Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi ya kuendelea kufanya kazi ya kulitumikia Taifa letu kupitia Bunge lako hili na pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi, na zaidi ya yote, kuniteua na mimi kuwa miongoni mwa Wabunge wanaounda Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilipata shida kidogo, mimi taaluma yangu ni mwandishi wa habari, nilipopelekwa kwenye sheria ndogo nikasema sasa inakuaje hii? Lakini kumbe ulikuwa unanipeleka shule nyingine ya kujifunza ili niweze kujua mambo mengi zaidi, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadhi ya Wanakamati wenzangu wametoa hoja nyingi za mambo ambayo tuliyapitia na kwa kweli niseme waraka huu ulioletwa na Kamati yetu mbele ya Bunge lako, tumefanya uchambuzi wa kutosha na kusaidiwa vya kutosha na wataalam tuliowashirikisha na wadau tuliowaita kwenye vikao vya Kamati na kwa maana hiyo nataka niseme tulijikita kwelikweli kuangalia na kufanya uchambuzi ili tuone namna nzuri ya kulishauri Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, nifanye mapitio madogo tu katika baadhi ya mambo ambayo wengine inawezekana wamekwishayataja; kwa mfano, tumejadili sana kuhusu sheria ndogo zinazoongoza masuala ya filamu. Na katika kujadili sana, kwa sababu yalikuwa ni mambo ambayo katika sura na tamaduni za kwetu bado ni mambo ambayo hayajazoeleka sana kwa Watanzania, hii tasnia ya filamu haijachukua kasi kubwa sana kama nchi za wenzetu. Kwa maana hiyo kuna mambo ambayo tuliyakuta yamewekwa kwenye mapendekezo ya sheria ndogo ambayo yalikuwa yananyima uhuru tasnia yenyewe kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kikubwa ni kwamba kama mtu anataka kuonesha kitu juu ya tatizo la dawa za kulevya, lazima aoneshe, lazima awepo mtu anayeonesha hizo dawa za kulevya yanatumiwaje na yanaathiri vipi. Lakini mwisho lazima matokeo yake yaoneshe madhara.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, haiwezekani filamu ioneshwe mtu anaiba mali ya umma halafu baadaye inaonekana ametajirika, maisha yake yanamekuwa mazuri, anaendelea na maisha yake. Uta-entertain watu wengi kufikiria kuiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani filamu ioneshe mtu anatumia dawa za kulevya halafu ionekane huyu amekuwa mchezaji bora mpaka akapata tuzo kwa sababu alikuwa anatumia dawa za kulevya. Lakini tunategemea hiyo filamu itakapoonesha mtu iruhusiwe kuonesha mtu anatumia dawa za kulevya, lakini matokeo ya mwisho ya filamu hiyo yaoneshe jinsi alivyoathirika na ambavyo amekuwa siyo wa msaada kwa Taifa. Kwa hiyo, hayo ndiyo mambo ambayo tumeyaelekeza katika maoni yetu kwenye Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo vilevile tuliyaona ambayo umeyaeleza hapa kidogo, juu ya utungaji wa kanuni, sheria mama inatoa loophole kwamba Waziri mwenye dhamana atatunga kanuni zinazosimamia sheria hii. Sasa anapokwenda kutunga zile kanuni unakuta kwenye kanuni kule kuna sehemu inasema, katika jambo hili uamuzi wa Waziri utakuwa wa mwisho. Tukasema hapana, lazima useme kwamba asiyeridhika atakwenda mahakamani, Mahakama ndiyo kiwe chombo cha mwisho cha kuamua juu ya watu. Usiseme uamuzi wa Waziri katika jambo hili utakuwa wa mwisho. Mambo hayo nayo tuliangalia katika baadhi ya sheria ndogo na tukafika mahali tukayaweka katika mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla mimi nirudie kusema kwamba nakushukuru sana kwa kunipanga kwenye Kamati hii. Bado ninaendelea kujifunza, lakini kwa ujumla ni kazi kubwa na muhimu, na niseme muda siku zote umekuwa hautoshi kwa sababu mpaka tunachambua sheria zote hizo unazosikia, bado kuna nyingi hazijafanyiwa uchambuzi, na bado kuna nyingi zinazolalamikiwa. (Makofi)

Kwa hiyo ni busara yako na Bunge lako kuona namna ya kuiongezea Kamati hii muda ili tusiendelee kuwa na sheria ndogo ambazo zinalalamikiwa huko mtaani. Ahsante sana. (Makofi)