Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango ulio mbele yetu. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa wasaa kwa kusimama mbele yako kuchangia Mpango huu. Vile vile kama ilivyo ada nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa mambo makubwa anayolitendea Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili niende nalo mbali kidogo kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa namna anavyolipendelea Taifa letu. Huu uongozi wetu sasa ni Awamu ya Sita, lakini katika Awamu zote hizo Mwenyezi Mungu amekuwa akituletea viongozi ambao kwa kweli wana kiu kubwa kuliona Taifa letu linatengemaa na linasonga mbele. Kwa hiyo tushukuru sana kwa Mwenyezi Mungu kwa karma hiyo ambayo ametupa sisi Watanzania, kutupatia Viongozi ambao kila kiongozi anayesimama, anasimama kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani hii haitakamilika kama hatutakishukuru Chama chetu Cha Mapinduzi kwa kulea viongozi, kwa sababu hawa viongozi wote wanapikwa ndani ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo chama kiendelee kupika viongozi ili Taifa letu liendelee kutengemaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirejea kwenye Mpango asilimia 90 kama siyo 95 ya waliochangia kuanzia jana mpaka leo wanazungumzia suala la kilimo, hii ni kuona namna gani kuna umuhimu wa kilimo kwenye Taifa letu. Kwa mtazamo wangu nasema bado kama Taifa hatujaamua kuwekeza kwenye kilimo. Hatujaamua kuwekeza kwenye kilimo kama ambavyo tunawekeza kwa maneno kuipa kilimo hizi semi mbalimbali; siasa ni kilimo, kilimo uti wa mgongo, kama haya maneno yangelingana na matendo yetu, leo kilimo kisingefika hapa tulipofika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika mahali ambapo Bodi zetu za Mazao zinaendeshwa na wakulima. Leo tunazungumzia mfano mmoja kama Bodi ya Korosho inaendeshwa na wakulima wa korosho. Kila mkulima wa korosho anapouza korosho yake Sh.25 inapelekwa Naliendele kwa ajili ya kuimarisha utafiti. Kila mkulima anapouza korosho yake Sh.25 inakwenda kwenye Bodi ya Korosho.

Kwa hiyo, mtaangalia taasisi zetu za kilimo zinaendeshwa na mkulima, Bodi zetu za Mazao zinaendeshwa na wakulima, Taifa linafanya nini kuhakikisha hivi Vyuo Vyetu vya Utafiti wanavitengea fedha za kutosha, tuweze kufanya utafiti wa kutosha ili tuweze kuzalisha vya kutosha na kufanya kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, Serikali kwenye Mpango huu napendekeza ije na Mpango mahsusi ituonyeshe ni wapi tunakwenda kupata mbolea, kipo kiwanda pale kinazungumzwa muda mrefu sana cha LNG. Kile kiwanda kingefanya kazi kutupatia malighafi nzuri sana kwa ajili ya kutengenezea mbolea, lakini leo hii tunakwenda kwenye uhuru wa miaka 60 hatuna kiwanda chochote kile cha mbolea chenye uhakika cha kuweza kukitegemea. Hapo utaona kabisa kwamba bado hatujaamua kuwekeza kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu; Mpango huu utakapokuja utuainishie kuna mkakati gani kwa ajili ya kuinua kilimo chetu. Kikubwa ambacho nakiona kwamba hii mipango tunayokuja nayo huwa hatujaifanyia tathmini kila baada ya mwaka. Tunapoletewa Mapendekezo ya Mpango huu, vile vile tuambiwe mwaka jana kwenye kilimo tulikuwa tumepanga nini na tumefikia wapi? Kwa nini hatukufikia tulipokusudia kufika na kama tumefika, tumefika kwa nyenzo zipi. Kwa akili yangu ya kawaida nasema hatujafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala lingine, suala la utalii. