Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii niweze kutoa maoni yangu katika mpango ujao. Lakini nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu, kipenzi chetu, kwa kazi nzuri anazozifanya, kwa dhamira yake ya dhati ya kuifungua Tanzania kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nishukuru kwa shilingi trilioni 1.3 ambayo kwa Jimbo la Meatu kwa trilioni 1.3 tumepata bilioni 2.6 ikiwepo miradi ya elimu, afya na maji. Lakini ukiongeza na fedha zingine ndani ya miezi mitatu, miradi ya barabara Jimbo la Meatu katika miezi mitatu tuna bilioni sita. Na kama watendaji wetu watakuwa na dhamira ya dhati ya kumsaidia Mheshimiwa Rais, dhamira ya dhati kuwasaidia wananchi wa Jimbo la Meatu, ndani ya muda mfupi Jimbo la Meatu linakwenda kubadilika kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze katika mpango wetu, nianze kwa kuunga mkono hoja ya Serikali, lakini niunge mkono hoja maoni ya Kamati ya Bajeti ambayo ni Mjumbe na nimpongeze Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Daniel Sillo, kwa namna anavyotusimamia katika Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Serikali inatarajia kuongeza makusanyo kwa asilimia 7.4 ikilinganishwa na mwaka 2021/2022. Kazi kubwa iliyopo mbele ya Serikali ni namna gani hizi asilimia saba tunaweza kuzifikia. Na Serikali imeweka msisitizo kuhakikisha kwamba mapato yote katika Wizara na taasisi za Umma yanaendelea kukusanywa kupitia mfumo wa GEPG, lakini katika utekelezaji wa mpango huu unaoendelea, Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 20 amesema kwamba kuna uvujaji mkubwa wa makusanyo ya maduhuli ya Serikali kwa Serikali za Mitaa na ulegevu wa matumizi ya EFD. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ninapenda niiambie Serikali, pamoja na kuzisema Halmashauri za Serikali za Mitaa, bado kuna taasisi 72 za Serikali ambazo hazijaanza kutumia mfumo wa EFD. Matokeo yake taarifa zake, takwimu zake haziwezi kusomwa katika mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali itoe mkazo na msisitizo kuhakikisha kwamba taasisi zote za Serikali zinajiunga na mifumo iliyoidhinishwa na Serikali kwa kuwa Serikali imetumia fedha nyingi kutengeneza mifumo hiyo. Hata kama tukisema taasisi hizo zipewe mitaji na Serikali, lakini pia kunakuwa na udhibiti katika makusanyo ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imeendelea kupokea fedha za mikopo ili kutekeleza miradi ya maendeleo. Naunga mkono hoja ya Kamati kwamba miradi yote inayotekelezwa kwa muda mrefu itumie mikopo ya muda mrefu ambayo ina masharti nafuu ambayo inaiva ndani ya miaka 10 Ili iweze kuleta faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali pia katika miradi ya aina hii, inayotekelezwa kwa muda mrefu ambayo inahitaji fedha nyingi itekelezwe kwa uchache. Inavyotekelezwa kwa uchache inatoa fursa ya kuweza kukamilishwa kwa wakati na kuanza kuleta faida ili iweze kusaidia kuchangia kurejesha mkopo na kuweza kusaidia deni letu liendelee kuwa himilivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, ipo miradi mingi iliyotekelezwa kwa kutumia mikopo, kwa mfano; daraja jipya la Selander alimaarufu kama Tanzanite Bridge. Miradi ya aina hii na mingine inayoonesha fursa ya kuweza kukusanya ushuru, naunga mkono hoja ya Kamati kwamba Daraja la Tanzanite litakapokamilika liweze kutumika kutozwa fedha kwa sababu kuna njia mbadala ambayo mwananchi ambaye ataona hawezi kutoa ushuru atatumia njia nyingine, kwa sababu taarifa tuliyoipokea ni kwamba magari mengi yanapita takriban kwa wastani magari 5,000 yanapita kwa siku katika barabara ile ya zamani. Kwa hiyo endapo kama asilimia kidogo au 25 au 30 itatumia Tanzanite Bridge kwa kutumia tozo, Serikali inaweza ikaingiza fedha ambayo itasaidia pia kuongeza katika kurejesha mikopo yetu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.