Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

MHE. RIDHIWANI J. M. KIKWETE - MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waheshimiwa sana Mawaziri, Wabunge wenzangu, wageni waalikwa, Mabibi na Mabwana na mimi kwanza nianze kwa kushukuru kwa sababu mwanzo nilikuwa natoa salamu za jumla za Kamati, lakini sasa nimepata nafasi ya kutoa maazimio au majumuisho, naomba nikushukuru wewe binafsi kama walivyotangulia wenzangu kusema, kwa kunipa nafasi na mimi kuwa mmoja kati ya Wajumbe wa Kamati hii ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, kwa hakika sio tu kwamba, nimeendelea kujifunza kama mwanasheria, lakini pia imenipa nafasi ya kuendelea kujua Tanzania na sheria ambazo zinaendelea kuhitaji marekebisho au uangalizi wa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia natambua kwamba michango iliyotolewa na Wabunge mbalimbali, Wabunge 14; lakini pamoja na hao pia ameongea Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na Sera, Vijana na Walemavu ameeleza naye katika hayo mambo yake. Lakini pamoja na hilo pia, niishukuru Serikali kwa kukubali kuchukua yale yote yaliyopendekezwa na Kamati yetu na kwenda kuyafanyia kazi. Lakini kwa umuhimu zaidi niwashukuru pia wachangiaji wote, kwa michango yao mizuri iliyolenga kuboresha taarifa yetu na kuifanya taarifa hii sasa iwe taarifa ya Kibunge, iwe na sifa za kuitwa taarifa ya Kibunge, lakini pia iwe taarifa ambayo inatosha katika maudhui yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mambo ambayo yameelezwa na mimi napenda niyasisitizie ambayo kwangu kama mtoa hoja, ni vyema nikayapazia sauti ili Serikali iweze kuyachukua katika uzito wake.

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa ambalo tumelizungumza ndani ya Kamati, lakini pia kutoka kwenye michango ya wajumbe wa Bunge lako, ni juu ya huu mtazamo ambao upo wa baadhi ya watu kutunga Sheria, ambazo zimekuwa kandamizi sana. Mheshimwia Waziri na Mheshimiwa Attorney General ni ukweli kwamba haya mnaenda kuyafanyia kazi, lakini kiukweli sheria zetu bado haziendelei kufurahisha watu wengi na hivyo kwenu ninyi kuchukua na kwenda kuyafanyia kazi ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, yameibuka hoja hapa ya ile ya bajaji ya kutozwa mpaka shilingi 200,000 kwa faini, kwa ajili ya wrong parking. Mheshimiwa Waziri mhusika ningeomba utoe maelekezo kwa Halmashauri zako na ikiwezekana utaratibu mzuri uwekwe, ikiwezekana kwamba sheria hizi kabla hazijaanza kufanya kazi basi Bunge hili liweze kuzipitia. Tofauti na sasa ambazo zinafanya kazi kwanza halafu baadaye, ndio Bunge linakuja kuziangalia kama zimefuata utaratibu au hazijafuata utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia limezungumzwa jambo hapa la vijana kuwa wanaminywa katika ajira. Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Attorney General, ndugu Wabunge wenzangu, jambo la ajira limekuwa ni kilio kikubwa cha muda mrefu, kama sisi Wabunge hatutakisimamia hiki katika ile dhana ambayo, Rais wetu mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan anataka vijana wapate ajira, sio tu katika zile ajira zilizo rasmi zinazotangazwa Serikali, lakini pia katika mazingira wanayoishi hatutoweza kufanikiwa kama jambo hili halitoangaliwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini naishukuru Serikali imesema jambo hili inalichukua na kwenda kulifanyia kazi ili liweze kuwa jambo ambalo linakwenda kutatua kero hizi. Lakini hili liende sanjari na lile jambo la ile Sheria ya Filamu ambayo nayo imelalamikiwa sana na wajumbe wengi wameipazia sauti ili kuweza kuweka sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ipo sheria nyingine ambayo imeonekana kwamba ni inaweza ikasababisha shughuli za kihalmashauri zisifanyike vizuri. Hiyo sheria inatambulika kama Sheria ya Kukusanya Ushuru ambayo sisi kwenye taarifa yetu tulionesha hiyo taarifa ya Same, lakini ndugu au Msomi Mheshimiwa Tadayo akaelezea juu ya pia taarifa nyingine inayofanana na hiyo ya kule Mwanga.

