Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia, kwenye mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa. Awali ya yote niungane na wenzangu ambao wametangulia kwenye kumshukuru na kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa fedha ambazo ametupatia kwenye maeneo yetu hasa kwenye eneo la elimu, afya, maji, umeme na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza sana ndugu yangu Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kuwasilisha vizuri Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nakupongeza wewe na Mheshimiwa Spika kwa jinsi ambavyo mnatuongoza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wenzangu ambao nafanya nao kazi kwenye Wilaya yangu ya Hanang kwa ushirikiano ambao wananipatia. Ushirikiano wao ndiyo uliowezesha Halmashauri ya Wilaya ya Hanang kuongoza Kitaifa kwenye makusanyo ya mapato. Hii imewezekana tu kwa sababu viongozi tumeshirikiana kuanzia Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkurugenzi, Waheshimiwa Madiwani na viongozi wengine, pamoja na watendaji wa Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza Wana- Hanang kwa jinsi ambavyo wanatuwezesha sisi kutekeleza majukumu yetu vizuri, sana sana wanaotuunga mkono kwenye ukarabati wa Hospitali ya Wilaya Tumaini, ambako tuna bajeti ya zaidi ya shilingi milioni 200 na mpaka sasa karibu bajeti yote imepatikana ya kukarabati Hospitali ya Wilaya. Ninawashukuru sana kwa jinsi ambavyo wamejitoa, ninaamini Serikali itatuunga mkono; kuna upungufu wa majengo pale, tutapata yale majengo ambayo yanapungua ili angalau, huduma za afya ziweze kutolewa vizuri kwenye Hospitali yetu ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie kwenye Mpango huu. Tumesema mara nyingi kwamba kilimo ni uti wa mgongo na tumesema na hata kwenye Mpango imeandikwa kwamba, asilimia zaidi ya 66 ya wananchi, wanategemea ajira zao kwenye kilimo, lakini ukienda kwenye maeneo ya vijijini ni zaidi ya asilimia 90 watu wanategemea kilimo na ndio wengi wapo huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, bila kuwekeza kwenye kilimo hatutapiga hatua. Tumekuwa na dhana na matamko mbalimbali kwenye eneo la kilimo. Tumekuwa na Kilimo Kwanza na matamko mengine kama hayo. Sekta hiyo inaajiri watu wengi. Ukiangalia wananchi au vijana wengi, wanaokimbia vijijini kwenda mijini, ni kwa sababu kilimo hakina tija. Ili tupate tija kwenye kilimo, ni lazima tuweke fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tupate wataalam watakaosaidia wakulima wetu kulima kisasa ili tupate tija kwenye kilimo. Tupate wataalam wa mifugo ambao watasaidia wafugaji ili angalau ufugaji upate tija. Bila kuwekeza kwenye kilimo kimkakati, bila kukiangalia kilimo na tukawa tunaweka fedha kidogo kidogo, hatutakwenda kokote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mambo mengi tunayoyafanya, tutakuwa tunaangalia sehemu ambazo zinaajiri chini ya asilimia 30 ya Watanzania. Kilimo chetu kina changamoto nyingi; kilimo kinategemea mvua. Ni lazima tuwekeze kwenye kilimo cha umwagiliaji. Tumeongea na tumeahidi kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kwamba tutatafuta mbegu, pembejeo, viuatilifu vya bei nafuu, lakini hali kwa sasa ni mbaya kwa wakulima wetu, lazima tuangalie eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunayo mashamba makubwa kwenye nchi yetu ambayo mengine tumeyabinafsisha. Tunayo sababu ya kuangalia ufanisi wa hayo mashamba ili hatimaye pia hayo mashamba ambayo tumewapa wawekezaji ambao inawezekana hawana nia au hawana uwezo wa kuwekeza; tufanye tathmini ya kina, mashamba yale ambayo tunaona hayana tija kabisa, tuyatwae ili kuyapangia matumizi mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia lazima tuwekeze kwenye suala la kufanya uchakataji wa mazao yanayozalishwa na wakulima wetu, ikiwepo kwenye upande wa kilimo na upande wa ufugaji ambako ndiko kuna wananchi wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye huu Mpango ambao tunaenda nao, lazima tuangalie sana eneo la miundombinu ya barabara za vijijini, kwani kule wakulima wakilima, mazao yale lazima yasafirishwe na kuwe na usafiri wa uhakika. Kuna maeneo mengine kwenye nchi yetu na hasa Jimbo langu la Hanang, mvua zikinyesha safari ndiyo imeishia hapo. Hakuna kwenda kupata huduma za kiafya, hakuna shughuli za kimaendeleo inayoendelea, mazao ya kilimo hayasafirishwi na tunatakiwa lazima tuwekeze kwenye eneo hilo. Tuwekeze kwenye uchakataji ambao hatimaye pia tutaleta ajira za kutosha kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiboresha kilimo bila kuboresha miundombinu hakuna kitu chochote cha maana ambacho tutakifanya. Lazima tuhakikishe kwamba tunaboresha upande wa bandari, tuboreshe viwanja vyetu vya ndege. Kwa mfano, Mkoa mzima wa Manyara pamoja na ukubwa wake wote, hauna hata kiwanja kimoja cha ndege. Ipo kwenye Mpango muda mrefu; Kiwanja cha Ndege cha Mkoa wa Manyara. Itakuwa rahisi watu kufanya shughuli zao kama kweli kuna usafiri wa ndege unaofikika kwa urahisi Mkoani Manyara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna barabara yetu ambayo inaenda kwenye mashamba yenye uzalishaji mkubwa wa ngano. Barabara ya kutoka Mogitu kwenda Haydom, kule tunazalisha ngano ya kutosha; shayiri pamoja na ngano ya chakula. Ile barabara ikitengenezwa itawafungulia wananchi fursa kubwa sana ya kusafirisha mazao yao na kupata tija kwenye eneo la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2020 wakati tukiwa kwenye Mpango na kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, alisema yale ambayo tunaweza kuzalisha ndani ya nchi, tuzalishe na tuondoe nakisi hasa kwenye ngano ya chakula lakini na mazao mengine ambayo tunaweza kuyazalisha nchini kwa wingi, tusiagize nje ya nchi. Kwa mantiki hiyo, uwekezaji ule ambao ulifanywa kwenye ngano ya chakula, shayiri mwaka 2020, bei ilikuwa ya uhakika na wananchi waliingia mikataba ya Kilimo cha Shayiri. Mwaka huu kidogo inasuasua. Wizara ya Kilimo iangalie eneo hili ili angalau wananchi wapate mikataba ya kulima shayiri na ngano ya chakula na uzalishaji uwe wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)