Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima, lakini pia nikushukuru wewe, kwanza kwa nafasi hii uliyonipatia ya kuchangia hoja hii ambayo imewasilishwa kwa umaridadi mkubwa na Makamu Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete. Lakini pia nikushukuru kwa kuamua kiniteua kuhudumu katika hii Kamati ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama wenzangu waliotangulia, mimi pia kwa taaluma yangu ni mwalimu, nilipoona nimepelekwa kwenye Kamati ya Sheria Ndogo nilishtuka kidogo nikasema sasa huku Mheshimiwa Spika amenipeleka nikafanye nini?

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya kuanza kufanya kazi mule niligundua ulinipa jukumu nyeti, kubwa na ambalo linahitaji umakini na muda. Kwa sababu mambo mengi yanayoendeshwa kwenye nchi hii yanaendeshwa kwa utaratibu wa kanuni na sheria ndogo ambazo sisi kwenye Kamati yetu ndiko tunakozipitia. Kwa hiyo nakushukuru sana kwa nafasi hii na ninakuahidi nitafanya kazi kwa nguvu zote na weledi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaenda kwenye vitu mahususi, niliomba kushauri kidogo, nadhani katika uwasilishaji tumeona katika muda huu mfupi tu kuna sheria ndogo zaidi ya 915. Hizi sheria ndogo zote zinaathiri maisha ya watu wa chini huko, zinapitishwa na mamlaka mbalimbali zilizokasimiwa na Bunge kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Spika, lakini katika sheria chache ambazo tumezipitia tumegundua mapungufu makubwa sana. Kuna mapungufu ambayo ukiyaangalia tu unasema hawa watu wakati wanatengeneza hizi sheria walikuwa wamejifungia wapi.

Kwa hiyo, kama alivyomalizia Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda wakati anamaliza mchango wake, mimi mwenyewe nimeona lipo hitaji la Kamati ya Sheria Ndogo kupata muda zaidi wa kupitisha sheria ili kupunguza kero tunazokutana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini kama sheria iliyopeleka zao la choroko na dengu kwenye Stakabadhi Ghalani ingeanzia kwenye Kamati ya Sheria Ndogo, wala tusingekuja kutoa maelekezo hapa Bungeni kuwaambia Wizara kwamba waandike waraka mwingine wa kwenda kuviondoa kwenye Stakabadhi Ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ambacho mimi nimekigundua katika muda mfupi kwenye Kamati hii, inawezekana kwenye maeneo mengi tunapeleka watu ambao hawayajui hayo maeneo kwenda kuyatengenezea sheria ndogo. Kwa sababu ninaamini, kwenye maeneo kama ya – tulikuwa tunaangalia hapa Sheria ya Bodi ya Filamu, kwamba mtu anakwenda kutengeneza kanuni za filamu, mtu ambaye kwenye maisha yake hata filamu kuiangalia huwa haiangalii, lakini anakwenda kuwatengenezea watu wanaoangalia filamu na watu wanaofanya maigizo kanuni pale.

Kwa hiyo, ipo haja ya Kamati hii kupata muda wa kutosha ili kuweza kuzipitia sheria hizi, naamini ofisi yako italiangalia hili.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi naomba nijikite kwenye baadhi ya mambo, lakini kitu cha msingi kabisa ambacho nataka nikiangalie, kuna sheria nyingi ndogo na kanuni ambazo zinatengenezwa zinakuwa hazikidhi uhaliasia wa mambo.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo wachangiaji awali wamechangia, unakuta sheria imetungwa lakini ukiangalia uhalisia wake, nilikuwa naangalia Sheria Ndogo ya Jiji la Mbeya ambayo naamini ilitungwa huko nyuma, sasa imekuja kuanza kazi sasa, iliyokuwa inasema kwamba kila bajaji ilipokuwa inatoka stand inatakiwa illipe shilingi 1,500. Unajiuliza huyu mtu aliyetunga hii sheria alikuwa amejifungia wapi? Yaani bajaji kila ikitoka stand shilingi 1,500. Yaani hii unakuta kabisa hawa watu ukiangalia, wakati huo kuna daladala wanalalamikia zile bajaji.

Kwa hiyo, mimi naamini wale daladala wanakwenda kuhonga wale au inawezekana kuna mtu aliyekuwa anatunga hizo sheria labda ana daladala ili afanye kabisa bajaji zisiingie stand, kwa sababu bajaji ikibeba watu labda wa shilingi 500 kila mtu kwa watu watatu ina maana yeye bajaji anakuwa kazi yake ni kulipwa na kulipa ushuru. Hakuna kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ilinishtua lakini nilipofuatilia na kwa faida ya Bunge hili, kwa sababu Mheshimiwa Naibu Spika ni Mbunge wa Mbeya, lakini ukiangalia, hii sheria imetungwa bado Mheshimiwa Naibu Spika hajawa Mbunge wa Mbeya. Inawezekana walijua watashindwa, kwa hiyo wakaona watengeneze sheria ambayo itakuja imfanye Mbunge anayekuja afanye kazi kwa ugumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ukiangalia sheria hizi zinapotengenezwa, ni lazima watu wanaozitunga wawe wana…

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kasalali, inaelekea ilitungwa wakati ule CHADEMA ndio wanaongoza Jiji, eh?

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa.

SPIKA: Mheshimiwa Cecilia nimekuona umesimama.

T A A R I F A

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba utungaji wa sheria haumlengi mtu, utungaji wa sheria yoyote, ama sheria mama au sheria ndogo, unalenga utekelezaji wa jambo fulani kwenye jamii uweze kufanikiwa. Kwa hiyo, jamii yoyote inayolengwa, haijalishi ni CHADEMA, CCM au asiyekuwa na chama, mkristo au mpagani, vyovyote vile, inalenga jamii kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na wanaoandaa sheria ndogo hizi wengi ni watendaji wetu kwenye ofisi zetu za Serikali. Kama mchakato unaanzia kwenye ngazi za kata, vijiji, inapanda kwa mfumo wa…

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninataka nimpe hiyo taarifa. (Makofi)

SPIKA: Yaani alichokuwa anasema ni kwamba sheria hii ilitungwa kipindi kile ambacho Meya na Madiwani wengi wa Jiji la Mbeya walikuwa ni wa CHADEMA; ndicho alichokuwa anasema. (Makofi)

Mheshimiwa Kasalali, sijui kama ulimaanisha hivyo?

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, hii taarifa niliyopewa ngoja niendelee kuwa nimepewa, lakini mimi kitu cha msingi ambacho nilikuwa nataka kukieleza ni kwamba Baraza la Madiwani lililopita la Halmashauri ya Jiji la Mbeya ndilo lililoshiriki kutengeneza sheria hii ndogo ambayo ilikuwa inawakandamiza waendesha bajaji na bodaboda wa Jiji la Mbeya ambayo sisi wakati tunajadili kwenye… (Makofi)

SPIKA: Bahati mbaya muda umekwisha.