jimbo la Konde, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote mimi nimekaa hapa kwenye kiti baada ya msiba wa marehemu Kaka yangu Khatib Said Haji, Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema roho yake peponi. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Amina.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru wewe pia kwamba ulikuwa unawasiliana na familia kwa ajili ya kusimamia matibabu ya Mheshimiwa Marehemu Khatib Said Haji. Yale mawasiliano uliyokuwa unafanya ulikuwa unafanya na mimi na niliziona juhudi zako. Kwa niaba ya familia tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru Serikali mbali ya juhudi ulizozifanya wewe, tulikuwa tukipata mawasiliano kupitia Serikali. Kwa ajili ya kuhakikisha mpendwa wetu yule maisha yake yanaokoka lakini kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu ilikuwa bahati mbaya Mwenyezi Mungu alimuhitaji zaidi. Kwa hiyo, kwa hali hiyo nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kuishukuru Serikali kwa kuendesha uchaguzi wa marudio wa Jimbo la Konde. Uchaguzi ambao ulikuwa ni mfano wa kuigwa, uchaguzi ambao ulionesha kwamba Tanzania tunaweza kufanya uchaguzi wa demokrasia, demokrasia ikashika nafasi yake na watu wote wakafurahia matunda ya demokrasia. Kwa kweli naipongeza sana Serikali kwa kufanya uchaguzi ule ambao hata kunguni hakuuliwa wala hakuguswa. Ahsanteni sana Serikali kwa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kumshukuru pia Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na kumpongeza sana, katika hotuba yake ambayo alionesha dhahiri ana nia ya kusimamisha demokrasia katika nchi yetu pale alipokuwa kwenye kumbukizi ya maisha ya Marehemu Maalim Seif Shariff Hamad. Namshukuru sana na ninamuomba, aendelee na nia hiyo hiyo ya kusimamisha demokrasia ili Tanzania tusiwe ni wahanga wa demokrasia tuwe tunafurahia matunda ya demokrasia. Kwa hiyo, ningependa kushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo nije kwenye mpango. Mimi natoka Visiwa vya Zanzibar ni Mbunge kutoka visiwani. Ukisikia Visiwa ni kwamba tumezungukwa na bahari. Bahari sasa hivi imekuwa ikimeza visiwa kila uchao, visiwa vimekuwa vikimegwa kupitia bahari. Hili lipo katika sehemu ya mazingira. Ukija kwenye Jimbo langu la Konde nimezungukwa na bahari kupitia sehemu zangu za Msuka, Makangale, Tondooni, Mnarani kote ni bahari tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahari imeshakula karibu nusu kilomita ya eneo la ardhi katika Jimbo langu. Sasa, nikija kwenye mapendekezo ya mpango napendekeza kwamba, katika Jimbo langu kuna kilimo kikubwa sana cha mwani, kilimo hiki mwenzangu Mheshimiwa Omar alikizungumzia jana lakini mimi nitakizungumzia katika eneo tofauti. Nitazungumzia katika maeneo mawili. Eneo la kwanza ni kwamba, kilimo cha mwani ni kilimo ambacho kinalimwa baharini na unapolima kilimo cha mwani maana yake bahari unaifanya ikimbie katika eneo la ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hiki kilimo ni kilimo ambacho Serikali inatakiwa kukiangalia sana na kukipa nguvu kubwa ili kuokoa ardhi kuliwa na bahari. Lakini lingine katika kilimo hiki unapolima kilimo hiki maana yake kunapatikana mazalia ya samaki, pia ni faida kubwa sana nimeona katika mpango, tunategemea kupata meli nane za uvuvi pia kama tutakuwa tuna mazalia wengi sana ya samaki, maana yake hizo meli za uvuvi ndio zitaweza kupata kazi. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba Mheshimiwa Waziri katika mpango wako uweke kipaumbele katika kilimo cha mwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikihama katika sehemu hiyo nakuja katika kukuza mapato. Katika mpango umetueleza kwamba mapato yameendelea kukua kwa asilimia 7.2 ni kweli kwa data ulizonazo wewe ni hivyo, kama tunavyojua njia kuu ya mapato ya Serikali ni TRA, TRA ndiyo wanakusanya mapato kwa asilimia kubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita TRA walilalamikiwa sana kwa kufanya makadirio ambayo yalisababisha wafanyabiashara wengi kufunga biashara zao. Sasa hawa TRA wamekuwa kama vile sijui nisemeje mimi. Maana yake wakati ule walilalamikiwa kwa kutoa makadirio makubwa, kuwalazimisha wananchi kodi ambazo hazina msingi, sasa wamehama katika stage ile wamewachenga kidogo wafanyabiashara, sasa hivi wameleta e-filing. E-filing maana yake mfanyabiashara atapeleka ripoti zake kwa kutumia mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini e-filing tuelewe kwamba wafanyabiashara wengi hawana uelewa wa mambo ya mitandao. Wafanyabiashara wetu ni wale ambao wameshindwa na maisha wakaamua kujiingiza katika biashara. Sasa basi e-filing walivyoileta wameweka mambo ambayo ni ya ajabu ambayo hayamsaidii mfanyabiashara. Kwa sababu, kama walikuwa na shida ya kukusanya mapato kwa kutumia system hii ni sawa, lakini kwanza wangetoa elimu kwa wafanyabiashara hili halikufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili wameingiza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, ahsante sana.