Mheshimiwa Spika, niombe Serikali iliangalie jambo hili vizuri, tukifanya mchezo Halmashauri zetu zitakosa vyanzo vya mapato na kwa kukosa mapato huko kutapelekea shughuli zetu baadhi yao zikwame. Sisi leo ndani ya Chalinze kwa mfano, moja ya chanzo chetu kikubwa ni mapato yanayotokana na kokoto. Kama ukitunga Ssheria ukasahau chanzo hiki cha mapato maana yake ni kwamba Halmashauri ya Chalinze itaingia katika mgogoro mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, jambo la kufundisha wataalam wetu ili wawe waandishi wazuri hili ni jambo ambalo lazima lipangiwe mkakati ili liwe jambo endelevu lakini liweze kusaidia halmashauri zetu kuweka mikakati vizuri na waandishi wetu waweze kuwa wamejengewa weledi ulio mzuri.

Mheshimiwa Spika, nimezungumzwa jambo lingine hapa la watunzi au waandishi wa sheria kutozingatia misingi ya Katiba. Katika jambo lililo muhimu ambalo sisi pamoja na wewe Spika wetu, tuliliahidi mbele ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni ulinzi wa Katiba yetu. Bila kulinda Katiba sisi ambao ndio watunzi wa sheria hizo tutakuwa ndio kituko na kichekesho cha kwanza katika nchi hii. Tusikubali Bunge lako ligeuzwe kuwa sehemu ya kuponda na kuvunja Katiba hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia kuendelea kukumbushana Wabunge wenzangu ambao pia ni Madiwani kwamba tusiache mambo yakaendelea kule kwenye Halmshauri zetu bila sisi kushirikishwa. Maana yapo mambo mengine haya tunaweza kuyamaliza kule majimboni kwetu au kwenye maeneo yetu kwa sisi kufuatilia mara kwa mara. Kitendo cha sisi kukaa huku Bungeni kisiwe kisingizio cha kupitishwa kwa mambo ndani ya halmashauri zetu bila kushirikishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia nikushukuru Mheshimiwa spika kwa maelekezo yako uliyoyatoa na hadithi uliyotupa hapa ya kweli juu ya wale vijana ambao wamejiajiri wenyewe na tabu wanayoipata, kwangu mimi hili sio tu kwamba ni maelekezo labda kwa Kamati au kwa Serikali lakini pia kwetu sisi sote kama Wabunge tujaribu kusimamia sheria hizi ili kutatua kero hizi ambazo zinakwenda kukabili vijana wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la rumbesa limezungumzwa hapa, hili jambo nadhani kwa yale maeneo au Halmashauri ambazo zina sheria hizi hebu tuziangalie tena vizuri ili tuweze kuweka mambo yetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho katika michango hii, nizungumzie mchango mzuri uliochangiwa na Mbunge Ndugu Neema Lugangira juu ya Asasi zisizo Kiserikali na zile ambazo zinafanya kazi katika jamii yetu. Kamati imesikia juu ya matatizo makubwa yaliyopo katika Kanuni hizi zinazokabili NGOs na CSOs kwangu mimi kwa kuwa mamlaka ya kuita kanuni hizi unayo wewe na Kamati yako imeendelea kufanya kazi kwa maagizo yako, tukuombe kupitia Kanuni yako, kupitia Katiba inayokupa nguvu wewe, uielekeze Serikali ituletee Kanuni hizo na sisi kama Kamati tupo tayari kwa ajili ya kuziangalia ili NGOs, CSOs na Asasi nyingine ziende kufanya kazi katika utaratibu tuliokubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia niwaambie tu ndugu zagu wa NGOs na CSOs kwamba kuja kwa kanuni hizo sio kwamba tunapata tiketi ya uvunjivu wa kanuni, hapana. Kamati itaangalia vizuri na kujiridhisha juu ya yale ambayo yanalalamikiwa na baada ya kujiridhisha mapendekezo yetu yatakuja hapa katika Bunge ili ninyi Bunge muweze kuamua katika haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeniambia kwamba unanipa dakika 20; lakini dadika 20 katika maana ya kufunga hoja kwangu mimi ni nyingi sana. Ningependa kutumia nafasi hii ya mwisho; kwanza kumshukuru kabisa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya, kazi ambayo kwa hakika inaigwa katika dunia nzima. (Makofi)

