Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MPAKATE D. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia hoja ya Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Walemavu, Wazee pamoja na Watoto. Kwanza kabisa, napenda niwapongeze Mawaziri hawa wote wawili kwa ku-translate Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika hotuba yao iliyofanya kila mmoja asisimke. Nasi ni wajibu wetu kuchangia kuongeza nyama ili pale ambapo pamepungua waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, naungana na wasemaji wenzangu waliozungumza awali kuhusu suala la wazee; tumezungumza bima, tumezungumza suala la dirisha maalum la wazee, lakini tunaleta msisitizo mkubwa kwa sababu Ilani ya Chama cha Mapinduzi tumeinadi sana vijijini kuhusu pensheni ya wazee zaidi ya miaka 65. Katika maelezo yake au hotuba yake haijaonyeshwa vizuri ni lini program hii itaanza au ikoje ili Waziri atakapokuja atueleze hawa wazee wataanza lini kufikiriwa suala hili la pensheni ya wazee wenye umri zaidi ya miaka 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nitazungumzia suala la Hospitali ya Wilaya ya Tunduru. Hospitali hii ni ya muda mrefu, tangu miaka ya 1990 huko, lakini hadi hivi sasa ina majengo yaliyochakaa na mbaya zaidi hakuna wodi ya upasuaji. Wagonjwa wakipasuliwa, wakitoka theater wanachanganywa na watu wengine pamoja na madonda yao waliyokuwa nayo. Hii ni hatari, inahatarisha zaidi afya ya wale wagonjwa ambao wanafanyiwa upasuaji. Kwa hiyo, naomba Serikali ifikirie namna ya kuweza kusaidia hospitali ile kupata wodi kwa ajili ya wagonjwa ambao wamefanyiwa upasuaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hospitali ya Wilaya ya Tunduru kulikuwa na chuo pale ambacho kilikuwa kinafundisha Manesi mbalimbali ambao walikuwa wanatoka vijijini, lakini chuo kile kiliungua moto zaidi ya miaka kumi iliyopita na mpaka leo majengo yale hayajafanyiwa renovation na kile chuo kimekufa moja kwa moja. Ile nafasi ambayo walikuwa wanapata vijana wa Tunduru kusoma pale na baadaye walikuwa wanaajiriwa na zahanati zetu zilizoko vijijini kwa mikataba na vijiji wakisubiri ajira ya Serikali Kuu, sasa imekufa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atupe majibu halisi, chuo kile ni lini kitakarabatiwa ili kiweze kuwafundisha vijana wetu ambao wanaweza kusaidia jamii zetu kwa sababu tunalalamika sana kwamba wahudumu ni wachache katika zahanati zetu na mbaya zaidi Wilaya ya Tunduru, pamoja na kuwa na zaidi ya vijiji 150, lakini kuna zahanati 49 tu, vituo vya afya vitano na gari ni moja tu ambalo lipo kwenye Hospitali ya Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, akinamama wanatembea umbali wa zaidi ya kilometa 30 kufuata huduma ya afya, ni mbaya sana. Naomba sana, pamoja na kwamba Wizara ya Afya inatekeleza sera, naamini pacha wake ambaye ni Serikali za Mitaa, analijua hili na naomba alifahamu na ikiwezekana baadaye waweze kufika kule waangalie hali mbaya ya Wilaya ile; kwa sababu Wilaya ile ni kubwa ukilinganisha na Mkoa wa Mtwara. Wilaya ya Tunduru ni kubwa na Mkoa wa Mtwara una Wilaya tano. Naomba sana hili tufikiriwe kwa sababu tuko katika hali mbaya sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia katika hotuba hii ni suala la wafanyakazi wa ustawi wa jamii. Ni kweli ni tatizo, kama nilivyochangia katika Idara ya Kilimo, suala la ushirika linafanana sambamba na ustawi wa jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara hii tumeisahau sana; watumishi ni wachache, huduma hakuna, usafiri hakuna, incentives hawapewi; sasa tunategemea vikundi vya akinamama vya maendeleo vyote vipate huduma kutoka kwa hawa watumishi wa ustawi wa jamii, lakini bahati mbaya nao wako katika hali mbaya, hoi, huduma hawapewi. Naomba sana wathaminiwe ili waweze kufanya kazi yao nzuri ya kuwasaidia ndugu zetu huko vijijini waweze kujikwamua kiuchumi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho naomba nichangie suala la upungufu wa madawa. MSD ni tatizo. Mara nyingi sana dawa nyingi zinazofika katika Hospitali, Zahanati zetu na Vituo vya Afya, zinakuwa zimepitwa na wakati. Sijajua ni kwa nini muda mwingi dawa zile zinakuwa zimepitwa na wakati. Mbaya zaidi wananchi wanasikia namna MSD wanavyoteketeza dawa ambazo zimepitwa na wakati, huku vijijini hakuna dawa. Naomba sana suala la MSD kupata dawa na kusambaza kwa wakati liwe la muhimu sana ili watu wetu wapate huduma ya dawa kwa wakati ili kufufua matumaini ya watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naomba sana Vyuo vya Maendeleo ya Jamii. Tunduru tuna Chuo cha Maendeleo ya Jamii, kipo pale Nandembo, lakini hakina huduma. Kwa mwaka kinafundisha chini ya watu 200. Sasa sijui maendeleo haya tunayoyataka kwa wananchi wetu wakati chuo kile hakiwezi kuchukua watu zaidi ya 200 kwa mwaka! Kwa kweli ni hatari! Tunaomba sana Serikali itilie mkazo chuo kile iweze kuwapeleka wataalam wazuri, iwapelekee fedha waendeshe program zao za kila siku ili watu wa Tunduru nao waweze kufaidika na jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naomba sana Serikali iangalie suala la usafiri katika zahanati zetu zilizoko na vituo vya afya ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja