Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa, napenda kutumia nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan. Kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwatumikia Watanzania na kwenda maeneo mbalimbali duniani, kutafuta nusura ya Watanzania hasa katika mambo ya msingi yanayotukabili. Nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa tunaanza kupokea huu Mpango ulituongoza ukatueleza na kutusomea kanuni, nami nimezingatia sana. Ukasema Mpango huu ni mwongozo wa bajeti ijayo, lakini ukasema vile vile tushauri vyanzo vipya vya mapato; na la tatu, ukasema tushauri vipaumbele vya bajeti. Nami nitajielekeza huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kwenda huko, katika maelezo yaliyotolewa na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake, ukurasa wa saba ameelezea utekelezaji wa baadhi ya miradi katika kipindi hiki, lakini nataka kuzungumza moja ya jambo kubwa ambalo nimekuwa nikilizungumza hapa Bungeni na ambalo nilijiteua kuwa balozi mimi mwenyewe, nalo linahusu suala la riba za mabenki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mzee Kimei, Mbunge mwenzangu ambaye ni mbobezi kwenye masuala ya mabenki alilizungumza vizuri sana kwa lugha ya kitaalam zaidi, mimi nitalishusha katika lugha ya kawaida ambayo kila mmoja anaweza akaielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa 2019/2020 watu waliokopa katika mabenki walikuwa asilimia 8.1, lakini mwaka wa 2020/2021 waliokopa katika mabenki walikuwa asilimia 4.3 yaani wakopaji wameshuka. Riba za mabenki kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri, zimeshuka kutoka asilimia 16.8 mpaka asilimia 16.6. Yaani kushuka kwenyewe ni kwa 0.2 percent. Napenda kuipongeza sana Kamati ya Bajeti, sana sana; Mwenyekiti na Wajumbe wote wa Kamati ya Bajeti, wamekokotoa jambo hili vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati riba za mabenki zimeshuka kwa 0.2%, riba za mikopo inayotolewa na Benki Kuu kwa mabenki ya biashara imeshuka kutoka 12% mpaka 7%. Maana yake imeshuka kwa 5%. Kilichotokea ni nini? Ni kwamba Benki Kuu imeshusha kwa 5%, mabenki ya biashara ambako ndiko yanakwenda sasa kwa watu wetu, hao ambao tunasema tunataka kuinua sekta binafsi, wameshusha kwa 0.2%. Hapa kushusha kwa Benki Kuu kumeenda kunufaisha mabenki badala ya kuwanufaisha wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ukiliangalia kwa sura ya kawaida, unaweza ukaliona tu; lakini ukiingia ndani zaidi, unaweza ukasema hapa kuna ufisadi. Kwa nini nasema hivyo? Maana Serikali yenyewe, Benki Kuu yake inatoa kuyapa mabenki ya biashara kwa 7%, lakini Serikali yenyewe inakwenda kukopa kwenye mabenki ya biashara kwa 15% ya riba. Najua kwa mujibu wa sheria Serikali haiwezi kukopa Benki Kuu, lakini huu ni mzigo mkubwa sana kwa wananchi, asilimia 15 ya riba kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti imeishauri Serikali na ninataka kuiomba Serikali yetu sikivu, izingatie ushauri huu. Isipozingatia ushauri huu, siku moja kwenye ukumbi huu tutaikataa bajeti. Imeishauri Serikali isikope kwenye mabenki ya biashara kwa zaidi ya asilimia 10. Msingi wake ni nini? Kuwapunguzia mzigo walipa kodi Watanzania wa kulipa asilimia kubwa ya riba ya mabenki. Isikope kwa zaidi ya asilimia 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili mnalitazamaje? Ni kwamba kama Benki Kuu inakopesha kwa 7% halafu wanatoka watu wa benki za biashara wanakopesha Serikali kwa asilimia 15 inawezekana wapo watu kwenye Serikali yetu, wana hisa kwenye haya mabenki, wanapiga hela kutoka huku Benki Kuu wanaleta huku, wanaikopesha Serikali, ikirudishwa wenyewe wanapata gawio kubwa. Ndiyo maana yake. Jambo hili ndiyo nasema, sitaki mimi nijipe kazi ya kuanza kuangalia kuna wakubwa gani kwenye Serikali wana hisa kubwa kwenye mabenki, kwa hiyo, wananufaika na mchezo huu? Sitaki kujipa kazi hiyo, lakini itoshe kusema busara ituongoze katika hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema hapa, nikamwuliza Waziri wa Fedha na kwa bahati mbaya haya maneno yetu huwa tunazungumza hapa wakati mwingine huwa yanageuka kama ngonjera tu, kwamba wayachukue wasiyachukue, sawa sawa. Ni kwamba, hivi ni nani anaye- control hizi microfinance institutions? Kampuni hizi za kukopesha wananchi ambazo zinapiga riba na wananchi wetu wanateseka, wamenyang’anywa ma-fridge na nini? Sikupata majibu mpaka leo na kazi hiyo inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha hata hii taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha inayosema, riba zimeshuka kutoka asilimia 16.8 mpaka asilimia 16.6, bado haina usahihi sana na hali ya sasa. Mimi nimekopa benki mwezi jana (Oktoba), na mwezi huu nimeanza kulipa mikopo ya kibiashara. Siyo mikopo yetu hii, hapana, ni mikopo ya kibiashara, maana mimi ni mfanyabiashara vilevile. Nimekopa kwa riba ya asilimia 21, akitaka mikataba yangu nitampa aione. (Makofi)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, nimekuruhusu Mheshimiwa.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: nikubaliane na mchangiaji na nimwongezee tu kwamba mfanyabiashara unapokopa kama una hati ya nyumba kwa maana ya dhamana ni asilimia 21 na kama hauna hati ni asilimia 24.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Ni sahihi sana na naipokea taarifa….