Tumeshuhudia ndani ya siku zake 100 kupitia hotuba ya Waziri Mkuu aliyoisema jana pale Dar es Salaam, akieleza kwamba Mama Samia amekwisha fanya na kuendelea kukamilisha miradi zaidi ya 73 ambayo inafanywa kwa fedha za ndani na nyingine kutoka katika fedha za wahisani ambayo inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia tumeshuhudia Mama Samia Suluhu Hassan katika akitimiza kwa vitendo nia yake nzuri ya kuhakikisha kwamba mazingira mazuri ya biashara yanaendelea kuimarika katika nchi yetu. Amefanya vikao zaidi ya viwili, akishirikiana na Waziri Mkuu na Makamu wetu wa Rais na Mawaziri wetu na tumeshuhudia nia yao nzuri ikianza kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia nimpongeze sana Mama yetu Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hakika ameanza vizuri sana kazi yake ya kutimiza ndoto za Watanzania. Sisi kama Kamati ya Sheria Ndogo au sisi kama Wabunge tunaendelea kumuunga mkono na niwaombe Wabunge wenzangu tuendelee kumuunga mkono mama yetu akitimiza nia nzuri ya kuhakikisha kwamba nchi yetu inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini siyo mwisho kwa umuhimu wake, niishukuru pia familia yangu; katika kipindi cha miezi miwili/mitatu ambayo tumekaa Bungeni hapa, tumekuwa mbali na familia lakini wanangu wamekuwa wananipigia simu wakinishukuru, wakinipa moyo na kunifariji, mke wangu amekuwa anafanya hivyo na kwangu mimi imekuwa ni faraja kubwa sana hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia leo asubuhi umewatambulisha rafiki zangu wawili; nisingependa jambo hili nichukue muda sana lakini kwa upekee uniruhusu nifanye hivyo; amekuja rafikii yangu mmoja hapa anaitwa Azizi. Azizi kwa taaluma yake yeye kinyozi, ni mtu ambaye ukimuona utamuona ni mtu mdogo sana, lakini Azizi ndiye ambaye anafanya mimi na wenzangu wengine tunapendeza na kuonekana hivi tulivyo. (Makofi)

Amekuja hapa nimemualika na ni mgeni wangu, nataka mjue ndugu zangu Wabunge wenzangu kwamba kuna umuhimu wa kwamba chamber hii kama alivyozungumza Mheshimiwa Spika ikawa chamber ya kila mtu. Siyo tualike tu wale wapiga kura wetu wa Katibu, Wenyeviti, Madiwani hapana na watu wengine ambao wanafanya Maisha yetu yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hilo pia yupo rafiki yangu Dkt. Mwinyi; Dkt. Mwinyi amekuwa ananisaidia sana, mimi kama alivyozungumza mama yangu Waziri Jenista Mhagama mimi bado nasoma pia, nipo UDOM hapo nasoma na ile ndoto ya Mama Jenista Mhagama huenda siku moja ikawa kweli na mimi nikawa Daktari. (Makofi)

Nakushukuru na ninaamini kabisa maneno yako hayawezi kuanguka na amekuwa msaada mkubwa sana Dkt. Mwinyi akinisaidia kuhakikisha kwamba na mimi natimiza ndoto za kuwa Daktari siku moja, lakini kuwa katika jamii ya vijana ambao ni wasomi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa maana siasa tuna mwisho kabisa, tuna mwisho kwa umuhimu kwa umuhimu wake; mwisho kabisa niendelee kukushukuru wewe kwa kunipa ruksa hii. Umenipa nafasi kubwa ya kuhudumia katika Kamati hii na mimi binafsi yangu namshukuru tena Mwenyekiti wangu Dkt. Rweikiza kwa nafasi kubwa aliyonipa ya kuja kusoma mbele yako, lakini pia ruksa hii inatupa nafasi na sisi ya kutokuwa na woga tunaposimama mbele yako. Maana hapa panatisha, lakini kwa kipekee nikushukuru wewe pamoja na Wabunge wenzangu tuendelee kupeana ushirikiano. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)