Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii jioni ya leo nami nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Afya. Awali ya yote, nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kusimama hapa katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile napenda kutoa shukrani za dhati kwa wapiga kura wangu, Wanaliwale kwa kunikabidhi jukumu hili la kuwawakilisha na sasa hivi ndiyo hiyo kazi naifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naanza kuwaasa ndugu zangu wa Kambi yetu ya Upinzani. Kambi ya Upinzani ndiyo tuliopewa jukumu la kuishauri Serikali. Serikali hii wanasikia na wanatuelewa. Wenzetu waliobaki kule nyuma, wamepewa kazi ya kushangilia na kupitisha. Sisi ndiyo tunatakiwa tuishauri hii Serikali. Hii Serikali siyo kwamba hawasikii, tatizo la Serikali yetu ni kwamba wako nyuma sana na wakati. Mliwashauri hapa mwaka 2010 kwamba safari za Mheshimiwa Rais hazina tija; Mwaka 2015 wametekeleza; mkawashauri mwaka 2010 kuhusu ufisadi, mwaka 2015 wametekeleza; tatizo ni muda gani wanautumia kuyatekeleza haya tunayowaambia? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzuri wa kusema ni kutazamana, ndiyo maana sisi tumetazamana na Mawaziri, wale wako nyuma, kwa sababu wanajua nini tunaongea. Nataka niwape faida moja; tunapochangia Upinzani na Mawaziri wako busy kuandika, kwa sababu wanajua sasa ndiyo wanashauriwa, kule wanasubiri kushangilia na kupitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa narudi kwa mabosi wangu, Wanaliwale, naomba niwawakilishe. Wilaya ya Liwale ni Wilaya iliyoasisiwa mwaka 1975 na mwasisi wa Wilaya ile ni Waziri Mkuu wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Rashid Mfaume Kawawa. Nakuja kwenye upande wa hospitali; sasa bahati mbaya ya wilaya ile, ina vijiji 76, tuna zahanati 30 tu. Wilaya ya Liwale ina kata 20, tuna kituo cha afya kimoja, mfu. Nasema kituo mfu kwa sababu ni mwaka wa tatu huu, vifaa vimekwenda pale vya upasuaji, viko kwenye maboksi mpaka leo. Havijafunguliwa, mchwa wanakula yale maboksi. Nimeyaona haya kwa macho yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Wilaya ya Liwale ina magari mawili ya wagonjwa; gari moja ndilo ambalo anatumia DMO kama gari la kufanyia kazi na gari moja ndiyo linalotumika kama la kusaidia wagonjwa. Bahati mbaya nyingine ya Wilaya ya Liwale, Mji ule upo; sijui nani anamjua pweza! Barabara zetu ziko mkia wa pweza, kwamba hatuunganishi kutoka kata moja kwenda nyingine, ni mpaka uende urudi, uende urudi. Nakupa mfano wa vijiji vichache vifuatavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Nahoro kwenda Liwale ni kilomita 135, Napata - Liwale Kilomita 120, Liwale - Lilombe Kilomita 65, Kikulyungu - Liwale Kilomita 120. Hawa wanatembea hizo kilomita 120, kufuata huduma Liwale Mjini. Wakifika Liwale Mjini, hospitali yenyewe ndiyo kama hiyo, takwimu hizo nilizokupa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale kwenye zahanati zetu 30 zinahudumiwa na wale mnaita one year course…
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Medical attendant wa one year course ndio wanaohudumu kwenye hizi zahanati. Kichekesho, nimekwenda na DMO kwenye baadhi ya zahanati, tumekuta dawa zimeharibika. DMO anasema hizi dawa zimeharibika kwa sababu hawa wahudumu hawazijui. Wanataka panadol zilizoandikwa panadol. Ukibadilisha boksi siyo panadol hiyo. Hili ni tatizo!
TAARIFA
MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Kuchauka keti kidogo....
MWENYEKITI: Mheshimiwa Zuberi unaikubali taarifa au unaikataa?
