Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango ulioletwa mbele yetu. Vilevile naomba nichukue nafasi hii kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwanza kwa kutoa bilioni 50 kwa ajili ya kunusuru soko la mahindi kwa wakulima wetu, limesaidia sana ingawa wakulima wale bado wanahitaji soko la kuuzia mahindi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza kwa kutoa shilingi trilioni 1.3 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo itasaidia kuongeza sana uhitaji na kuboresha maisha ya wananchi katika maeneo yetu. Naomba naomba nichukue nafasi hii nimpongeze Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Bajeti, Mheshimiwa Daniel Sillo kwa kuwasilisha taarifa nzuri pia niwapongeze wanakamati wenzangu kwa kuchambua hii taarifa na kuileta mbele ya Kamati yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuandaa taarifa pamoja na timu yake yote ya Wizara ya Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasimama hapa kuchangia draft ya mpango ulioletwa mbele yetu kwa ajili ya kujadili na kutoa maoni, kabla sijaanza kuchangia naomba nitoe masikitiko niliyonayo kwamba tunajadili mambo mengi, tumekaa karibu miezi minne kujadii bajeti ambayo iliisha tarehe 30 mwezi wa Sita lakini kulikuwana mipango mingi sana ambayo tuliipanga na kuijadili ukifanya tathmini ya utekelezaji wa kipindi cha robo mwaka katika taarifa ambayo tumeletewa sasa hivi ukurasa wa 16 kwenye utekelezaji wa robo mwaka ya bajeti inaonesha kwamba kwenye utekelezaji, bajeti ya maendeleo ya mwaka 2021/22 hakuna fedha zilizotolewa kwa ajili ya maendeleo kwenye upande wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, slogan yetu tunasema kwamba kilimo ni uti wa mgongo kwa Watanzania. Sasa unajiuliza kilimo cha Tanzania sehemu kubwa tunalima kwa kipindi kwamba tunategema mvua na ni sehemu chache sana ambazo anafanya umwagiliaji. Sasa unajiuliza sasa hivi ni mwezi wa 11 na wananchi wanajiandaa kuingia kwenye kilimo hawana mbolea ya kupandia, hawana mipango yoyote wakati huo tunategemea kwamba ni kilimo ni uti wa mgongo katika uchumi wetu. Sasa najiuliza huu uti wa mgongo utakuwa ni uti wa mgongo salama au hauna msaada katika maisha yetu Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo vilevile tumepata changamoto kubwa sana huko nyuma sasa nilitaka nione, kwa mfano nimepitia mpango ukiangalia kuna changamoto ambayo ilijitokeza inayohusiana na sumukuvu. Mpango wa Serikali na mikakati ni kujenga maghala na kuhakikisha kwamba tunaondoa hili tatizo la sumukuvu lakini kumbe sumukuvu inatakiwa katika mpango wetu tuangalie uwezekano wa kusaidia kuanzia kwa wazalishaji ili ku-trace ile sumukuvu ni sehemu gani ambayo unatakiwa uisimamie. Kwa sababu ninachofahamu kwa uzoefu wangu sumukuvu wakati mwingine inatokana na ubichi au wakulima wanavuna mazao mabichi na kuyaweka kwenye maghala matokeo yake yanasababisha sumukuvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika mpango wetu naomba uboreshwe, uwekwe mkakati ambao utasaidia kuondoa sumukuvu kuanzia kwa wakulima.

Vilevile nilipopitia mpango sijaona mkakati ambao umewekwa wa dharura kuhakikisha kwamba wakulima hawa wanasaidiwa kwenye suala la pembejeo. Suala la pembejeo ni kizungumkuti. Sasa hivi hatuna taarifa yoyote ile ya mbolea na hatuna taarifa ya kwamba mbolea hizi hata kama zitapatikana zitauzwa bei gani kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu ni kwamba mpango utakapokuja uboreshwe, uoneshe kwamba bei za mbolea pamoja na pembejeo zingine ziwe zimeshuka kwa kiwango kikubwa ikiwezekana iwe sawa na bei ambayo wakulima wetu walinunua mwaka jana ili iweze kuwasaidia katika uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa kilimo utakuta mpango wetu haujaonesha muunganiko uliopo kuanzia kwenye uzalishaji, kwenye masoko na viwanda. Kwa mfano, sasa hivi tunaweka mikakati mingi sana ya kuhamasisha uzalishaji wa michikichi lakini mpango haujaonesha kwamba sasa hii flow ya uzalishaji, masoko pamoja na suala la viwanda kwa ajili ya kuchakata hiyo michikichi ambayoo tunaiandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisisitize sana kwenye upande wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawekeza kwa kiasi kikubwa sana kwenye upande wa kilimo ili kuwasaidia wakulima wetu kuondokana na mazingira magumu ambayo yapo ili kuhakikisha kwamba tunaongeza uzalishaji. Kwa hiyo, kwenye hilo nategemea kwamba mpango utakapokuja kama walivyoshauri wenzangu tuhakikishe kwamba Serikali inaweka subsidies kwenye pembejeo pamoja na mbolea za aina mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika mikakati yetu tuliweka hoja ya kuhakikisha kwamba Serikali inapima udongo. Kwenye upimaji wa udongo nilikuwa nashauri mpango uangalie uwezekano wa kuweka maabara za upimaji wa udongo kwenye kila Mkoa ili tuweze kuwasaidia hawa wananchi kuweza kupima udongo na kupata mbolea ambazo zitakwenda sambamba na udongo uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumeweka mikakati mingi sana na mipango mingi ya maendeleo lakini tumeangalia kwenye masuala ya maji, masuala ya kilimo, ufugaji na miundombinu mbalimbali lakini nilikuwa naomba mpango unapokuja baada ya kuboresha uangalie ni namna gani tunaweka mikakati ya kusimamia kwenye suala la mazizngira ili kuhakikisha kwamba hii miradi yetu ambayo tunaitekeleza kwa kutumia fedha nyingi za Serikali iweze kuwa himilivu kwa kipindi kirefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe mchango wangu kwenye suala la madeni. Kwenye mpango tumeonesha kwamba kuna madeni mbalimbali ambayo Serikali inadaiwa lakini nataka nijikite kwenye suala la madeni ya ndani. Madeni ya ndani kuna madeni ya wafanyabiashara na kuna madeni ya wakandarasi, kuna kipindi Serikali ilikuwa inafanya uhakiki wa madeni ya wafanyabiashara ambao walisambaza mbolea na pembejeo mbalimbali kwa wakulima wetu. Takribani sasa ni zaidi ya miaka mitano wafanyabiashara wale hawajalipwa chochote, kila siku wakiuliza wanaambiwa kwamba uhakiki bado unaendelea na ninaona kwamba wale wafanyabiashara wameingia kwenye matatizo magumu na wana hali ngumu kwa sababu wana madeni mengi ya kwenye benki mbalimbali na wanashindwa kulipa yale madeni kwa sababu madeni yao bado hayajahakikiwa.

Kwa hiyo, naomba sana kwenye mpango utakaokuja uhakikishe kwamba unasimamia na unaweka mikakati ya kuhakikisha kwamba tunawalipa wale wadau mbalimbali ili kuondoa adha ambayo inawakabili. Nakushukuru sana. (Makofi)