MWENYEKITI: Na bado mnakopa Waheshimiwa? Asilimia 24?

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Ni sahihi kabisa.

MWENYEKITI: Endelea Mheshimiwa.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, una kitu kinaitwa letter of offer asilimia 24, kama una tittle deed asilimia 21. Kwa hiyo asilimia 16 inayozungumzwa hapa haipo, sijui labda kwenye baadhi ya mabenki, Kamati ya Bajeti inatueleza nini? Kamati ya Bajeti inatueleza kwamba BOT imeshindwa kuwasaidia wananchi katika kupunguza riba za mabenki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme, katika mambo yanayohusu utumishi wa wananchi sina urafiki. BOT siku moja inaweza ikamrudisha Waziri wa Fedha viti vya nyuma, asipoiangalia BOT siku moja itamrudisha viti vya nyuma. Hatuwezi kwenda hivi, wananchi wanapiga kelele, hali mbaya ya uchumi, tunasema, tunasema lakini hakuna linalokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wenzangu wametangulia kusema hapa na naomba niseme, narudia kumpongeza sana Raisi wetu mpendwa. Jana kuna lugha ilitoka hapa, ni vizuri katika mambo haya kuwekana wazi, Mheshimiwa mwenzetu Mheshimiwa Mpina, alisema lugha ambayo wengi haikutufurahisha. Haikutufurahisha kwa sababu mama au kiongozi wa nchi anapokwenda kutafuta manufaa kwa ajili ya watu wake, akija hata kama na uji, onyesheni kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Raisi amekuja na trilioni 1.3, kuna kazi inafanyika ambayo haijawahi kufanyika ndani ya kipindi kifupi kama hiyo kwenye majimbo yetu; Mheshimiwa Mpina anachotueleza nini kwamba wameacha pesa nyingi huku, pesa gani anazosema? Pesa ambazo zipo katika Mahakama ya Usuluhishi wa Kikodi baina ya Barrick na Serikali kuhusu masuala ya kodi zinazotokana na madini, yaani zipo kwenye Mahakama, yeye ndio anatuambia ndio pesa zimeachwa. Ikihukumiwa kwamba nyie hamna kitu maana yake hamna kitu. Sasa huo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kilumbe nikuhakikishie…

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Ndio.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina huwa analewa togwa, kwa hiyo msamehe tu, asikupotezee dakika zako. (Kicheko)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka kusema habari ya kutuambia kwamba tunapiga makofi mpaka mikono inataka kuchubuka kwa sababu ya trilioni 1.3, kama yeye amezipuuza nashauri ile miradi ya maendeleo iliyopelekwa Jimboni kwake iletwe Jimboni kwangu mimi nazithamini sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)