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Taarifa yake naikataa, kwa sababu zifuatazo: Waziri Mkuu wa kwanza Tanganyika huru ni Mwalimu Nyerere, lakini Waziri wa Kwanza wa Tanzania ni Mzee Kawawa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee Kawawa ni Waziri Mkuu wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, uwezo wake wa kuifahamu historia haiwezi. (Kicheko/Makofi)
MWENYEKITI: Endelea!
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Hiyo ni historia fupi tu ameshindwa kuielewa. (Makofi/Kicheko)
MWENYEKITI: Endelea Mheshimiwa na kiti kinakulinda, uko sahihi! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu Waziri wa Afya, watu wengi wamewasifia na wanaendelea kuwasifia, nami naendelea kuwasifia, lakini nawapa pole. Nawapa pole kwa sababu jukumu mlilonalo ni kubwa, mazingira ya kazi ni magumu, kwa bajeti hii kwa kweli dhamira yenu ni nzuri, nami nataka niwaambie kwamba ili muweze kuonekana angalau mmetekeleza kidogo, mnahitaji kufanya kazi ya ziada. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama takwimu zinavyosema, bajeti ya Serikali imeongezeka kwa trilioni sita point something, lakini bajeti ya Afya imepungua kwa asilimia 11. Sasa mwone hiyo kazi mliyonayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narejea kule kule Liwale. Liwale sisi tunayo matatizo, sisi tuna upungufu wa Clinical Officer 40. Mheshimiwa Waziri atakapokuja naomba anieleweshe, hivi DMO anaruhusiwa kutibia? Anaruhusiwa kuingia ofisini kutibu watu? Maana DMO wangu yeye ni mtawala, hajawahi kuingia ofisini kutibia. Sasa sijaelewa, mimi kwa sababu siyo mtaalam sijaelewa. Hapo mtakapokuja, mtanielewesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, jiografia ya Wilaya ya Liwale kiutendaji kuwa na gari moja la wagonjwa ni tatizo. Gari lile likiondoka, watu wengine huku nyuma hawana usafiri tena na ni kilomita kama hizo nilizokupa. Liwale hospitali ile, mimi nimeingia haina X-Ray mwaka mmoja uliopita.
Namshukuru Naibu Waziri, nilikwenda ofisini kwake akanisaidia, akanipa njia ya kupata mtaalam, nikampata mtaalam nikapeleka X-Ray ile ikatengenezwa. Kama Waswahili wanavyosema, “Siku ya Kufa Nyani, Miti yote Huteleza.” Ile X-Ray sasa hivi ni nzima lakini haina mhudumu. Mpiga picha hatuna, kwa hiyo, tumerudi pale pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya ya Liwale haina ultrasound. Mwezi Januari kuna dada mmoja alikwenda pale kwa lengo la kujifungua, wale akinamama wakaenda kumpima, wakampapasa wakamwambia njoo wiki ijayo. Wiki ijayo yule mama hakufika, tumbo likawa la njano wamemrudisha pale yule mama kafa. Hospitali ya Wilaya ya Liwale!