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan, ameamua kukuza utalii nchini. Sasa ombi langu kwenye Mpango utakaokuja tuone ni namna gani tunakwenda kupokea hao watalii, tumejiandaa vipi kupokea hawa watalii. Kwa taarifa nilizonazo, hawa wamiliki wa ndege zetu hizi ndogo ndogo ukiachia Air Tanzania, kwanza ni wachache, halafu uwekezaji kwa hapa nchini wanasema ni ghali mno na hizi Regulatory Authorities nazo ni nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo hii mtalii gani atakuja, ambaye anaambiwa kutoka Dubai kuja Dar es Salaam ni rahisi zaidi kuliko kutoka Arusha kwenda Mikumi, kweli are we serious? Kama mtu anatoka nje, anakuja kutalii analipa fedha kidogo, kuliko fedha atakayolipa kutoka Arusha kwenda Ngorongoro. Hili jambo naomba mpango utakapokuja watueleze, mama anahangaika huko kuimarisha utalii na huku Mawaziri watuonyeshe kwamba tumejiandaa, tunazo ndege kiasi gani za kupokea hawa watalii kupeleka kwenye hizo hifadhi zetu na kwenda kwenye vivutio vyetu. Tuna ndege kiasi gani? Tuna watoa huduma wangapi? Jambo hili naomba watakapokuja nalo lizungumzwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna jambo hapa kama nimeanza kulisikia sikia kuna azimio la anga la Jumuiya Afrika Mashariki, anga huru la Jumuiya Afrika Mashariki, mpango huu utakapokuja utuambie ikitokea azimio hili kweli likaletwa hapa Tanzania tumejiandaa vipi kulipokea, maana inawezekana mkafungua hili anga mkifungua mnawafungulia watu tu ninyi mna ndege tano wengine wana ndege 1,000 unaingiaje kwenye utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mpango utakapo kuja naomba utuelekeze mpango huu utakapoletwa utuambie tumejiandaa vipi kukabiliana na janga hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nijielekeze kwenye sera mara nyingi tunazo sera ambazo zinamipaka yake labda niseme miaka mitano, miaka miwili lakini tunazo sera zingine ambazo hazina limit na utekelezaji wake umekuwa ni mgumu sana kwa sababu hatuna kipimo. Mfano tumekuja na sera kuunganisha barabara zetu za mikoa na kila mkoa hatujasema mpaka lini, matokeo yake sasa hivi tumehama tunaenda kuunganisha wilaya wakati bado kuna mikoa bado hatujamaliza kuiunganisha na hii ni kwa sababu hatujajipa muda ifikapo mwaka fulani tutakuwa tumemaliza kuunganisha mikoa tuingie kwenye hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sera ambazo zinakuja bila kuwa na muda maalum ndiyo hizo zinakuwa zinatubabahisha tunakuwa hatujui nini tunafanya matokeo yake tunaruka kwenye hatua moja tunaenda hatua nyingine kabla hatua ya pili hatujamaliza, leo hii kuna mikoa bado hatujaweza kuiunganisha lakini tayari tumeshaanza kuunganisha Wilaya kwa Wilaya. Sasa zile Mikoa sijui tumeacha au sera imekufa sijaelewa hapo.

Mheshimiwa mwenyekiti, kwa mfano tuko na sera nyingine kwamba kila kata iwe na kituo cha afya, nashukuru mwaka huu Serikali imekuja na Sera nyingine kwamba siyo kwamba kila kata itajengwa kituo cha afya badala yake tunakwenda kujenga kituo cha afya kwa kimkakati kulingana na uhitaji na mazingira yaliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini je, tumeshaletewa tathimini tunapokwenda kuiacha ile sera tunakuja na sera nyinge tumeshaletewa tathimini hapa Bungeni kwamba tuonyeshe kwamba ile sera tuliyokuja nayo ya kila Kata na kituo cha afya imetufikisha wapi? Ina shida gani? Na kama ilikuwa na mafanikio kwa kiwango gani? Kwa hiyo, ninaiomba Serikali kwa hayo machache ilikuwa mchango wangu kwa hayo mambo mawili tu Kilimo, Utalii na hii ya Sera. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)