Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika mpango huu. Na kwa umuhimu mkubwa nitachangia katika sekta ya kilimo, hasa kwa kutambua umuhimu wake mkubwa katika kuongeza Pato la Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua umuhimu mkubwa wa sekta hii katika kukuza uchumi wa Taifa letu, na hasa tunapozungumzia sekta ya kilimo, ni sekta ambayo imetanuka kwa upana wake. Leo hii tumeketi katika Bunge hili ni kwa sababu tumekula chakula vizuri na ndiyo maana tumekusanyika hapa, yote hii ni sekta ya kilimo tunaigusa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini umesimamia kikao vizuri hapo kwa sababu umekula chakula kizuri. Leo hii tunamuona Waziri wa Fedha amekaa pale kwa kutulia, ni kwa sababu amekula chakula vizuri; yote hii tunaigusa sekta ya kilimo. Hata mgonjwa anapokuwa hospitali, doctor anapompa dawa anasisitiza kwamba ale chakula kwa kutambua umuhimu wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunapozungumzia viwanda, ili viwanda viende sawasawa ni lazima kwanza mtu awe amepata chakula, ameshiba na ndiyo maana atafanya kazi katika viwanda. Kwa hiyo hii ni sekta muhimu sana katika Taifa letu na tunatakiwa tuichukulie kwa uzito wa hali ya juu sana kwa ajili ya kukuza uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, tuamini kwamba hakuna uchumi unaoweza kukua katika Taifa lolote kama sekta ya kilimo itawekwa nyuma kwanza. Ni lazima tuitangulize sekta ya kilimo mbele ndipo tunaweza kufanikiwa katika mambo mengi ya kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema sekta ya kilimo ni muhimu sana; leo hii sekta ya kilimo inachangia kwa asilimia 26.7 katika kukuza uchumi wa Taifa letu, hivyo, tunapaswa kujua kwamba hii ni sekta muhimu sana kwa ukuaji wa uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la ajabu na la kusikitisha ni kuona kwamba sekta muhimu ya namna hii yenye kukuza uchumi wa Taifa letu inakua kwa asilimia 3 mpaka 4; hiki ni kitu cha kushangaza sana kwenye Taifa letu. Na ninashukuru jana Mheshimiwa Rais Samia alipokuwa akihutubia aliweza kuigusia sekta ya kilimo, kwamba ni sekta muhimu katika kukuza pato letu la ndani. Hata Mheshimiwa Rais anatambua umuhimu wa sekta hii katika kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninaona kwamba kwa namna sekta hii inavyokuwa kwa kusuasua inaonesha kwamba siyo kipaumbele katika Serikali yetu. Ninaweza nikazungumzia hali halisi, hasa kwa mikoa yetu ambayo kwa asilimia kubwa wanategemea kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii wananchi wa Mkoa wa Songwe wamekaa kusikiliza kauli ya Serikali inasema nini kuhusu pembejeo za kilimo maana hali ni mbaya sana ambayo inasababisha wananchi wengi na wakulima asilimia kubwa kukata tamaa kutokana na bei ya pembejeo za kilimo kuwa mara mbili ya ilivyokuwa awali. Na bei hizo zimesababisha wakulima wengi kushindwa kumudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu huu ukienda kwenye mikoa yetu ni mikoa ambayo wakulima wengi wanakuwa wameandaa mashamba lakini ni tofauti kabisa na miaka yote. Sasa hivi ukienda kila mkulima amekaa kwa hali ya kujisahau maana hana tumaini lingine. Watu wanawaza watapataje hizo pembejeo za kilimo kutokana na hali ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri tu Serikali, kama tunavyoweza kuweka kipaumbele katika miradi mingine, kama tunavyoweza kuhakikisha sekta ya ujenzi inakua kwa kasi, kama tunavyoweza kutumia nguvu kubwa kukuza sekta ya nishati, nguvu hiyo hiyo tuielekeze katika sekta ya kilimo ili kukomboa uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali siyo shwari kwa mikoa yetu. Sasa hivi hata tukienda huko kwenye mikoa yetu kuna hatari ya kupigwa mawe, maana mwananchi hana tumaini kabisa na hajui kesho yake itakuaje. Na kwa kujua kwamba mawazo huwa yanasababisha vidonda vya tumbo, ni hatari zaidi huko kwa wananchi wa Mkoa wa Songwe kuugua vidonda vya tumbo maana hawana tumaini, wamejawa na msongo wa mawazo, kitu ambacho kinaweza kikawasababishia matatizo ya kiafya kwenye miili yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali itumie njia ya dharura kutatua suala la pembejeo za kilimo kwenye mikoa yetu. Tuombe Serikali itoe ruzuku kwa dharura ili kupeleka katika pembejeo za kilimo na wananchi wetu waweze kupata pembejeo za kilimo kwa bei ndogo ambayo kila mkulima ataweza kumudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulikuwa tunanunua mbolea kwa shilingi 65,000 lakini bado kilikuwa ni kilio kwa wananchi. Leo ukienda Mkoa wa Songwe, mfuko wa mbolea unaupata kwa shilingi 120,000, jambo ambalo hakuna mkulima anayeweza kumudu gharama hizi. Lakini wakati huohuo ukienda sokoni mkulima anauza gunia la mahindi kwa shilingi 30,000 na kwa kanuni, ili ulime eka moja na uweze kuvuna mahindi ya kutosha ni lazima uwe na mifuko sita ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mkulima gani ambaye anaweza kumudu shilingi 720,000 kwa ekari moja tu; mkulima yupi wa namna hiyo? Hiki kitu hakiwezekani, hebu tuombe Serikali jambo hili mlichukue kwa udharura. Kwa wakati mwingine tunasema mioyo yetu inavuja damu maana tunajua hali za wakulima wetu huko mikoani hali ni mbaya mno. Na kuna wakati sisi kama Taifa tunapaswa kujifunza hata kwa nchi jirani ambazo zimetuzunguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda Zambia na Malawi bei za mbolea ziko chini kuliko Tanzania, lakini Malawi na Zambia wanajumua mizigo yao huko nje ambako ndiko na Watanzania tunakojumua na wanapitia katika Bandari ya Tanzania kwenda kwenye nchi zao lakini bei zao zipo chini. Hii inaonesha kwamba mrundikano wa kodi kwenye nchi yetu unawatesa na kuwaumiza wakulima wetu. Tuombe tuwanusuru wakulima wetu, lakini tunusuru uchumi wa Taifa letu; tuweke ruzuku katika pembejeo za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ninaomba kuishauri Serikali kama wengine walivyosema kwamba fedha zilitolewa zaidi ya bilioni mia moja ishirini na kwa ajili ya kununua mazao. Nataka kusema jambo hili kwa uchungu kabisa. Fedha hizi kwa asilimia kubwa hazijamgusa mkulima wa chini maana fedha hizi kwanza zimefika kwa kuchelewa lakini badala yake zimewagusa wafanyabiashara badala ya wakulima. Wakulima bado wana maumivu, bado wana kilio pamoja na Serikali kutoa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuombe kwa wakati mwingine fedha zitolewe kwa wakati ili ziweze kumlenga mkulima mdogo ambaye ndiye anayehangaika kule chini na anasota, fedha zitolewe kwa wakati. Na ninaamini tukifanya hivi tunaweza kumkomboa mkulima wa chini ambaye anataka kukwamuka kutoka hatua ya kwanza kwenda ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, ahsante. (Makofi)