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wanamwambia Mheshimiwa Waziri, njoo kwetu, njoo kwetu, mimi sisemi aje Liwale; naomba atusaidie Liwale. Akiona namna ya kuweza kuja, karibu Liwale, aje ajionee haya ninayoyasema. Ile Wilaya imesahauliwa, ni ya siku nyingi, lakini ukienda ukiiangalia utafikiri ni Wilaya ambayo imezinduliwa juzi. Hayo ndiyo matatizo tuliyonayo Wilaya ya Liwale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati napita kuomba kura niliwaambia, sitakubali kuona akinamama wakienda kujifungua wanakwenda kama wameachika; anakwenda na beseni, ndoo, carpet; maana hizi mackintosh wao hawana, kule wanatumia hizi carpet za kawaida. Anakwenda na carpet, ndoo, beseni, wembe, kanga, gloves na sindano. Nikasema sitalikubali hilo. Kwa kuonesha mfano huo, nimepeleka, mackintosh 5,000 mwezi uliopita. Nimeona nianzie hapo, lakini hali yetu ni mbaya, tunaomba msaada wenu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye upande wa MSD. MSD ni tatizo jamani. Nakumbuka siku moja tulikwenda MSD nikiwa kwenye Kamati ya UKIMWI; yule Mkurugenzi alituambia kwamba tatizo la Halmashauri wanatupa order haraka. Wanatupa order leo, kesho wanataka hela, lakini hii siyo kweli. Sisi Liwale tumepeleka pesa Desemba, shilingi milioni 35. Dawa tulizopata mpaka leo ni za shilingi milioni 20, inaonekana dawa tulizopewa siyo zile tunazozihitaji. Tumepewa dawa zile ambazo MSD wanazo. Mkurugenzi alisema kwamba mkileta pesa, baada ya wiki mbili au wiki tatu mtakuwa mmepata, lakini hii siyo kweli. Huo ndiyo ukweli halisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye CHF. Tarehe 8 Januari, Mkoa wa Lindi ulizindua CHF Kitaifa na mimi mwenyewe nimechangia watu 100 kwenye Jimbo langu, lakini CHF imenitia kitanzi, kwa sababu nimehamasisha Wanaliwale, kabla ya uzinduzi tulikuwa asilimia 10 ya wanajamii wa Liwale, lakini mpaka namaliza tarehe 30 Aprili, tulikuwa tayari tumefika asilimia 46.4 na nikawaahidi Wanaliwale, kufikia Agosti tukiuza ufuta tunataka tusahau masuala ya CHF. Tunataka tuchangie asilimia mia moja. Sasa hiyo imenitia kitanzi. Imenitia kitanzi mimi na Madiwani wangu kwa sababu tuliwaambia, mkienda dirishani mkikosa dawa, njooni kwetu. Sasa vyeti vyote vya dawa vinakuja kwetu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti vyeti vyote vya dawa vinaenda kwa Diwani, vinaenda kwa Mbunge kwa sababu tuliwaahidi mtoe pesa mtapata dawa; dawa hazipo! Tunawaomba Mheshimiwa Waziri, CHF inatutia kitanzi. Nashukuru mwenzangu Mheshimiwa Bobali aliona mbali, akawaambia wasichange kabisa. Sasa mimi nimeji-commit kwamba tunachanga na kweli wananchi kwa sababu wananikubali, nikiwaambia wanatekeleza. Mwezi Agosti Mheshimiwa Waziri alituahidi tutakuwa tumefikia asilimia mia moja. Naomba Mheshimiwa Waziri, mnitoe kwenye hiki kitanzi. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye hivi mnasema Vituo vya Saratani ya Mlango wa Kizazi. Lindi kuna vituo vinne, Liwale hatuna. Hivi Liwale kuna nini? Jamani, tuoneeni huruma, hata Mzee Kawawa hamumwenzi, simba wa vita! Jamani nawaombeni mtukumbuke na sisi tumo. Kwenye mchango wetu, pato la Taifa tumo! Tunalima korosho kwa wingi, tunalima ufuta kwa wingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kwenye masuala ya UKIMWI sasa, nakuja kwenye masuala ya UKIMWI. Takwimu zinaonesha wanaotumia dawa za ARV mpaka mwaka 2015 ni watu 700,000 na inakadiriwa mpaka mwisho wa 2016, wanafika watu 900,000, lakini pesa iliyotengwa ni ya watu 200,000. Maana yake mpaka sasa hivi tunasema watu 500,000 hawana dawa. Hiyo ni takwimu sahihi kabisa zinazohusiana na mambo ya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba Mheshimiwa Waziri hili suala la UKIMWI tulipe kipaumbele. Kama kweli dhamira yetu ni kuwasaidia watu wetu, hili suala la UKIMWI tulipe kipaumbele. Vile vile narudi tena kwenye upande wa MSD. MSD hata hizo dawa chache wanazozileta, kwa jiografia ya Liwale na Mkoa wa Lindi ha… (Makofi)
MWENYEKITI: Basi.
MHE.ZUBERI M. KUCHAUKA: Nashukuru kwa kunisikiliza.