Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa maoni yangu katika mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Arusha vilevile naomba niendelee kumpongeza Mama yetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuongoza kwa weledi mkubwa na vilevile kwa kuendeleza diplomasia ya kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuchangia kwenye sekta muhimu ya afya. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha huduma hizi za afya pamoja na maboresho yote yaliyofanyika bado kuna changamoto nyingi sana kwa wananchi wetu kupata huduma bora za afya. Changamoto hizi ni pamoja na gharama kubwa za afya kwa wananchi wetu, ubora wa afya wanaopata wananchi wetu na vilevile kupata kwa huduma za afya kwa wakati. Changamoto zote hizi suluhisho lake ni moja tu ni kuwapatia wananchi wetu bima ya afya kwa wote. Taarifa za kutoka Wizara ya Afya mpaka leo hii ni asilimia 12 tu ya Watanzania ambao wananufaika na huduma hizi za bima ya afya kwa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Kamati ilivyoshauri kwenye mapendekezo yake na mimi naomba niweke msisitizo kwa Serikali kutuletea Muswada wa Sheria wa Bima ya Afya kwa wote ili basi sheria hii iweze kwenda sambamba na Mpango wetu wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa na vilevile wananchi wetu waweze kunufaika na huduma bora za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile niweze kuchangia katika mwenendo wa riba za mabenki. Jana tulimsikia Mheshimiwa Waziri hapa akisema moja ya mafanikio ya sekta hii ya mabenki ni kushuka kwa riba kutoka asilimia 16.8 hadi asilimia 16.6, punguzo la asilimia 0.2 tu. Sisi kama wawakilishi wa wananchi hatuwezi kwenda kusema kwamba punguzo la asilimia 0.2 tu ni mafanikio ya sekta hii ya kibenki. Wananchi wetu bado wanateseka na riba kubwa za mikopo ya kwenye mabenki nasi Wawakilishi wao inabidi tufanye jitihada za makusudi kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumemsikia Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwenye hotuba zake nyakati tofauti akiagiza Benki Kuu ya Tanzania iweze kushusha riba hizi za mabenki hadi kufikia asilimia 10 au chini ya hapo. Asilimia 16.6 inayosemwa hapa hii ni wastani tu, bado kuna wananchi wengi wanakopa kwa riba ya zaidi asilimia 18. Natambua sana jitihada zinazofanywa na Serikali yetu kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka, wamesema wenzangu hapo ikiwemo mojawapo ni kupunguza kiwango cha chini cha akiba ambazo mabenki haya yanawekeza BOT yaani Statutory Minimum Reserve hadi kufikia asilimia Nane, lakini bado tumeona hili siyo suluhisho la kushusha riba za mabenki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Serikali yetu imetoa Shilingi Trilioni Moja imewapa Benki Kuu ya Tanzania ili kuweza kushusha hizi riba za mabenki, lakini bado tumeona siyo suluhisho pia ya kushusha riba hizi. Pamoja na hayo jitihada zote zilizofanywa bado tunaona ni punguzo la asilimia 0.2 tu ambayo bado sidhani kama tunaweza tukajisifia kuwa ni mafanikio ya sekta hii ya kibenki. Naamini Benki Kuu ya Tanzania pamoja na Wizara yetu ya Fedha inao wachumi wabobezi wengi na kwa pamoja wanaweza kushirikiana kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka kwa asilimia kubwa. Ili uchumi wetu uweze kuwa uchumi shirikishi na jumuishi lazima wananchi wetu waweze kwenda kwenye mabenki mbalimbali na kuwa na uwezo wa kukopa kwa riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti tuliweza kukutana na Umoja wa Mabenki ya Tanzania (TBA) na walitupa changamoto zao nyingi ambazo zinachangia gharama kubwa za uendeshaji wa mabenki na hivyo wao wanalazimika kuongeza riba katika mabenki yetu. Sababu nyingi walizotupa kati ya hizo kuna sababu mbili ambazo zipo ndani ya Wizara ya Fedha ambao wao wanaweza kuzitatua ili basi kuhakikisha riba hizi zinaweza kushuka kwa wanachi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu walizozitaja moja wanasema kupishana kwa sera kati ya Mamlaka ya Mapato ya Tanzania na Benki Kuu ya Tanzania, zote hizi ni Taasisi za Serikali naamini Waziri wetu hapa anaweza kukaa na taasisi hizi na kusuluhisha na kufanya riba za mabenki ziweze kushuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu nyingine waliyoitaja Umoja wa Mabenki, walisema vilevile ni kutokuwa na ushirikiano kati ya Mamlaka ya Serikali na mabenki ya biashara. Naamini pia hii sababu iko ndani ya Wizara ya Fedha, wanaweza kwa pamoja wakashirikiana na umoja wa mabenki haya ili basi watafute suluhisho la kushusha riba hizi za mabenki kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo pia namuomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hotuba yake aweze kutueleza hapa mikakati Serikali iliyonayo itakayofanya kwa ajili ya kushusha riba za mikopo kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)